Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

Hon. Luhaga Joelson Mpina

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisesa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

MHE LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa nafasi hii ili na mimi niweze kuchangia Taarifa ya hizi Kamati mbili; Kamati ya Katiba na Sheria, Kamati ya Sheria Ndogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ujumla hoja zote za Kamati naziunga mkono japo kuna baadhi ya maeneo taongezea ushauri wa Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ni madai na usuluhishi; Serikali yetu imekuwa ikiendesha kesi mbalimbali za madai na usuluhishi Kitaifa na Kimataifa na tulipewa taarifa kwamba na labda kwa kuanzia mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Katiba na Sheria na tulipewa taarifa kwamba Serikali imeweza kuokoa shilingi trilioni 13.33 katika haya mashahuri ya madai na usuluhishi yaliyokuwa yakiendeshwa Kitaifa na Kimataifa. Lakini kiwango hicho ni kikubwa, lakini pia ni cha kupongezwa kwa Serikali kuweza kuokoa matrilioni hayo ya shilingi ya Watanzania katika madai na usuluhishi yaliyokuwa yakiendeshwa sehemu mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa changamoto moja tu; kiwango tu ni cha fedha, lakini bango kitita sasa linaloeleza kwa kina ni kesi gani, zilifunguliwa mwaka gani, kwa mkataba gani, juu ya nani, tulishtakiwa na kampuni gani mpaka tukaokoa hizi fedha ili tuweze kujua kwanza tuliingiaje kwenye mikataba hiyo na mpaka leo tumeendesha mashauri ya madai na mashauri ya usuluhishi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili; Serikali haijatuambia katika kipindi hiki cha ripoti hii wakati inawasilishwa ni mashauri mangapi ya madai na usuluhishi ambayo Serikali imeshindwa? Na yalikuwa kwenye maeneo gani? Tulikuwa tunashtakiwa kwenye nini? Ni fedha kiasi gani tulicholipa mpaka sasa hivi? Hii itatuwezesha Wabunge kufahamu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haiwezekani Bunge hili likawa linaletewa tu tumeshindwa kesi Mahakamani, mmeshindwa kesi hiyo juu ya nini? Mmeshindwaje shindwaje na lazima uwepo utaratibu mzuri wakuwa wanawasilisha haya mashauri kama sasa hivi tunavyozungumza wewe unajua kwamba ndege yetu moja ya Airbus imekamatwa juu ya mkataba mbovu, imeshikiliwa kwa sababu tunadaiwa. Sasa hilo nalo tunapaswa tuelezwe hatima ya hiyo ndege yetu mpaka sasa hivi ikoje?

MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Kuhusu Utaratibu.

MWENYEKITI: Kuhusu Utaratibu, nimekuona Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

KUHUSU UTARATIBU

MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe taarifa kwa mujibu wa Kanuni ya 71; shauri analoliongelea Mheshimiwa Luhaga Mpina kuhusu kukamatwa kwa ndege bado lipo Mahakamani kwenye Mahakama ya Usuluhishi wa Migogoro ya Kiuwekezaji. Kwa hiyo, kwa mujibu wa Kanuni ya 71 ni shauri ambalo haliwezi kuwa na sifa ya kujadiliwa kwa sasa.

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Mwenyekiti unilindie muda wangu. Sijadili, lakini Bunge hili linalo haki ya kupewa taarifa kama alivyoisema sasa hivi ambayo haina siri yoyote, tujue, unaambiwa tu ndege imekatwa, ndege imekamatwa kwa jambo gani? (Makofi)

