Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, nami nikushukuru kwa kunipatia fursa ya kuchangia katika ripoti hii na ninachangia kama Mjumbe wa Kamati ya Kilimo, Mifugo na Maji.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu leo ni siku ya mwisho ya mwezi Januari, na kuna Waheshimiwa Wabunge hatujaonana, naomba kwanza niwatakie Heri ya Mwaka Mpya kwa sababu najua sijachelewa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitachangia kwa uchungu sana suala moja nyeti ambalo ni uharibifu wa vyanzo vya maji na athari zake. Waheshimiwa Wabunge wenzangu wameshachangia mambo mengine kwenye Sekta za Kilimo, Mifugo na Uvuvi, mimi ngoja nijikite kwenye uharibifu wa vyanzo vya maji na athari zake.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kuunga mkono hoja ya ushauri wote ambao kamati imetoa. Nchi yetu ya Tanzania tuna baraka kubwa sana, tumejaliwa kuwa na vyanzo vingi vya maji. Tuna mito mingi, maziwa, chem chem na tuna maji mengi ambayo tumeambiwa na Wizara ya Maji kwamba yako chini ya ardhi. Rasilimali maji hizi ni muhimu sana katika maisha yetu ya kila siku. Tusipokuwa waangalifu kuhakikisha kwamba tuna tunza na kuchunga rasilimali maji hizi, huko mbele ya safari tutapata shida kubwa sana kwa sababu hatutaweza kuzalisha chakula, hatutapata maji ya kunywa na kadhalika na kadhalika, athari ziko nyingi sana.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kutokana na umuhimu wa maji kwenye hizi sekta ambazo tunazisimamia ni umuhimu sana sana kutunza vyanzo vya maji ili tuhakikishe tunapata maji na hasa tukizingatia kwamba sasa hivi kuna mabadiliko ya tabianchi ambayo yanaendelea. Uharibifu wa vyanzo vya maji umekithiri katika maeneo mengi nchini kwetu na uharibifu huu umeshasababisha matatizo makubwa kwenye mambo mbalimbali kama vile uzalishaji wa umeme, wote ni mashahidi kwamba kulikuwa na katakata ya umeme hapa nyuma, ni kutokana na upungufu wa maji katika vyanzo vyetu vya maji.

Mheshimiwa Spika, uharibifu huu unatokana na nini hasa? Uharibifu huu tunafanya sisi wenyewe binadamu. Binadamu sisi ndiyo vyanzo vya uharibifu wa hivi vyanzo vyetu vya maji ambapo watu kwa kujua kabisa au kwa makusudi wanakata miti bila kuzingatia sheria. Baada ya kukata hii miti, tunapata athari kubwa sana za upungufu wa maji ambayo tungeyatumia kwenye shughuli nyingine kama vile za kilimo, kuwapa ng’ombe maji wanywe, kupata maji ya kunywa majumbani pamoja na shughuli za uvuvi.

Mheshimiwa Spika, huku kukata miti ambako kunaendelea katika maeneo mengi ya nchi hii kumeshasababisha mabadiliko ya tabianchi ambapo tunajionea wote. Ukienda kwa mfano kule Kilimanjaro, ule mlima sasa hivi uko uchi kabisa. Theluji imekwisha pale mlimani na kama nilivyosema awali kwenye maeneo mengi kwa kuwa tunakata kata miti sana, maji yamepungua na nimeshasema athari ambazo tumeshajionea hivi karibuni. Ni sasa hivi tu mvua zimeanza ndiyo tumeanza kujinasua na matatizo ya ambayo yapo.

Mheshimiwa Spika, nitatoa mfano, kule Dar es Salaam mliona wenyewe crisis ambayo ilitokea. Jiji la Dar es Salaam ambalo ndiyo jiji letu kuu la biashara, ilikuwa hamna maji na watu walipata shida kubwa sana. Tukubaliane Waheshimiwa Wabunge wote huko tulikotoka tulikuwa na crisis ya maji hata kule Kilimanjaro pamoja na kwamba tuna maji mengi kwenye mito lakini kulikuwa na mgao wa maji na hii ilitokana na kuharibu vyanzo vya maji.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, pale Dar es Salaam shida kubwa ilikuwa ni matumizi mabaya yaani utunzaji mbaya wa Bonde letu la Mto Ruvu. Kumekuwa na activities za binadamu ambazo zimeharibu Bonde la Mto Ruvu na Pangani na maji hayakufika Dar es Salaam na tumeona shida ambayo ilitokea pale. Kama tunataka tuwe salama, niiombe Serikali chonde chonde tuhakikishe tunatunza vyanzo vya maji na kwenye kamati yetu tumesema mambo mengi ya kufanya lakini nitashauri vitu vichache.

Mheshimiwa Spika, ninaishauri Serikali kitu cha kwanza cha kufanya, tumeshapitisha Sheria ya Kutunza Vyanzo vya Maji ya Mwaka 2022. Niiombe Serikali iajiri wanasheria wa kutosha katika mabonde yote tisa, tuwapatie zana zote muhimu waende wakapambane na huu uharibifu wa kukata miti ili ile sheria itekelezwe. Mtu yeyote anayeharibu vyanzo vya maji achukuliwe sheria kwa hiyo, ushauri wangu wa kwanza ni kwamba Serikali iboreshe vitengo vya sheria kwenye mabonde yote ili hawa wanasheria waweze kufanya kazi na vyanzo vyetu vya maji viwe salama na sisi wote tuwe salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu wa pili kwa Serikali, Serikali za Wilaya na Serikali za Mikoa, maji ni suala la Usalama wa Taifa na tusicheze na suala la maji kabisa. Ninashauri hizi Serikali za Wilaya na za Mikoa na za Kata ikiwezekana, zile Kamati za Usalama za haya maeneo zijihusishe kikamilifu kuhakikisha kwamba tunatunza vyanzo vya maji. Wawe wanafanya inspection from time- to-time wahakikishe kwamba vyanzo haviharibiwi na mahali ambapo wameharibu, zichukuliwe hatua za kisheria za kuwapeleka hawa watu mahakamani.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu wa pili waswahili wanasema mtoto wako ukitaka asife kama kuna mchawi karibu mpe yule mchawi akusaidie kumtunza yule mtoto. Mimi nashauri Serikali ianzishe program muhimu kabisa ya kufundisha wananchi ambao wako kwenye vile vyanzo vya maji, umuhimu wa kutunza hivi vyanzo na washirikishwe kikamilifu. Kwa hiyo, elimu itolewe na Serikali ili wananchi watunze hivi vyanzo vya maji.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Kengele imeshagonga ya pili Mheshimiwa.

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)