Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022

Hon. Simon Songe Lusengekile

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Busega

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022

MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami nichangie taarifa hizi za Kamati Tatu, nizipongeze sana Kamati kwa kazi kubwa ambazo zimefanya kutuletea taarifa ambayo inaenda kutufungua macho nini kinafanyika kwenye Kamati hizi Tatu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa masikitiko makubwa sana katika taasisi zetu hizi mbili TANROADS pamoja na TAA katika muingiliano wa mamalaka ya utendaji wa kazi, kuna tatizo kubwa ambalo 2016 Mwezi Agosti ujenzi na upanuzi wa viwanja vya ndege ulihamishwa kutoka TAA kwenda TANROADS.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeona matatizo makubwa viwanja wana-delay kufanya kazi lakini bado haitoshi wanaingiliana katika maamuzi. Nikupe mifano michache, mpaka sasahivi tunavyozungumza Kiwanja cha Ndege cha Shinyanga, Tabora, Sumbawanga hakijajengwa kwa sababu ya muingiliano wa majukumu kati ya TAA pamoja na TANROADS nini kilifanyika hapa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mfadhili aliyekuwa anatuletea fedha kwa ajili ya ujenzi wa viwanja hivi alifanya due-diligence pamoja na TAA mwaka 2017 lakini baadae alivyotaka kuleta fedha akagundua kwamba tayari Mamlaka ya Ujenzi wa Viwanja Vya Ndege umehama kutoka TAA kwenda TANROADS akakataa kuleta fedha na ujenzi haukuendelea, nini kilifanyika hapa? Wamekaa zaidi ya miezi 30 hamna kilichoendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninamshukuru sana Mheshimiwa Rais ameendelea na mazungumzo, mwaka jana Mwezi Februari, wameleta Dola za Kimarekani Million 12 kwa ajili ya Ujenzi wa Viwanja hivi, kwa masikitiko makubwa kwa sababu ya mwingiliano huu mpaka sasa hivi hakuna kinachoendelea na fedha zipo kwa Serikali yetu, ni masikitiko makubwa sana fedha hizi ni za mkopo walipa kodi watakuja kurudisha mkopo huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo mpaka sasa hamna kinachoendelea itafika sehemu tutalipa riba ya kutokutumia fedha ambazo zimekopeswa. Mpaka sasa hivi Mkandarasi aliyefanya quotations 2017 ameambiwa afanye implementations ya mradi naye amekataa amesema hawezi kwa sababu vitu vimepanda bei hawezi kufanya sasa hivi naye ameongeza bei. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, watu wako ofisini wamekaa, watu wanajadili ofisini zaidi ya miezi 11 wako ofisini wameshindwa kutoa maamuzi kwa ajili ya ujenzi wa Kiwanja cha Ndege Shinyanga, Tabora na Sumbawanga. Mheshimiwa Rais anafanya kazi kubwa sana katika Nchi yetu, lakini Watendaji wa Wizara wanamuangusha Rais kwa kutofanya maamuzi kwa wakati. Leo tuna Dola za Kimarekani Million 12 TANROADS hazijafanya kazi ni kwa sababu ya mwingiliano wa majukumu haya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo tunaomba sasa kama inawezekana tuamue kwa pamoja Wabunge turudishe Mamlaka ya Ujenzi wa Viwanja Ndege tutoe TANROADS tupeleke TAA ili kazi iweze kufanyika la sivyo tutakuwa tunazungumza viwanja havipanuliwi, hakuna kinachoweza kufanyika lakini mwingiliano huu utaona umetupa hasara ya Million 236 Kiwanja cha Ndege cha Dodoma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka jana walipanua wakaweka taa za solar kwa ajili ya kutua hizi ndege kubwa, lakini leo TAA zile taa ziliwekwa na TANROADS leo TAA wamekataa kwamba zile taa hazifai tena kwa sababu Mji wa Dodoma umepanuka sasa hawatatumia tena taa za solar wanaitaji taa za umeme Million 236 za walipa kodi zimepotea na sasa haiwezekani. Kwa nini? Kwasababu wanakati wanaweka hizi taa za solar hawakuwa na mawasiliano na kati ya TAA na TANROADS na fedha Million 236 za walipa kodi zimepotea kwa sababu ya Watendaji ambao hawana mawasiliano, hawawezi kufanya kazi zao kwa ajili ya kumsadia Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni lazima leo tuwe na maamuzi ili tuweze kuisaidia Serikali, hawa wote ambao wanasababisha hasara kwa Taifa hawa wote ambao wanasababisha hasara kwa nchi yetu wachukuliwe hatua ili iwe mifano kwa watu wengine kwa ajili ya kunusuru Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili ambalo nataka nichangie. Limechangiwa kidogo suala la riba katika miradi yetu. Leo nilikuwa natafakari hivi inawezekanaje Afisa Masuuli yeye anajisikiaje moyo wake anasaini vocha ya kupitisha malipo ya nyongeza ya kutokulipa kwa wakati kwa sababu amechelewa! Unapitisha voucher ya Milioni 100, unapitisha voucher ya Bilioni Moja unaenda kulipa kwa sababu wewe mwenyewe ulichelewa kumlipa Mkandarasi, haiwezekani leo Wabunge tuamue! Ni kwanini kila siku tunapiga kelele kwa sababu ya ucheleweshaji wa malipo? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ikiwezekana Bunge hili liamue sasa Wizara ya Fedha ituletee taarifa ya kutupatia sababu kwa nini wanachelewa kulipa Malipo kwa Wakandarasi na kuleta riba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano Daraja la Busisi wamechelewa siku 30 wamelipa riba ya milioni 58. TAA Bilioni 11 lakini Kiwanja cha Ndege cha Mwanza bilioni mbili. Sasa inawezekanaje Afisa Masuuli unasaini Vocha ya kulipa kwa sababu wewe mwenyewe ulichelewa na wewe uko ofisini haiwezekani! Ni lazima tutafakari tuisaidie nchi, ni lazima tutafakari tumsaidie Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Rais anafanya kazi kubwa, hawa Watendaji hawamsaidii. Leo Bunge tuamue ili tumsaidie Mheshimiwa Rais na wananchi wanamfurahia lakini kuna watu wanamuangusha. (Makofi)