Kwa hiyo, taarifa ni muhimu sana na yeye kama Mwanasheria Mkuu wa Serikali alitakiwa kuleta kwenye Kamati ya Katiba na Sheria ikaelewa nini kinachoendelea juu ya mambo hayo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, na usiri huu utakuja kushtukia mambo yanatokea mengine ndege imetaifishwa, ndege imefanya nini? Tuwe tunapeana taarifa juu ya mambo haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na tatizo na changamoto hapa ya muda ninachoweza kusema tu kuanzia sasa hivi tuongeze azimio moja la kuitaka Serikali mashauri yote ambayo Serikali imeshindwa Mahakamani wayalete kwenye Kamati husika, tujue wameshindwa kwenye jambo gani, kabla ya kulipa hizo fedha za Watanzania. Hatuwezi kuendelea kulipa fedha za Watanzania katika mchezo, mchezo tu ambao baadhi ya watumishi wa umma wanaenda kunufaika na hizo kesi na ndiyo maana hata Mheshimiwa Rais amelalamikia sana juu ya jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, marekebisho ya Katiba na upatikanaji wa Katiba mpya; Mheshimiwa Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan alitoa mwongozo kuanzia Juni, 2022 kuhusiana na kuanza mchakato wa maandalizi ya marekebisho ya Katiba tuliyonayo, lakini pia hata mapendekezo ya Katiba mpya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo mpaka sasa hivi Wizara ya Katiba na Sheria na Mwanasheria Mkuu wa Serikali hakuna mwongozo wowote, hakuna deadline yoyote, hakuna utafiti wowote, hakuna jambo hili mpaka sasa hivi toka kiongozi wa nchi atoe maelekezo leo ni miezi saba halijawekwa mahala popote kwa hiyo huwezi hata kuona linafanyika kazi kwa namna gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ninafikiri na ninaungana kabisa na Mheshimiwa Rais kwamba muda muafaka wa kuangalia Katiba yetu na moja ya eneo ambalo ni muhimu sana ni kwamba Katiba tuliyonayo haina nguvu za kutosha kulinda na kusimamia fedha na rasilimali za umma kwa sasa na ndiyo maana sasa hivi Wabunge wote hapa walivyokuwa wakichangia Kamati hizi za kifedha wote wamelalamika fedha zimeibiwa, fedha zimeliwa, kila mtu Taarifa za CAG, Taarifa ya TAKUKURU, Taarifa ya PPRA zote watu wanalalamikia juu ya wizi wa fedha lakini wizi wa fedha ambao hauna dawa inawezekana kabisa tobo kubwa lipo kwenye Katiba ndiyo maana hatujaweza kutatua tatizo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, matobo unaweza kuyaona, Taarifa ya CAG hapa Bungeni, Taarifa ya PPRA na Taarifa ya TAKUKURU hazipati muda wa kutosha kujadiliwa na Wabunge juu ya hatua mahususi zinazochukuliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia usiri wa mikataba; kuna usiri mkubwa sana wa mikataba, matokeo yake usiri huu wa mikataba ndiyo imekuwa tobo la kusababisha fedha za Watanzania kupotea. Hapa kuna mkataba ule wa SGR kipande cha Tabora – Kigoma ambao tayari una mashaka ya shilingi trilioni 1.7 malipo ambayo yanatarajiwa kwenda kulipwa yenye mashaka, lakini tuna Mkataba wa Bwawa la Mwalimu Nyerere ambao mpaka sasa hivi haujulikani mradi huu utaisha lini, tarehe haijulikani, lakini hata hatma ya Watanzania fine ya shilingi trilioni 1.3 anayotakiwa kuilipa mkandarasi haijulikani na CSR ya shilingi bilioni 260 na yenyewe haijulikani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna mikataba kama ya TRAT na TRAB, CAG amesema tulipwe, Waziri wa Fedha anasema tusilipwe. (Makofi)

Sasa mpaka nayo haina hukumu hiyo na mikataba mingine yote ambayo inaingiwa na Serikali kwa siri. Tukatae mambo haya kwa kumuunga mkono Mheshimiwa Rais kuziba hili tobo kwenye Katiba mpya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hapa Bungeni Waziri wa Fedha…

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa, nani anatoa Taarifa?

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Mwenyekiti, unitunzie muda wangu.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Waziri wa Katiba na Sheria, Dkt. Ndumbaro, Taarifa.

T A A R I F A

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, naomba nimpe taarifa mzungumzaji kwamba TRAB na TRAT sio mikataba bali ni vyombo vya utatuzi wa migogoro ya kodi. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mpina, unapokea taarifa?

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa yake. Ni hukumu ya TRAT na TRAB. Nilimaanisha hukumu ya TRAT na TRAB ambayo CAG ameshathibitisha Watanzania tunaweza kulipwa shilingi trilioni 5.595, lakini mpaka sasa hivi hakuna hatima yake na hata tukihoji Wabunge mnakaliwa kimya, hamjibiwi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mikataba mingine iliyoingiwa na Serikali mingine inaingiwa kwa usiri, mingine hatujui hata tumeingia mkataba ambao una madhara gani kwa Watanzania. Hili tobo hili ni lazima tulizibe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa katika Bunge usimamizi dhaifu wa sheria, Waziri wa Fedha alisimama hapa akasema, nimalizie lingine nimeongea tena na ndugu yangu jirani kwamba mwaka juzi reserve zimeshuka kutoka dola bilioni 6,000 zimeshuka zikawa bilioni 4,500. Jamani masomo ya uchumi ni sayansi, narudi tena twendeni tufuatilie kwa makini reserve zina-build vipi. Reserve zilizoongezeka zilikuwa ni trilioni 1.3 tumetoa IMF na ndio zikaongezeka reserve.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza, toka nchi hii ianze hatujawahi kuwa na akiba ya fedha za kigeni bilioni 6,000 wala hatujawahi kuwa na akiba ya fedha za kigeni reserve bilioni 4,500. Kwa hiyo, haya ni maneno ya uongo, hatujawahi…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)