Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze moja kwa moja kwa kumpongeza sana Waziri wetu Mheshimiwa Innocent Bashungwa pamoja na Manaibu wake wawili Mheshimiwa Ernest Silinde na Mheshimiwa Dkt. Dugange kwa kazi nzuri na kubwa wanaoifanyia hii nchi yetu. Ofisi ya Rais TAMISEMI hii Wizara wanayoiongoza hawa ndugu zetu ni ofisi ambayo inatoa huduma kubwa sana katika nchi yetu, inafanya kazi ambazo zinagusa maisha ya wananchi moja kwa moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo ndiyo sababu wamepata bajeti kubwa kwenye bajeti hii ya 2022/2023 watapata trilioni 8.77 ambayo ni sawa na asilimia 21 ya bajeti yote ya nchi hii. Kwa hiyo, ukweli vijana chapeni kazi. Niwapongeze pia Katibu Mkuu, na Manaibu Makatibu Wakuu kwa kazi nzuri wanayoifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende moja kwa moja kwenye hoja zangu za leo na nitachangia kwenye sekta ya afya kwenye Jimbo langu barabara na elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa Bungeni nimekuwa ninasimama mara nyingi nikiwa na agenda ya kuiomba Serikali tujengewe hospitali ya Wilaya na nichukue fursa hii rasmi kuishukuru sana Serikali kwa sababu tayari wameshatenga shilingi milioni 500 na kazi ya ujenzi wa hospitali ya Wilaya kule kwenye Jimbo langu Moshi DC imeshaanza, kwa hiyo naishukuru sana Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ya pekee nimshukuru sana Mkurugenzi wa Maendeleo wa Moshi DC huyu alikuwa very fair alipeleka barua Kata zote 32 za Halmashauri yetu walioleta barua yenye vigezo wamechagua Kata mbili ambazo zilikidhi vigezo vya kujenga Hospitali ya Wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hospitali hii inajengwa kwenye Kata ya Mabogini na tunaishukuru sana Serikali. Pamoja na shukrani zangu kwa Serikali bado niseme tu kwenye Jimbo la Moshi Vijijini tunachangamoto kubwa sana ya miundombinu ya vituo vya afya. Katika Kata zangu 16 ni Kata Tatu tu zina vituo vya afya na kuna upungufu kama asilimia 81 hivi kwamba asilimia 81 ya maeneo hayana vituo vya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamuomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja ku-summarize hapa, nimeomba vituo vya afya vya kimkakati, nilikuwa nimeomba nijengewe kituo cha afya kwenye Kata ya Arusha Chini, Kata ya Old Moshi Mashariki na Kata ya Kibosho Kirima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika vituo 252 ambavyo unajenga nchi nzima Mheshimiwa Waziri haukunipa hata kimoja kwa hiyo naomba unifikirie kama kutakuwepo na namna hizi Kata zangu za kimkakati hii asilimia 81 ili ipungue kidogo na sisi tupandepande wananchi wangu wafurahi. Katika Jimbo langu pia kuna zahanati ambazo zimeshakidhi vigezo vya kuwa vituo vya afya niombe kuna zahanati ya Lima ambayo ipo Kibosho kati, hii ilijengwa na msamaria mwema akaweka karibia kila kitu kipo kwa hiyo tunaomba ipandishwe hadhi iwe kituo cha afya ili kupunguza huu ukakasi wa vituo vya afya ambao uko kwenye Jimbo langu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna zahanati nyingine kwenye Kata nyingine kwa mfano zahanati ya Shiha katika Kata ya Kimochi, zahanati ya Kindi au tunaita Mary Bennett Clinic na zahanati ya Uru Kaskazini katika Kata ya Uru kaskazini hizi zipo tayari kupandishwa kuwa vituo vya afya, tunaomba Wizara itusaidie ili haya maeneo nayo yapandishwe hadhi tupate vituo vya afya vya kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu wa pili ni kuhusu barabara. Kwanza niishukuru sana Serikali ya Mama Samia kwa kutupatia Bilioni 1.5 kufanya marekebisho ya barabara za Moshi Vijijini ambazo zina changamoto kubwa sana wakati wa mvua, pamoja na kupata fedha hizi lakini bado kuna changamoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe Mheshimiwa Waziri na timu yote kwamba waangalie kwa namna ya pekee zile pesa ambazo mmeleta mpaka sasa hivi mikataba ilisainiwa tangu Desemba lakini mpaka sasa hivi wamefanya grading tu katika barabara kama sita hivi ambazo tulipangiwa zitengenezwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tunaomba mfuatilie tuhakikishe kwamba zinakamilika kwa kiwango cha changarawe kama tulivyopewa ahadi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama alivyosema Mheshimiwa Noah Lemburis…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Prof. Patrick Alois Ndakidemi kwa mchango wako.

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)