Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

Hon. Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa fursa nami niweze kuchangia. La kwanza niseme kwamba yale yote ambayo Waheshimiwa Wabunge wametupatia kama ushauri na yale ambayo wametupatia kama maelekezo tumeyapokea. Tutaenda kuyafanyia kazi; na yale ambayo yanaangukia kwenye Sekta yetu, tumeyapokea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niweke kumbukumbu sawa katika baadhi ya mambo ili Hansard zako ziweze kupata vizuri. Nikianza na jambo moja ambalo ameliongelea Mheshimiwa Mpina; katika mchango wake amechangia mengi, lakini eneo mojawapo amesema tunapata mfumuko wa bei kwa sababu ya mismanagement ya Sera za Fedha. Akaelezea kwamba tumefanya malipo nje ya bajeti. Kwa maana hiyo, yeye akakichukulia hicho kama kitu ambacho ni mismanagement ya Sera za Fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niweke kumbukumbu sawa. Moja, fedha hizo anazosema zimelipwa, siyo zilizolipwa. Ni vizuri sana Waheshimiwa Wabunge, tunaitwa Waheshimiwa, tunapotoa taarifa kwenye chombo hiki kikubwa tuwe tunatoa taarifa ambazo tuna uhakika nazo. Fedha ambazo tumelipa nje ya bajeti, yako mafungu kama matatu hivi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, fungu la kwanza tumelipa fedha nje ya bajeti baada ya kugundulika kuna wanafunzi 29,000 wamekosa mikopo ya elimu ya juu. Tukaja hapa Bungeni, Waheshimiwa Wabunge mkasema tena kwa azimio, kwamba tafuteni fedha kokote watoto hawa wote wawe wameenda vyuoni; na walikuwa wanatangatanga, wanazagaa zagaa. Wameshapata admission, lakini hawana fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekwenda kuchukua Shilingi bilioni 86 ambazo hazikuwepo kwenye bajeti, na watoto wetu wako Vyuo Vikuu hivi tunavyoongea. Tusingeweza kuwaacha wanafunzi 89,000 kisa eti hazikuwepo kwenye bajeti ilhali Bunge liliopitisha bajeti limeshatoa maelekezo hayo ya kuwapeleka watoto hawa vyuoni. Hilo lilikuwa eneo la kwanza ambalo tumetoa fedha ambazo hazikuwepo kwenye bajeti. Wanafunzi 29,000 wanapata mikopo na sasa wapo mashuleni na wiki ile ile Bunge lilipotoa maelekezo, kulitulia, hamkusikia tena kelele inayohusu mikopo ya elimu ya juu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ambalo tumetoa fedha ambazo hazikuwepo kwenye bajeti, tulitoa Shilingi bilioni 160 kwa ajili ya kujenga madarasa 8,000 ili mwaka huu wanafunzi wote waliotakiwa kwenda Form One, waende Form One. Ninyi mmetokea majimboni kule, mmeyaona hayo madarasa, na ninyi wenyewe ndio mmeshawishi fedha hizo za madarasa zipatikane. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, anapotokea Mbunge anasema tumetoa fedha hizo nje ya bajeti na kuishambulia Serikali kama vile imefanya uamuzi mbaya, nadhani lazima kuwe na kasoro katika thinking. Kama mzazi huwezi ukachukia wanafunzi masikini kupewa mkopo; kama mzazi huwezi ukachukia fedha zinazotolewa kwenda kwenye madarasa. Nilitamani na nilidhani Wabunge makini wangemshukuru Mheshimiwa Rais kwa kuchukua uamuzi huo wa kutoa fedha na watoto wote wakapata mikopo. Nilidhani Mbunge yeyote aliye makini atampongeza Mheshimiwa Rais kwa kutoa Fedha zikajenga madarasa 8,000 mpaka na second selection watoto wale wakaenda shuleni… (Makofi)

