Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022

Hon. Francis Kumba Ndulane

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia katika mjadala huu wa leo. Kwanza napenda nimpongeze CAG kwa kufanya kazi nzuri ya kukagua Halmashauri zetu katika ukaguzi maalum ambao ulifanyika mwezi Mei hadi Julai, mwaka 2021. Kwa hakika CAG ametufungua macho. Kama tafsiri halisi ilivyo, lile ni jicho letu sisi Wabunge na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa ujumla. Kwa hiyo, ameifanya kazi yake vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama walivyotangulia kuzungumza wazungumzaji wenzangu waliochangia hii taarifa ya LAAC. Kwa ujumla kuna madudu mengi sana yameonekana katika ule ukaguzi maalum uliofanyika mwaka 2021, lakini hatua hazijachukuliwa. Ukienda pale katika Halmashauri hizo nne ambazo zilifanyiwa ukaguzi maalum; Halmashauri ya Ubungo, Kigamboni, Ilemela pamoja na Iringa DC, kuna karibu Shilingi bilioni tisa ambazo zimevuja kutokana na miamala kufutwa kinyume cha utaratibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile, ukienda kwenye suala la ubadhirifu wa fedha za umma kutokana na matumizi ya fedha kabla ya kuzipeleka benki, yaani fedha mbichi, kuna shilingi milioni 858, Halmashauri nne tu.Kwa hiyo, kuna shida katika Halmashauri zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kilicho kibaya zaidi, pale katika Halmashauri ya Ilemela ule mfumo sijui ukoje! Kwa sababu imefikia hatua watumishi waliohama wamekuwa na wale ambao wamestaafu wamekuwa na access ya kuingia kwenye mifumo. Pia hii inaonesha namna gani mifumo yetu haiko vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ombi langu nilikuwa naiomba Wizara yetu ya TAMISEMI inapokuja na mfumo mpya wa TAUSI, baada ya kuachana na ule wa LGRCIS, izingatie suala la security ya hii mifumo. Inaonesha mifumo yetu haiko madhubuti kwenye security. Tusije tukarudia makosa. Haya makosa yaliyojitokeza yawe fundisho kwetu ili tunapotengeneza ile database ya Mfumo wa TAUSI, basi iwe madhubuti makini katika ku-trace makosa mbalimbali ambayo yatafanyika ikiwemo haya ya watu ambao wamehama au kustaafu kuweza kuingia.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo ningeomba wizara ya TAMISEMI ifanye kazi kwa karibu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia ningeiomba TAMISEMI ifanye kazi kwa karibu sana na hizo Halmashauri zetu, kuna wakati niliwahi kusema kwamba CAG anapofanya ukaguzi ni kama vile mvuvi ambaye anakuwa anavua kwa njia yile ya kokoro. Kwa hiyo, ndani ya zile hoja zinapotengenezwa unakuta kuna mapendekezo yanahitaji utekelezaji wa Wizara ya TAMISEMI nyingine Sekretariati za Mikoa, nyingine Halmashauri zenyewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama hakuna muunganiko mzuri wa kujibu hizi hoja tutaendelea kupigwa kila siku na mwisho wa siku hizi hoja zitabaki zinaelea hazijibiki. Kwa hiyo, ninaiomba TAMISEMI kwanza ichukue hatua dhidi ya wale wote waliohusika na hizi changamoto, kwa sababu imeonekana tangu mwaka juzi ukaguzi ulivyofanyika na hizi taarifa zikawasilishwa Wizara ya TAMISEMI na kule kwenye Halmashauri zetu mwezi Septemba hatua madhubuti hazijachukuliwa kuwadhibiti hawa Watumishi ambao wamefanya huu ubadhirifu. Hii inaonesha kwamba ni kwa namna gani TAMISEMI imetengeneza gap kati yake na Halmashauri zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ningeomba TAMISEMI tumieni nafasi yenu kwa sababu hizi hoja ni mtambuka, zingine zinahitaji utekelezaji wa moja kwa moja na TAMISEMI, kama haya masuala ya kinidhamu chukueni hatua na mchukue hatua haraka. Mna-premises nyingi hapa Dodoma, mnaweza mkaziita zile Halmashauri husika, mkakaa nazo mkajadili kwa pamoja ili hoja ambayo inahusika na TAMISEMI utekelezaji wake unatakiwa utekelezwe na TAMISEMI kama uchukuaji wa hatua zile za kinidhamu, basi chukueni hatua haraka ili kudhibiti vitendo hivi vya ubadhirifu wa fedha za Halmashauri.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunalia kila siku mapato ya Halmashauri ni madogo lakini udhibiti ukifanyika basi mapato yataongezeka. Security zikiongezeka kwenye mifumo yetu tutajikuta tayari mapato yetu yanaweza kulindwa na kuweza kutumika kwa ajili ya shughuli mbalimbali za maendeleo.

Mheshimiwa Naibu Spika. vilevile kumekuwa na changamoto kubwa kwenye manunuzi, imefika mahali kule kwa mfano kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Iringa, hospitali inajengwa vifaa vinapokelewa, vinaonekena vimezidi hata idadi ya vile vifaa vilivyokuwa vinatakiwa. Sasa hii inatokeaje? Ni ukosefu wa kuzingatia Kanuni na Sheria ya Manunuzi. Kwa hiyo, ninaiomba TAMISEMI pamoja na Sekretariati zichukue majukumu yake ya kuzilea hizi Halmashauri pia kuchukua hatua pale inapoonekana kwamba kuna shida.

Mheshimiwa Naibu Spika, pesa nyingi inakwenda kwenye manunuzi, matumizi ya fedha za Serikali sehemu kubwa inakwenda kwenye eneo la manunuzi, ndiyo maana nafikiri huyu CAG amezingatia sana hayo maeneo hayo muhimu, kwa hiyo niombe Serikali isimamie vizuri hizi Halmashauri ili hatua zichukuliwe kwenye maeneo yote ambayo yanaonekana taratibu hazifuatwi lakini kuna ukiukwaji mkubwa wa taratibu za mapato na mambo mengine ambayo yanafanyika kule kwenye Halmashauri ili kuondoa haya madudu.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya nasema naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)