Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

Hon. Samweli Xaday Hhayuma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, kabla sijaanza kuchangia naunga mkono hoja za Kamati zetu zote mbili za Kudumu za Bunge.

Mheshimiwa Spika, Wabunge wenzangu wameongea sana suala la upungufu hasa wa walimu na jinsi unavyoathiri ufaulu wa watoto wetu, lakini changamoto hiyo pia ipo kwenye sekta ya afya. Kwamba, tunao upungufu mkubwa kiasi kwamba, huduma zinazotolewa zinaathirika kwa sababu ya upungufu wa watumishi, lakini haya mimi nilitaka tu ni high light.

Mheshimiwa Spika, nitaongea zaidi suala la usimamizi wa rasilimali chache tulizonazo. Una Mwalimu anakaa karibu kilometa 40 kutoka Halmashauri, hapo nimechukua wastani wa kawaida. Anazo stahiki zake ambazo hazina uhakika kila siku anarudi Halmashauri, hivyo hafanyi kazi iliyokusudiwa ya kufundisha wanafunzi. Watumishi wa afya vivyo hivyo, ana stahiki zake Halmashauri atarudi kila siku.

Mheshimiwa Spika, natoa mfano, kwenye suala la kuwapandisha watumishi vyeo. Unaweza ukakuta kwamba, aidha Halmashauri ina watumishi 700 nafasi zinatolewa 400, unampa mtihani Afisa Utumishi je, atachaguaje hao 300 kati ya 700 ambao wote wanastahili? Sasa unakuta kila mtu anafanya lobbying badala ya watu kufanya kazi muda wote wanashinda Halmashauri ili angalao waweze kuangaliwa. Maeneo hayo yapangwe vizuri kwenye suala la kuwasimamia watumishi. Kama Halmashauri ina watumishi 700 ikiwezekana twende kwa phases, Halmashauri ngapi zinapandisha watumishi ili wawe comfortable wafanye kazi.

Mheshimiwa Spika, Serikalini kumekuwa na kuongea suala la kuweza kusawazisha watumishi, kuweka usawa. Kwamba, kuna maeneo mengine watumishi wamekuwa wengi kuliko maeneo mengine, lakini tumeongea sana suala la kuboresha mazingira au wale wanaofanya kazi kwenye mazingira magumu wapewe posho maalum, badala ya kuhangaika kuangalia sehemu gani kuna watumishi wengi, sehemu gani hakuna watumishi wengi, maeneo ambayo yana hali ngumu wapewe posho maalum ya mazingira magumu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, wanaokaa mijini wanayo maji, wanao umeme, usafiri siyo mgumu sana. Wanaokaa vijijini wanakaa maeneo ambako hakuna umeme, hakuna maji, akitaka kusafiri ni changamoto kubwa, hao wapewe vivutio mahsusi ili waweze kufanya kazi kwa utulivu kwenye maeneo hayo. Ukifanya hivyo wale wa mijini wakiona kuna usawa wa huduma kati ya mijini na wa vijijini hawataona taabu kwa sababu wanapata zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaishukuru sana Serikali ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri iliyofanyika kwenye ujenzi wa miundombinu ya elimu, ujenzi wa miundombinu ya afya, lakini ninaomba kwenye kupanga miundombinu hii si lazima kila sehemu tupeleke kituo cha afya kilichokamilika, tunaweza tukaangalia yale mahitaji ya msingi. Mheshimiwa Kakunda ameongea kidogo vitu ambavyo vinahitajika, zipo Kata nchi hii ambazo zimepata zahanati zile za mwanzo, tunaweza tukachagua tukajenga OPD nzuri ikawa na vyumba vile vyote vinavyohitajika, tukaweka huduma ya mama na mtoto wakati huo tukiendelea kutanua kila Kata ipate kituo cha afya. Tunaweza tukajenga kwa awamu wakati huo tukijielekeza kwamba, maeneo mengi yapate hizo huduma kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, ule mtazamo wa Serikali wa kwamba, Makao Makuu ya Tarafa lazima kuwe na kituo cha afya cha kisasa, safi kabisa, ili angalao yale ambayo tunayatengeneza kwenye Kata yaweze kupata rufaa na huduma zilizokamilika kwenye ngazi ya Tarafa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninasema hivi, unaweza kukuta kata ambayo kituo cha afya au zahanati imejengwa sasa hivi na ile ambayo ilikuwa nayo kabla tofauti ni kubwa sana. Suala la ramani ameshaliongea Mheshimiwa Kakunda, kwamba ramani tulizokuwa nazo mwanzo na zilizopo sasa ni tofauti kabisa. Zile za zamani hazikidhi, hivyo maeneo yale yakaangaliwe.

Mheshimiwa Spika, tumeongea sana masuala ya udhibiti wa vifaa tiba, dawa chakula na vipodozi. Kwenye chakula kuna vitu vinaitwa, bidhaa ambayo ni dawa au chakula, kwenye vipodozi kuna vipodozi vidogo dawa au Kipodozi tunaita bodyline products zinakosa udhibiti makini kwa sababu zinadhibitiwa na taasisi mbili tofauti. Naomba bidhaa hizi, bidhaa za chakula vipodozi ambavyo vilikuwa vinadhibitiwa na TFDA ambayo kwa sasa tunasema Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba; bidhaa hizi zote zidhibitiwe na taasisi moja ili kuhakikisha zile border line products zinasimamiwa vizuri ili kulinda Afya ya Watanzania.

Mheshimiwa Spika, ni muhimu sana kwa sababu kwa sasa bidhaa zinazodhibitiwa na TBS, kuna changamoto ya utaalam, lakini wanasimamia bidhaa nyingi hivyo hawatoi umuhimu mkubwa kwenye upande wa chakula na vipodozi.

Mheshimiwa Spika, niseme kidogo kuhusu suala la vipaumbele vya namna ya kuamua mradi gani utekelezwe sehemu gani. Sasa hivi kumekuwa na utamaduni kwamba Wizarani wanasema kuna fedha either ya kujenga shule, ya kujenga Zahanati au ya kujenga jengo la utawala ilhali kwenye maeneo halisia unakuta mahitaji ya Wananchi ni Shule, Mahitaji ya wananchi ni ukarabati wa shule. Ninachoomba ile mipango inavyopangwa ianzie kule chini kwenye ngazi ya vijiji ili kujua mahitaji halisi ya chini. Badala ya tunasema tuna fedha kwa ajili ya kujenga majengo ya utawala, tunafedha kwa ajili ya kujenga zahanati. Tuangalie mahitaji halisi ya maeneo yetu. Kuna shule imechakaa tujielekeze kwenye kukarabati shule, nyumba za walimu hazipo tujielekeze kujenga nyumba za walimu.

Mheshimiwa Spika, lakini tunachangamoto kubwa sana; tumejenga shule za kata nyingi lakini umbali ni mkubwa kutoka wanako kaa watu. Ili kufika shuleni kwenda na kurudi unatembea zaidi ya Kilometa 40. Sasa tuone namna ya kujielekeza kujenga mabweni kwa ajili ya watoto wetu ili wawe salama na waweze kusoma vizuri. Unakuta wanachoka kabla ya kufika shuleni hawana namna ya kujifunza kwa utulivu, tuwekeze kwenye eneo hilo. Inawezekana fedha ni nyingi lakini tuwashirikishe wadau wa elimu ili kuhakikisha tunatatua changamoto hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa nafasi.