Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022

Hon. Ng'wasi Damas Kamani

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022

MHE. NG'WASI D. KAMANI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kupata nafasi hii ya kuchangia katika ripoti za Kamati hizi tatu muhimu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu wa leo utajikita katika wizi, upotevu, ubadhirifu na ufujaji wa fedha katika halmashauri zetu. Mimi ni mjumbe wa Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa na katika moja ya majukumu ya Kamati yangu ni pamoja na kuangalia namna fedha zinavyotumika kuendesha miradi mbalimbali na kuleta maendeleo kwa wananchi katika halmashauri zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mengi ambayo yamesomwa kwenye ripoti yetu naomba tu ni-highlight machache. Kuna suala zima la kubadili miamala katika mfumo bila kufuata utaratibu na katika halmashauri ya Ubungo tuna hasara ya Shilingi Milioni 21.3; Kigamboni, Bilioni 10.8; Ilemela, Bilioni 8.7. Katika matumizi ya fedha mbichi; Ubungo tuna Milioni 196.3, Kigamboni Milioni 47, Ilemela milioni 627, lakini hii ni bila kuzungumzia fedha ambazo zimelipwa kwa mkandarasi bila kuwa ametoa ushahidi Milioni 356, fedha ambazo zimelipwa kwa kazi ambayo haijafanyika Ilemela Milioni 138 na Fedha ambayo imelipwa zaidi ya kiwango kilichokuwa kinadaiwa Milioni 237.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini nimeyataja haya? Nimeyataja ili Bunge lako Tukufu na wananchi wajue viwango vya fedha tunazozungumzia. Katika hizi halmashauri tatu tu ripoti yetu inaonesha ni zaidi ya Bilioni 20 zinaoneshwa kwenye ripoti ya CAG zina mashaka na hazijaeleweka namna ya matumizi yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, kinachoshangaza zaidi ni kwamba, watumishi wanaohusika katika wizi, ubadhirifu au uzembe huu wanafanyiwa yafuatayo: -

(i) Wanapewa barua za onyo;

(ii) Wanahamishwa kupeleka katika halmashauri zingine;

(iii) Wanaanza kufanyiwa uchunguzi na cha kushangaza zaidi baadhi ya watumishi bado wapo katika halmashauri wakati bado wanafanyiwa uchunguzi; na

(iv) Wengine wanapelekwa Polisi au TAKUKURU na hawa ni wachache, lakini bado haitoi justification kuwapeleka watumishi hawa Polisi au TAKUKURU kwa ajili ya uchunguzi kwa sababu ripoti ya CAG ina uzito wa kuweza kutumika kama ushahidi mahakamani. Kwa hiyo, maana yake hawa watu walitakiwa wafikishwe mahakamani na hatua zichukuliwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, inakuaje leo hii Mheshimiwa Rais anazunguka sehemu mbalimbali kutafuta fedha kuhakikisha wananchi wanaletewa maendeleo, fedha zinamwagwa kwenye halmashauri zetu ili watu tupate maendeleo. Fedha hizi tulitakiwa tuzione zina-reflect kwenye mzunguko wa fedha kwa wananchi, lakini hatulioni kwa sababu kuna uzembe, wizi na upotevu mkubwa unafanyika kwenye halmashauri zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine, humu Wabunge wengi sana kwenye simu zao wana soft cope za CV zimejaa watu wanaomba watafutiwe ajira, wana hard copy mafaili yamejaa wanaomba watafutiwe ajira. Hizi ajira zinatoka wapi kama fedha ambazo zinapelekwa kwenye halmashauri zetu kwenye jamii zetu zitumike kuleta maendeleo, kuzalisha ajira, kufanya uwekezaji zinaibiwa na zinaingia kwenye mifuko ya watu.

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Taarifa.

MHE. NG'WASI D. KAMANI: Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii darasa moja fedha zimeenda kwenye halmashauri zetu Milioni 20 kwa darasa moja, darasa la vioo la...

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa subiri kuna taarifa.

T A A R I F A

MHE. NICODEMUS H. MAGANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Napenda nimpe taarifa tu dada yangu mchango wake ni mzuri sana kwa kusisitiza kwa kweli Serikali, hawa waliothibitishwa na CAG ni majangili, ni majambazi wanatakiwa wakamatwe mara moja haraka, tena wakaishi mahabusu huko. Ahsante sana. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kamani, taarifa hiyo.

MHE. NG'WASI D. KAMANI: Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea taarifa hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii huko mitaani vijana wanakosa hata shilingi laki mbili ya kuanza kujiajiri kuanzisha kitu kidogo tu, lakini kuna watu kwenye halmashauri zetu wamejilipa pesa. Pesa ambazo hazina idadi wamejilipa na ikithibitika kwamba wameiba wanaambiwa warudishe taratibu kwa muda ambao haueleweki ni muda gani. Hii naiona kama ni mikopo ambayo mtu anaamua kujipa isiyo na riba, isiyo na muda siku akiamua kumaliza kulipa anajilipa. Hii sio haki na haikubaliki.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia sisi kama Wabunge, Madiwani na Mheshimiwa Rais hatutakubali mwaka 2025 tusulubiwe na wananchi kwa sababu hatujaweza kutatua changamoto zao, lakini fedha zilikuja na baadhi ya watu wali-mismanage fedha hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hapana, hapana, hapana, hatutakubali. Ninachoomba ushauri wangu, Serikali iangalie namna, ituletee mabadiliko ya Sheria katika Bunge hili na Wabunge najua ni wazalendo tutapitisha mabadiliko hayo, tuangalie upya mfumo wa uwajibikaji katika utumishi wa umma. Hatuwezi kuwa watu wanafanya makosa kama haya, viwango vikubwa vya fedha kama hivi tunaishia kuwapa onyo au kuwahamisha hapana. Kuna vijana wengi sana mtaani ambao wangeweza kufanya kazi hizi, ni wazalendo basi tuwaondoe watu hawa tuwape wale vijana kazi wafanye.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikupe mfano mdogo, leo hii tuna project ya vijana chini ya Wizara ya Kilimo, building a better tomorrow imepewa bilioni tatu tu kwa hatua ya mwanzo ya kuandaa hekari laki na sitini kutengeneza miundombinu kwa ajili ya kuwaweka vijana waanze kufanya kazi. Kama Shilingi Bilioni tatu inaweza kufanya kazi kwenye mikoa mitatu tu hizi Bilioni 20 tungepeka Tanzania nzima tungefanya nini kwa vijana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba wananchi wa kawaida kwenye Sheria zetu, The Penal Code, Section ya 265, mwananchi wa kawaida akikutwa na kosa la wizi regardless ya kiwango hata kama ni kuku, anapewa adhabu ya mpaka miaka saba kufungwa, lakini hawa watu wanaoiba kutumia numbers, wanaiba kutumia mifumo yetu, mabilioni ya fedha, tunawapa onyo na kuwahamisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, haikubaliki. Naomba sheria ije tuifanyie marekebisho na kama inashindikana, kusiwe na double standard; basi na wananchi wanaoiba nao tuishie kuwapa onyo au waishie tu kuwashauri ili nao wawe sawa na sisi. Vinginevyo nasema fedha ya umma lazima itumike kuleta maendeleo kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)