Mheshimiwa Naiba Spika, nizungumze kidogo kwa ajili ya mifuko hii ya wakopeshaji ya wajasiliamali wadogo wadogo. Tumeletewa taarifa kwenye Kamati tuna Mifuko 52 na ilikaguliwa Mifuko 13, lakini nimekuja kugundua katika mikopo waliyotoa bilioni 90 kati ya hiyo bilioni 90, bilioni 50 ni mikopo chechefu haiwezi kukusanyika, inawezekanaje?

Haiwezekani watu wanakopeshwa na mwisho wa siku hawarejeshi! Tumegundua kwa sababu, gani? Ni kwa sababu, wanakopeshwa watu ambao hawana sifa, inafika sehemu wanashindwa kurejesha mikopo ile. Sasa haiwezekani! (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini eneo la pili kwenye hii mifuko; wamekopesha zaidi ya asilimia 72 kwa benki za biashara, jambo ambalo si lengo la mifuko hii. Lengo kubwa la mifuko hii ni kukopesha wajasiriamali wadogowadogo, lakini tumekuja kugundua zaidi ya asilimia 70 zinakopeshwa benki ambayo si lengo la mifuko hii, tunayo ya nini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mifuko hii imetengenezwa ili iawasaidie wajasiriamali wadogowadogo kule vijijini, lakini hawapati mikopo kwa sababu wanaokopeshwa si wale wanufaika; na ndiyo maana sasa tunakuwa na mikopo chechefu kwa sababu watu wameacha malengo na makusudi ya ile mikopo wameenda kwenye malengo ambayo hawakupanga kuyafanya. Ukiona hivi maana yake hatukujiandaa katika hili eneo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia tunayo mifuko mingi, 52, wote wanafanya kazi moja; na kwa sababu hawawasiliani, hamna sehemu wanaonana; leo Mheshimiwa Songe anakopa mfuko A, kesho akifulia kidogo anaenda kukopa B, keshokutwa akifulia kidogo anaenda kukopa C, mwisho wa siku anashindwa kurejesha.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tunaishauri Serikali, ifike mahali mifuko hii sasa iunganishwe iwe michache, badala ya 52 iwe hata minne ili iweze kuwasaidia wananchi wetu. Hata ikiwa inawezekana basi iweze kusomana ili kama umekopa sehemu A basi usipewe mkopo sehemu B, kwa sababu, hatimaye utashindwa kurejesha mikopo hii, ili iweze kuwasaidia wananchi wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo hili linatakiwa lichukuliwe hatua za haraka ili tuinusuru nchi yetu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)