Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

Hon. Prof. Joyce Lazaro Ndalichako

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kasulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia hoja iliyoko mezani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa kuipongeza Kamati kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya na niseme kwamba naunga mkono hoja za Kamati zote mbili, Kamati ya Katiba na Sheria pamoja na Kamati ya Sheria Ndogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati imetoa ushauri katika maeneo mbalimbali, lakini na Waheshimiwa Wabunge pia ambao wamechangia nao wametoa maoni yao. Kimsingi kama nilivyosema Serikali imepokea maoni yote na tunaunga mkono maazimio ambayo yametolewa na hizi Kamati na tunapenda kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge kwamba Serikali itayafanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumze kwa kifupi katika baadhi ya maeneo; nianze na kuhusu Mfuko wa Maendeleo ya Vijana. Taarifa inaonesha kwamba hadi kufikia mwezi Februari, 2022 Serikali ilikuwa imetoa kiasi cha shilingi milioni 205 kati ya shilingi bilioni moja ambazo zilikuwa zimetengwa. Naomba nichukue nafasi hi kuriarifu Bunge lako tukufu hadi kufikia Juni, 2022 fedha zote shilingi bilioni moja ambazo zilikuwa zimetengwa kwa ajili ya Mfuko wa Maendeleo ya Jamii zilikuwa tayari zimekopeshwa kwa walengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la utoaji wa elimu, hilo tutalizingatia na nichukue nafasi hii kuwafahamisha Vijana kwamba mwongozo wa namna ya kupata mikopo unapatikana katika halmashauri zote nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwongozo huu tumeuboresha; kwanza, tumeongeza kiwango cha juu cha kutoa mkopo kutoka shilingi milioni 10 hadi shilingi milioni 50; lakini pia tumelegeza masharti kwamba mtu anaweza kukopa kama kikundi au anaweza kukopa kama mtu mmoja, mmoja. Kwa hiuyo, yote hiyo ni kuwawezesha vijana ambao ni wabunifu, mwingine anaweza akawa na ubunifu wa peke yake ambapo ukimlazimisha mpaka awe na kikundi inakuwa ni vigumu kukidhi hayo masharti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo Waheshimiwa Wabunge pamoja na Kamati wamelizungumzia ni suala la mwongozo wa utekelezaji wa ujumuishaji na uimarishwaji wa huduma kwa watu wenye ulemavu. Serikali imepokea maoni kwamba upo umuhimu wa kutoa elimu na kuhakikisha kwamba taasisi zote za Serikali na zisizo za Serikali zinatekeleza kikamilifu mwongozo wa utoaji wa huduma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la upatikanaji wa takwimu, ni suala la msingi na Sensa ya Watu na Makazi iliyofanyika mwaka 2022 iliweka kipengele mahususi kwa ajili ya kupata takwimu za watu wenye ulemavu hapa nchini. Tunaamini kwamba Taasisi ya Takwimu ya Taifa (NBS) ikikamilisha uchakati wa takwimu za sensa tutapata idadi kamili ya watu wenye ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia tunashirikiana na Ofisi ya Rais, TAMISEMI, tunaandaa mfumo ambao utakuwa ni endelevu ambao tutakuwa tunaweka taarifa za watu wenye ulemavu kama Kamati ilivyoshauri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo ningependa kuzungumzia ni Sera ya Taifa ya Vijana. Kama nilivyosema maoni yote tumeyapitia lakini kwa taarifa tu, napenda niliarifu Bunge lako kwamba mchakato wa kufanya mapitio ya Sera ya Taifa ya Vijana unaendelea vizuri na tumefikia sasa hatua ya kupokea maoni kutoka kwa wadau. Kwa hiyo, tutasimamia na kuhakikisha kwamba hadi kufikia Disemba yaani mpaka tutakapokuwa tunakuja kutoa utekelezaji wa maazimio haya itakuwa imetekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda naomba nikushukuru tena kwa nafasi na niseme kwamba naunga mkono maazimio na kuhakikisha kwamba tutayasimamia kuhakikisha utekelezaji wake, ahsante sana. (Makofi)