Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze mchango wangu kwa kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa uhai. Pia nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa namna anavyoliongoza Taifa letu kwa weledi na umahiri mkubwa sana. Niendelee kumwombea kwa Allah ampe umri mrefu wenye manufaa. Nimpongeze pia Mheshimiwa Waziri na wasaidizi wake wote wawili, kwa kazi kubwa ya kumsaidia Mheshimiwa Rais na mwisho niwapongezi watendaji wote kwenye Wizara hii wakiongozwa na Katibu Mkuu Ndugu yetu Profesa Shemdoe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi leo mchango wangu utajikita sana kwenye kushukuru na kushauri katika baadhi ya mambo muhimu na nianze kwa kumshukuru sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuiheshimisha kwa kutupatia fedha nyingi za miradi mbalimbali katika sekta ya afya, elimu, maji na miundombinu ya barabara. Halmashauri ya Liwale haijawahi kupata fedha za miradi mikubwa kama mwaka huu, tangu nchi hii imepata uhuru. Niseme ahsante sana kwa Mheshimiwa Rais, ahsante sana kwa Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuboresha utendaji na weledi kwenye Halmashauri zetu nchini, watendaji hawa wasikae muda mrefu zaidi vituoni kwao, kwani wapo watumishi wanazaidi ya miaka kumi katika kituo kimoja. Jambo linalowafanya wafanye kazi kwa mazoea na pengine kushirikiana na wapiga deal na wala rushwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Serikali inapeleka fedha nyingi kwenye Halmashauri zetu, na kwa kuwa wasimamizi wakuu wa fedha ni pamoja na Wabunge na Madiwani, hivyo basi ni muhimu sasa kuwaongezea nyenzo za kufanyia kazi Madiwani wetu ikiwa pamoja na maslahi yao. Madiwani wanafanya kazi kubwa sana na katika mazingira magumu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Liwale ina uhaba mkubwa sana wa vitendea kazi ikiwemo magari, ziko idara ambazo hazijawahi kuwa na gari, kwa mfano Idara ya Mipango, Idara ya Misitu, Idara ya Kilimo, Idara ya Mifugo, Idara ya Ukaguzi wa Ndani, na Idara zingine zina magari yaliyochoka, hizi ni Idara ya Afya, Idara ya Elimu, na Idara ya Uhasibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti,Halmashauri ya Liwale ina mtandao mkubwa sana wa barabara za vumbi na za changarawe, hivyo basi niiombe sana Serikali kutuongezea fedha za miradi ya barabara ili kuwezesha barabara hizo kupitika majira yote. Mtandao wa barabara za lami kwenye Halmashauri yetu una jumla ya kilometa 1.8 tu. Hivyo naiomba sana Serikali kutuongezea mtandao wa barabara za lami katika mji wa Liwale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la wanyama pori katika Wilaya ya Liwale ni janga kubwa sana hasa ukizingatia Wilaya hii inapakana na Hifadhi ya Selous. Madhara yanayotokana na uwepo wa wanyama hawa ni makubwa sana kwa watu kujeruhiwa na mazao yao kuliwa na wanyamapori. Mimi naishauri Serikali kuweka askari wa wanyama pori kwenye kila kata zinazopakana na hifadhi ili kusaidia ulinzi katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mara nyingine tena leo naomba kuongeza mchango wangu kwa Wizara hii kwa kushauri mambo yafuatayo; Wizara ione umuhimu wa kununua vifaa (mitambo) vya kuiwezesha TARURA kuweza kuzifanyia matengenezo madogo barabara zake hasa pale barabara za udongo zinapohitaji japo kufukia mashimo tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkaguzi wa Ndani wa Halmashauri aondolewe kwenye Ofisi ya Mkurugenzi wa Halmashauri kwa sababu si vyema mkaguzi akamkagua bosi wake, kwani Mkurungenzi kwa kazi hii ni kama mwajiri wake. Kama kwenye Idara ya Elimu wasimamia ubora wa elimu wana ofisi yao inashindikanaje kwa mtu huyo muhimu ambaye ni jicho la Halmashauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Liwale kata zake zote zina barabara kuelekea Wilayani, lakini ni kata chache sana zilizounganishwa kwa barabara hata za udongo hivyo kuifanya jiografia ya Halmashauri hii kuwa ni ngumu sana. Hivyo naiomba Serikali kupitia TARURA itusaidie kuzifungua barabara zinazounganisha kata kwa kata ili kurahisisha mawasiliano.

Mheshimiwa Mwenyekiti,suala la watumishi kukaa muda mrefu sana kituo kimoja linapunguza tija na weledi wa watumishi hao. Mfano mimi kwenye Halmashauri yangu wako wakuu wa idara wana miaka zaidi ya kumi na tano, kama vile Idara ya Misitu, Kilimo na Mipango. Watumishi wa idara hizi ni changamoto sana kwenye Halmashauri yangu. Naiomba Serikali kuhamisha watumishi hawa kwa maslahi ya Halmashauri yetu.