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niliona hiyo niiweke sawa. Bunge lilitoa maelekezo kwamba watoto hawa waende shule na Serikali ikaitikia, tukatoa shilingi bilioni 86 za mikopo ya elimu ya juu, tukatoa shilingi bilioni 160 kwa ajili ya madarasa 8,000 ambayo yamejengwa katika majimbo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya mambo tusiwe tu tunatamani kushambulia Serikali hata kama haijafanya makosa. Serikali ikifanya makosa ikosoeni, lakini ikifanya jema, iambieni. Hizi ndizo fedha ambazo zimetoka nje ya bajeti. Hizi fedha ninazosema zimetoka nje ya bajeti, wala haziwezi zikasababisha mfumuko wa bei. Sijui ni uchumi wa wapi huo ambao ukijenga madarasa yanaleta mfumuko wa bei wakuweza kuleta matatizo hayo. Niliona niliseme vizuri hili ili liweze kueleweka. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine limeongelewa kwamba tunasamehe wawekezaji na tunatoza masikini. Nchi hii imetoka mbali sana mpaka kufika hapa; nchi hii imetoka katika miaka ambapo ilikuwa na mainjinia wawili na madaktari wawili; nchi hii imetoka katika eneo ambalo wanafunzi wa elimu ya juu ilikuwa nao saba ikaenda kumi ikaenda ishirini, ikaenda thelathini. Hivi tunavyoongea kila mwaka ukijumlisha wanafunzi waliotoka Darasa la Saba na hawakwenda Kidato cha Kwanza, ukajumlisha waliotoka Kidato cha Nne na hawakwenda Kidato cha Tano, ukijumlisha waliotoka Kidato cha Sita na hawakwenda Vyuo Vikuu na ukajumlisha Vyuo vya Kati wamemaliza, na ukajumlisha waliotoka Vyuo Vikuu wamemaliza, utakuwa na idadi isiyopungua wanafunzi milioni moja wanaoingia kwenye soko la ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kama kuna wanafunzi zaidi ya milioni moja wanaingia kwenye soko la ajira, lazima ubadili utaratibu wa kuwaza kuhusu utengenezaji wa ajira hizo.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu utaratibu.

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu wa kutengeneza ajira hizo ni kuvutia uwekezaji. Hawa wote hawawezi wakaingia kwenye Halmashauri. Huwezi ukawa na wanafunzi milioni moja kila mwaka wanatafuta soko wakaingia kwenye Halmashauri, wakaingia Serikalini. Lazima utengeneze uwekezaji unaostahili kuajiri hawa, lazima utengeneze viwanda, lazima utengeneze uzalishaji.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Kuhusu Utaratibu. Utaratibu!

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, haya mawazo ya kudhania unasamehe mwekezaji kwamba unamsamehe mtu tajiri na unamtoza masikini, ni utaratibu ule ule wa baba asiye na hekima ambaye anaonea wivu kupanda mbegu kwa kudhania kwamba anatakiwa apike ile mbegu ili wale kama familia. Ukitaka kuvuna lazima upande ndiyo utaratibu wa kiuchumi. Ukitaka kuvuna, lazima upande. Huwezi ukavuna bila kupanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunapowekeza, tutatoza watakapoanza uzalishaji. Huwezi ukaendelea kuwazia kutoza watu ambao hawajaja. Umewasamehe wapi ambao hawajaja? Tunatengeneza vivutio waje ili tuwatoze. Unahesabu kumtoza mtu ambaye hajaja! Yaani unahesabu watoto walioko tumboni mwa mama zao kwamba hawafanyi kazi! Watafanya kazi gani nyingine? Unatakiwa ulee mimba, wakizaliwa uwalee, uwatunze, wakishakua ndiyo uwatume kazi. Mnataka kuwatuma kazi watu ambao bado wako kwenye mataifa yao? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunavutia wawekezaji, tunaweka na vivutio waje wawekeze. Wakishawekeza, Watanzania watapata ajira, na waliowekeza watalipa kodi. Ninyi mtaka kuhesabu kodi ya watu ambao hawajaja! Uchumi wa wapi huo? That is vicious cycle, kuwaza kwamba unamhurumia masikini kwa kuzuia uwekezaji, that is vicious cycle. Unawasababisha masikini waendelee kuwa masikini. Wekeza wapate kazi ili watoke kwenye umasikini. Wekeza wapate ajira ili watoke kwenye umasikini. Wekeza ili upate sekta binafsi kubwa ili sekta binafsi ilipe kodi uwatoe masikini kwenye kulipa kodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, masikini wakibaki peke yao utaendelea kuwatoza wao wenyewe. Masikini wakibaki wao watupu, utaendelea kuwatoza wao watupu. Tunaleta wapya, tunaleta makampuni mapya yawekeze, tunaleta sekta binafsi ikue ili tuweze kuitoza hiyo sekta binafsi tuwahurumie masikini. That is how to broke the vicious cycle.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hebu tujadilini mambo mengine mengine huko yanayohusu uganga wa kienyeji na vitu vingine, kwenye uchumi, this is my profession. Tunajadilije hivi vitu ambavyo vipo clear? (Makofi)[Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka tusimvunje moyo Mheshimiwa Rais anavyo…

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: …anavyohurumia masikini, anataka Sekta iendeshe uchumi…

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa!

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii tumebakiza Watumishi wa Umma ndio walipakodi wa nchi hii. Watumishi wa Umma ndio tunaotoza kodi kwa sababu hata hawawezi kukwepa. Walipa kodi wakubwa…

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima tuwe na Sekta binafsi imara ndiyo tunaweza kuongeza…

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa!

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Dkt. Mwigulu. (Makofi)

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilidhani niyaseme hayo. Nakushukuru sana.