Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

Hon. Michael Constantino Mwakamo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibaha Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Kwanza, mimi ni miongoni mwa Wajumbe wa Kamati ya Utawala za Serikali za Mitaa, kwa hiyo, nitajielekeza kwenye taarifa ambayo Kamati yetu tumeifanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, lakini kabla sijaanza kuchangia nichukue nafasi hii kuiomba Serikali hasa watumishi waliopo kwenye Wizara mbali mbali ambazo tumepata taarifa zao kwamba wachukue taarifa hizi na maazimio ambao yanapitishwa leo, yanapitishwa na vikao vya Bunge na kutoa ushauri unaofaa ili Serikali iweze kufikia malengo ya kuwahudiwa wananchi wake.

Mheshimiwa Spika, mimi nitaanza na suala zima la Soko la Kariakoo. Masoko ya Kariakoo yalianzishwa kwa historia yake mwaka 74, lakini walikuwa na soko moja tu wanaloshughulika nalo Soko la Kariakoo lililoanzishwa na sheria namba 36. Soko hili lilikuwa na wanahisa wawili kwa maana ya Jiji la Dar es Salaam lakini pia na Msajili wa Hazina kwa naiba ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, lakini kwa mujibu wa taarifa ambayo imewasilishwa Jiji la Dar es Salaam lilikuwa na hisa asilimia 51. Moja ya kazi kubwa ambayo walikuwa wamepewa Mashirika ya Soko la Kariakoo ni kuhakikisha wanalisimamia Soko la Kariakoo na kuyaendeleza masoko mengine ambayo watakabidhiwa nayo.

Mheshimiwa Spika, lakini sote tupo kama mashahidi, kwamba Shirika hili tangu wakati huo mpaka leo linalisimamia Soko la Kariakoo na hatujayaona masoko mengine ambayo yanaweza yakawa yalikabidhiwa kwao na yaweze kutoa tija kama ambavyo Soko la Kariakoo limetoa tija.

Mheshimiwa Spika, sasa kwenye Kamati tumeweka azimio, kwamba ni vizuri Serikali ikaangalia namna ya kubadilisha sheria hii badala ya hili shirika kuwa ni Shirika la Masoko ya Kariakoo ikiwezekana likaanzishwa Shirika la Masoko nchini. Ili tuwe na shirika moja kama ambavyo tulivyo na Shirika la Nyumba, ambalo linatoa huduma nzuri ya ujenzi na uendeshaji wa miradi hii katika nchi hii. Tutakapofanya hivi tutatumia shirika hilo kuyaendeleza masoko yote nchini ambayo yataweza kusaidia kupokea bidhaa za wakulima na kuweza kuwaongezea kipato chao.

Mheshimiwa Spika, leo hii nchi nzima tunafahamu, mkulima wa nyanya ya Iringa, mkulima wa mboga mboga kutoka maeneo yeyote, mkulima wa ndizi, wanapakia mazao yao safari inaelekea Kariakoo. Kwa sababu wakulima wana matumaini kwamba kwa namna ya miundombinu yake ilivyo, wafanyabiashara wapo pale na wanaohitaji huduma zao watawakuta pale na wanaweza kufanya biashara za mazao yao vizuri. Kwa hiyo, endapo tutakuwa tumeanzisha kweli Shirika la Masoko nchini na likachukua jukumu la kuyaendeleza masoko nchini, tunawezekana tukawa na masoko yenye ubora na yenye kutoa tija kwenye kila kanda ikiwezekana.

Mheshimiwa Spika, na kutokana na nchi yetu ilivyokaa na Mungu alivyotujalia kila kanda ina aina yake ya mazao wanayovuna. Kwa hiyo inawezekana ikasaidia wateja wa aina fulani ya mazao wakasogea kwenye soko lililojengwa kwa ubora mzuri na linalosimamiwa kwa utaratibu mzuri, ambapo wakaenda kuchukua mazao yao na wananchi wale wakapata kipato chao kwa urahisi. Kwa kufanya hivyo, kuna hili genge ambalo ndugu yangu Saasisha amelielezea, la madalali, wanaweza wakakosa nguvu ya kumuonea mkulima kwa sababu mkulima anatumia dalali kuweza kumsafirishia mazao yake kutoka shambani mpaka sokoni, kumsimamia mauzo naye kumpatia pesa. Lakini masoko yakiwa yameenea na yana ubora maana yake wale wanunuzi ambao wanahitaji bidhaa hizo watafuata kwenye masoko ya jirani kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ningeshauri kwamba lile azimio la Kamati ambalo ni azimio la Bunge la kuomba Serikali kupitia na kuona namna bora ya kuanzisha Shirika la Masoko nchini lifanyiwe kazi kwa kina, kwa sababu linaweza likatuletea tija kubwa sana kwenye nchi. Kwa sababu tulipokuwa tunapitia taarifa ya masoko, Soko la Kariakoo kwa mwaka wanaingiza bilioni nne, kwa taarifa ambayo wale waliwasilisha. Sasa tungekuwa na masoko mengi nchi ambapo kila soko limesimamiwa vizuri maana yake Pato la Taifa lingeongezeka. Kwa hiyo ni vizuri sana wataalam kwenye hizo Wizara wakatusaidia kuhakikisha wanaweza kusimamia hili azimio na likatekelezeka vizuri.

