Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

Hon. Mashimba Mashauri Ndaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii kukushukuru kwa kunipa nafasi ili pia niweze kuchangia mapendekezo, maoni na maazimio ya Kamati yetu ya Kilimo, Mifugo na Maji. Kwanza nianze kwa kuishukuru sana Kamati yetu chini ya Mwenyekiti Dkt. Ishengoma na Makamu Mwenyekiti Mheshimiwa Maige. Tunawashukuru sana kwa ushauri wao na kwa maelekezo ambayo wameendelea kutupa kama Wizara, lakini pia tunawashukuru sana kwa kututia moyo na kuendelea kufanya kazi hii vizuri katika mazingira ambayo tunakuwepo.

Mheshimiwa Spika, niwashukuru sana pia Wajumbe wa Kamati. Wajumbe wa Kamati kila tulipokutana nao walikuwa very positive na sisi na walikuwa wakitushauri mambo ambayo yanaweza kuleta tija kwenye Wizara ya Mifugo na Uvuvi, tunawashukuru sana.

Mheshimiwa Spika, nimshukuru sana Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kutuongezea bajeti hasa kwa mwaka huu wa 2022/2023. Bajeti yetu pia iliongezwa kwa asilimia 62, mwaka uliopita ule tulikuwa na bajeti ya shilingi bilioni 168 mwaka huu tuna bajeti ya shilingi bilioni 269. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais na sisi tunaahidi kwamba, kwa fedha hii tutafanya yale yote yanayowezekana kutokana na bajeti hii, yaweze kukamilika ili mwaka unaokuja aweze kuvutika na pengine kutuongezea bajeti kufikia bajeti ile ambayo tulikuwa tunaihitaji.

Mheshimiwa Spika, nianze na suala hili la uduumavu wa samaki na niseme kidogo. Suala hili sio tu Kamati ililiona, lakini pia sisi kama Wizara tuliliona hasa kuhusiana na Bwawa la Mtera. Sasa sababu ni moja tu ambayo inaonekana hadharani kwamba, kuna uchafuzi wa mazingira kuzunguka bwawa lile, lakini sisi tukasema hatuwezi kuchukua sababu hiyo moja ndio ikawa sababu ya kudumaa kwa samaki walioko kwenye Bwawa la Mtera. Kwa hiyo, tumeenda mbali zaidi na kuiagiza Taasisi yetu ya Utafiti inayoitwa TAFIRI ili ifanye utafiti, iangalie kama kuna sababu nyingine na hatua zinazoweza kuchukuliwa ili kuondokana na tatizo hilo.

Mheshimiwa Spika, sasa nataka niwahakilishie Watanzania kwamba suala la udumavu nimezungumza na Kamati, lakini Kamati ikifanya reference na Bwawa la Mtera. Kwa hiyo, samaki wengine wanaotoka kwenye maeneo ya bahari na maji matamu au maji baridi wako salama na Watanzania wakila samaki bado wanabaki ni salama.

Mheshimiwa Spika, nizungumzie suala la ajira, ambalo limezungumziwa na Wabunge wengi, lakini mmojawapo Mheshimiwa Thea Ntara. Alizungumza akitaka kujua ni kwa namna gani sekta hii kwa sababu ni ya uzalishaji pia, inatengeneza ajira. Sekta ya Mifugo na Uvuvi, imejiandaa kutengeneza ajira kwa kadiri itakavyowezekana na kwa kadiri ambavyo tunapata fedha kutoka Serikalini. Kwa wakati huu tuna vituo atamizi vinavyoshughulika na masuala ya mifugo pekee nane na tuna vijana 240 kwenye hivyo vituo tayari kunenepesha mifugo na kuiuza. Lengo la vituo hivi vya kifugaji ni kujaribu kubadilisha fikra za wafugaji wetu waweze kufuata vijana hawa namna watakavyokuwa wakifuga ili tuongeze tija na tufuge kibiashara upande wa mifugo.

Mheshimiwa Spika, pia upande wa uvuvi, tuna vijana 200 sasa hivi wako kwenye vituo vyetu atamizi vya binafsi 14 na vituo atamizi vya Serikali viwili, ambavyo kwa kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu wako kule kujifunza ufugaji wa samaki na wakitoka pale hawa ni wafugaji wa samaki moja kwa moja. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa sababu anatuunga mkono na kwa kuwapa allowance vijana wale. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kwenye uvuvi tuna vizimba ambavyo tayari vinaanza hivi karibuni. Kuna wanufaika zaidi ya 1,800 na kitu. Miongoni mwa wanufaika hao watakuwemo vijana. Kwa hiyo, ajira kwa vijana sekta hii pia tunaitengeneza kupitia shughuli hizi ambazo Wizara imepangiwa.

Mheshimiwa Spika, niendelee na suala la Serikali kujenga mabwawa kwa kushirikiana. Suala hili hata tulipofika mbele ya Kamati tuliwaeleza kwamba sisi Wizara tatu; Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Wizara ya Kilimo na Wizara ya Maji, tayari tuko kwenye mazungumzo na wataalam wetu wameshatengeneza memorandum of understanding ili turatibu kwa pamoja. Tuweze kufanya kwa pamoja hizi kazi za kuchimba mabwawa, tuwe na design inayoeleweka, tuwe na viwango vinavyofanana ili Serikali inapotaka kujenga bwawa la mifugo, lakini litatumika pia kama chanzo cha maji ya binadamu na chanzo cha maji wakati mwingine kwa ajili ya umwagiliaji. Kwa hiyo, tayari Serikali tuko kwenye mchakato na tukikamilisha tutasaini memorandum of understanding, halafu suala hili litafanyika kwa pamoja kwa uratibu mzuri na changamoto ambazo zimetajwa na Waheshimiwa Wabunge pengine zitapungua kama sio kuondoka kabisa.

Mheshimiwa Spika, nizungumzie suala la malisho kwa mifugo yetu ambalo limezungumzwa pia na Waheshimiwa Wabunge. Sasa hivi tumetengeneza sera au mfumo wa mabadiliko wa Sekta ya Mifugo. Moja ya suala ambalo tunalizungumza kwenye mabadiliko haya ni namna gani malisho yatapatikana kwa mifugo yetu hapa nchini. Kwa hali ilivyo…

SPIKA: Sekunde 30.

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, kwa hali ilivyo sasa hivi, wafugaji wetu wanategemea maeneo ya malisho ya jumla. Sasa kwenye mfumo na mabadiliko haya tunayokuja nayo, tunataka wafugaji wenyewe wamiliki maeneo ambayo watakuwa wanalisha mifugo yao. Wamiliki wenyewe na tutasaidiana na Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kuwapa hati kwa ajili ya maeneo hayo ya malisho.

Mheshimiwa Spika, pia tunataka maeneo yaliyotengwa yote kwa kufuata ule mpango wa matumizi bora ya ardhi, maeneo yote yaliyotengwa kwa ajili ya ufugaji tuyasajili halafu tuyatangaze kwenye gazeti la Serikali ili yalindwe kisheria, badala ya hali ilivyo sasa hivi wakati maeneo hayo yanapotengwa yasipolindwa mtu yeyote anaweza akaja na kuyachukua. Kwa hiyo, tuko na mpango huo na tutaendelea kuwaelimisha wafugaji wetu ili waweze kuelekea kwenye mwelekeo huo na tunahisi tukienda pamoja na wafugaji wetu tutapunguza migogoro inayosababishwa na ukosefu au upungufu wa malisho kwenye nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ya muda…

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa.

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)