Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

Hon. Edwin Enosy Swalle

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lupembe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia kwenye taarifa za Kamati ya Katiba na Sheria pamoja na Kamati ya Sheria Ndogo.

Kwanza na mimi niungane na Wajumbe wenzangu ambao wameshachangia, kuwapongeza sana Wenyeviti wa Kamati hizi zote mbili kwa kazi nzuri ambayo wamefanya kuwasilisha hizi mada ndani ya Bunge lako tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo la pili niseme pia kwamba ninaunga mkono maazimio yote ya Kamati zote mbili ambazo Wenyeviti wamewasilisha ndani ya Bunge lako tukufu. Mimi nitachangia maeneo yote mawili, nikianza na sehemu ya Kamati ya Sheria Ndogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tangu asubuhi tumesikia ndani ya Bunge lako tukufu Wabunge wengi ambao wamechangia hapa wameonesha dosari mbalimbali kwenye sheria ndogo ambazo nyingi zinatungwa na Mamlaka zetu za Serikali za Mitaa, Wizara mbalimbali na mamlaka mbalimbali za nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo tumesema hapa ndani, mamlaka ya kutunga sheria zote za nchi hii ni kazi ya Bunge na Katiba imesema vizuri sana, imesema mamlaka yote, imetumia neno yote kwa maana kwamba Bunge hili ndio lenye mamlaka ya utunzi wa sheria zote za nchi hii. Kwa hiyo, hata kama kuna sheria ndogo kwenye Manispaa, kwenye Majiji au kwenye Halmashauri, kama inaumiza watu maana yake Bunge hili tunawajibika kuirekebisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana yake nini? Wajumbe wa Kamati ya Sheria Ndogo kwenye Taarifa ya Kamati hapa, imetolewa wazi kwamba yako maazimio ya Bunge yaliyotolewa ya Mkutano wa Sita na wa Saba, lakini mpaka leo hayajatekelezwa na sheria hizi bado ziko mtaani.

Nilikuwa naomba kutoa rai, kama ambavyo Wabunge wamesema kwamba kwa sababu mamlaka ya utunzi wa sheria hizi ni kazi ya Bunge haitegemewi mamlaka nyingine yoyote ya Serikali au Halmashauri zetu za Mitaa kuendelea kupuuza maazimio ya Bunge hili ambayo sisi tumeazimia mambo yafanyiwe marekebisho, na tukiruhusu hili Bunge hili tutakuwa hatufanyi wajibu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo la pili ambalo naomba kuchangia hapa, napenda kusema kwamba pia sisi kama Bunge tunapotunga sheria mbalimbali kwa ajili ya nchi yetu tunaunga mkono kazi nzuri ambayo Mheshimiwa Rais anaifanya kwa ajili ya nchi yetu. Rais wetu tangu ameingia madarakani kati ya maeneo muhimu anayofanyia kazi ni kurekebisha mifumo ya sheria ili watu wetu wapate uhuru zaidi, ili watu wetu waishi kwa amani katika maeneo yao. Na Mheshimiwa Rais juzi wakati anaongea na Tume ya Kurekebisha Haki Jinai aliongea maneno yafuatayo na naomba kumnukuu Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Mheshimiwa Rais amesema; “Hakuna kitu kibaya kukichepusha duniani kama kuchepusha haki ya mtu.” (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Rais anaamini kwamba kuchezea haki za wananchi ni kitu kibaya sana, na sisi kama Bunge na mimi kwa maoni yangu ninaamini, haki za wananchi zinaweza kuchepushwa katika maeneo mawili; sehemu ya kwanza zinaweza kuchepushwa na mamlaka ambazo zinasimamia haki za wananchi wetu zikiwemo Mahakama, vyombo vya polisi, TAKUKURU na kadhalika; lakini eneo la pili linaloweza kuchepusha haki za wananchi ni sisi Bunge kutokutunga sheria bora za kusimamia wananchi wetu. (Makofi)

Kwa hiyo, naliomba Bunge lako tukufu tutumie mamlaka yetu vizuri ya kutunga sheria, ziwe na tija, zisaidie kuboresha huduma za wananchi badala ya kuweka ugumu kwenye maeneo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo la pili, naomba nichangie mahususi kwa ajili ya Law School, kabla sijaenda mbele kwanza ni-declare interest kwamba mimi nimesoma Law School ya Tanzania, na ili kuweka mchango wangu vizuri, mimi nimesoma Law School na nilifaulu katika first sitting, sikufeli kama wanafunzi wale wengine. Nataka huu mchango ukae vizuri, kwa hiyo, ninapochangia kuhusu Law School sichangii kuipaka matope nachangia kwa ajili ya kuboresha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati yetu ya Katiba na Sheria, kwenye maoni yao, wameshauri kwamba ili kupata wanafunzi bora wa sheria ni vema kuwe kuna mitihani ya kuingilia kusoma Law School ya Tanzania. Tafsiri yake ni kwamba, wale ambao watafeli mitihani ya kuingia Law School hawatakwenda kusoma Law School.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakubaliana na azimio hilo, lakini mimi nakwenda mbali zaidi na Waziri wa Katiba yuko hapa ndani, naomba hili jambo alisikie na alifanyie kazi. Wanafunzi wengi wa sheria Tanzania hivi sasa wamekuwa kama watoto yatima, degree za sheria nchini sasa hivi mwanafunzi akikaa darasani miaka minne, miaka mitatu, ni kama hajasoma shule kwa sababu matangazo yote ya Serikali huwezi kupata ajira nchi hii sasa hivi kama hujasoma Law School. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tafsiri yake ni nini? Tafsiri yake ni kwamba kusoma Law School Tanzania imekuwa ni jambo la lazima, suala ambalo sio sawa na hii sio haki. Mwanafunzi aliyeuza ng’ombe, ameuza mahindi, amejibana akasoma degree miaka minne, miaka mitatu, unamwambia bila Law School hupati ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naamini kwa kuwa Katiba yetu, Ibara ya 22 inasema kila raia wa Tanzania ana haki ya kufanya kazi katika nchi hii, ninaliomba Bunge lako tukufu na Waziri wa Katiba na Sheria, suala la kusoma Law School liwe ni optional, sio lazima. Sio kila mwanasheria ana mpango wa kuwa wakili kama mimi, sio kila mwanasheria ana mpango wa kuwa kwenye mambo haya. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naunga mkono hoja na nakushukuru sana. (Makofi)