Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Joseph Zacharius Kamonga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ludewa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Ludewa inaiomba sana Serikali kuzifungua kata nne ambazo hazifikiki kabisa kwa gari. Kata hizo ni Lifuma, Makonde, Kilondo na Lumbila ambazo zipo kandokando mwa Ziwa Nyasa ambako hata meli tuliyoitegemea kwa muda mrefu haifanyi kazi. Wilaya imeanzishwa mwaka 1975 na Wabunge tisa walionitangulia wameomba sana jambo hili pasipo mafanikio. Sasa wakati umefika Serikali iwahurumie wananchi wa maeneo haya na ipeleke fedha za kutosha ili barabara za maeneo hayo ziweze kupitika kwa magari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, tunaomba sana TARURA makao makuu itume wahandisi wake ili kujionea changamoto hii na kushauri njia nzuri ya kuondoa kero ya kukosekana kwa barabara kwenye kata hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Mkoa wa Njombe kupitia Wilaya ya Ludewa wanategemea sana huduma za matibabu na kuokoa maisha yao Hospitali ya Peramiho. Ili kufika hospitali hii iliyoko Mkoa wa Ruvuma, wananchi wanaiomba sana Serikali kutoa fedha za kujenga daraja kwenye Mto Ruhuhu eneo la Igugu ili kuunganisha Kata ya Ibumi iliyoko Wilaya ya Ludewa, Mkoa wa Njombe na Kata ya Itumbandiosi iliyoko Wilaya ya Mbinga Mkoa wa Ruvuma. Hii itaongeza sana fursa za kiuchumi kwa wananchi wa maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kata za Madilu, Ludewa, Lupingu, Lugarawa, Luana, Ludende, Mkongobaki zimekamilisha maboma ya jengo la utawala ya vituo vya afya hadi hatua ya uezekaji na upigaji ripu kwa kutumia nguvu za wananchi hivyo wanaiomba Ofisi ya Rais - TAMISEMI kutembelea maeneo haya ili kutoa msaada wa umaliziaji na kutoa maelekezo mahususi kwa Halmashauri kuelekeza mapato yake ya ndani kwa awamu kwa ajili ya umaliziaji wa vituo hivyo vya afya ili jasho la wananchi lisipotee bure na tusiwavunje moyo wa kushiriki katika kujitafutia maendeleo yao na ya nchi yao.