Mheshimiwa Spika, lakini pia, tumeona kwa wachangiaji na kwenye taarifa; kuna suala hili linaitwa la madalali. Tumeona Serikali kupitia Wizara ya Kilimo inavyoamua kuhakikisha kwamba wakulima watengenezewe mazingira bora ya kuzalisha. Zoezi linalofanywa na Serikali leo la kuhangaika na usambazaji wa mbolea na upatikanaji wa mbegu bora. Kama tutakuwa na masoko yanayosimamiwa katika Shirika moja zuri, hizi kazi zingeweza zikaratibiwa vizuri na zikafanya vizuri kabisa na wakulima wangelima vizuri zaidi.

Mheshimiwa Spika, lakini jambo lingine, kuna chombo hapa kimetajwa hapa, Bodi ya Mikopo ya Serikali za Mitaa. Chombo hiki nacho Kipo pale TAMISEMI. Ukiangalia historia inaonesha kimeanza kutoa huduma mwaka 1965, lakini imetoa mikopo kwenye halmashauri 57 tangu kianzishwe. Kati ya hizo halmashauri 57 halmashauri 12 mpaka leo zinadaiwa. Ukipitia ile taarifa, sisi tulikuwa kwenye Kamati, ukiangalia mikopo iliyokuwa inatolewa na hii bodi ya mikopo na ukiangalia jinsi pesa zile zilivyokuwa zinakopwa na halmashauri na jinsi zinavyotumika, hakuna tofauti kabisa na kilio tunacholia leo, kazi zinazofanywa na SACCOS mbali mbali zinazoshindwa kuendelea. Kwa sababu mtu ameanzisha halmashauri inakwenda kukopa kwenye bodi hii, anakopa pesa za kwenda kufanya ukarabati wa gari. Sasa, tija hii inapatikana wapi.

Mheshimiwa Spika, matokeo yake wanashindwa kurejesha mikopo. Bodi inashindwa kujiendesha, bodi inashindwa kuwa na uwezo wa kuongeza vyanzo vingine kwa sababu wakopaji walipeleka pesa zile kwenye miradi ambayo haitoi tija. Sasa kwa sababu haitoi tij maana yake fedha zimeshindwa kurudi.

Mheshimiwa Spika, lakini ukiangalia bodi hii chanzo chake cha mikopo eti ilikuwa ni michango ya halmashauri husika. Sasa hebu tuangalie halmashauri zimechangia nyingi lakini zilizokopeshwa mpaka leo ni halmashauri 57. Hivi yule ambaye tangu ianze hii bodi mwaka 65 hajawahi kukopeshwa anachangiaga tu, hiyo nguvu ya kuchangia anaitoa wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo mimi ningeshauri kwamba Serikali ione namna bora ya kukisimamia hiki chombo na ikiwezekana ikiongezee vyanzo vya mapato. Pia, kuna kazi tunahangaika nayo sasa hivi ya asilimia 10 ya mikopo. Wabunge Wengi wanalia kwamba ile idara iliyopewa kukopesha inapata tabu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kumbe TAMISEMI tuna chombo kinaitwa Bodi ya Mikopo, kwa nini tusijifunze, tukakiongezea nguvu hiki, ikasimamia mikopo yote ikiwezekana na hiyo ili iweze kwenda kwa tija kwenye maeneo yanayostahili, ili ikakusanywa zile fedha ikaonekana tija yake?

Mheshimiwa Spika, lakiniā€¦

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa muda umekwisha naunga mkono hoja. (Makofi)