Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

Hon. Amb. Dr. Bashiru Ally Kakurwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

MHE. BALOZI DKT. BASHIRU A. KAKURWA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Kwa sababu ya ufinyu wa muda nianze kwa kuunga mkono mapendekezo yote na taarifa nzima ya Kamati ya Kilimo, Mifugo, Uvuvi na Maji ambayo mimi ni Mjumbe. Nitakayoyazungumza yameshajadiliwa kwenye Kamati na baadhi ya Wajumbe kazi yangu itakuwa ni kuweka msisitizo.

Mheshimiwa Spika, la kwanza, mwaka jana tulikuwa na matatizo makubwa mawili kama Taifa, ukame na mfumko wa bei hasa za vyakula. Kwa hiyo nitagusia kidogo kwenye eneo la ukame kwa Sekta ya Maji lakini mchango wangu kwa sehemu kubwa utagusa Sekta za Uzalishaji, kwa maana ya kilimo, mifugo na uvuvi.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kuipongeza Serikali na hasa Wizara ya Maji na Shirika letu la DAWASA kwa namna walivyoshughulikia tatizo kubwa la uhaba wa maji hasa katika Jiji la Dar es Salaam. Tatizo hilo limetupa mafunzo mengi kwamba uwezo wa Serikali kukabiliana na majanga ni mkubwa na kama Serikali inamiliki vyombo vya kufanya kazi hiyo inakuwa salama zaidi na hapa tujifunze kwamba, mawazo ya kubinafsisha huduma za maji hayafai katika nchi maskini kama ya kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama tatizo lile lingetokea wakati watoa huduma ya maji wangekuwa ni Sekta Binafsi tungetafutana, lakini uratibu, ufuatiliaji na juhudi na hatua za haraka ziliwezekana kwa sababu jambo hilo lilishughulikiwa mia kwa mia na Serikali. Kwa hiyo tujifunze kwamba katika maeneo nyeti ya huduma za kiuchumi na za kijamii, vyombo vya Kiserikali ni muhimu sana. Hilo ni funzo pia kwenye eneo la nishati na umuhimu wa kuimarisha Shirika letu la TANESCO na mashirika mengine ambayo yanaweza yakatusaidia wakati nchi inapoingia kwenye mtikisiko wa dharura usiotarajiwa.

Mheshimiwa Spika, funzo la pili ni kwamba, DAWASA walibaini kwamba kama matatizo ya maji kwa Ruvu Juu ni makubwa na Ruvu Chini ina nafuu, wanaweza wakaunganisha mifumo ilhali ikiwa mbaya Ruvu Juu, Ruvu Chini iweze kusaidia, maana yake nini? Maana yake kuna haja ya kufikiria kuwa na mfumo ambao unafananafanana na Gridi ya Maji ya Taifa. Kwa sababu vyanzo vyetu vimetawanyika, kuna maeneo yenye ziada na kuna maeneo yenye uhaba. Kwa hiyo miundombinu yetu ikizingatia namna ya kusaidiana kwenye maeneo ya ziada na uhaba, tunaweza tukawa na mpango mzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimalizie dakika zangu tatu zilizobakia kwenye eneo la uzalishaji. Nitasema kwa ufupi tu kwamba, njaa inadhalilisha heshima na uhuru wa nchi na njaa inatweza utu wa binadamu. Kwa hiyo tatizo la mfumko wa bei za vyakula ni tatizo ambalo tutake tusitake lazima tuongeze kiwango cha ubunifu kukabiliana nalo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mwenyezi Mungu ametuwezesha kama binadamu hakuna ukomo wa ubunifu. Wananchi wanakabiliana na tatizo hili, nilikuwa nazungumza na baadhi yao, mmoja anasema wamepanga milo kwa kupiga pasi. Kwa maana ya kwamba staftahi ya asubuhi na chakula cha mchana vinaunganishwa kwenye majira ya saa 5.00 na saa 6.00 mchana halafu na mlo wa usiku unaunganishwa kati ya majira ya saa 11.00 na saa 12.00 jioni, hawasubiri kujadili mambo ya Ukraine na tabianchi na kadhalika wameanza kuchukua hatua.

Mheshimiwa Spika, mwingine ananiambia pesa aliyokuwa anaitumia kunua unga ni ileile na chanzo cha mapato yake hakijaongezeka, lakini bei ya unga imeongezeka kwa hiyo unga aliokuwa anaununua kwa pesa ileile kusonga ugali, ameamua kukoroga uji. Sasa kama wananchi wanakabiliana na hali hiyo na nchi inaenda, miradi ya maendeleo inaendelea haijasimama. Kwa nini Serikali isipanue wigo wa kufikiri na ubunifu kukabiliana na tatizo hili? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimalizie kwa kuacha maswali machache kuongezea ulipotuongoza, je, ruzuku ya mbolea na mafuta na mbegu imepunguza makali kiasi gani ya mfumko wa bei ya vyakula? Je, kutokuwa na lockdown kumepunguza kiasi gani makali ya mfumko wa bei za vyakula? Je, udhibiti wa kuuza vyakula nje ukiwepo unamnufaisha nani na pia vyakula vikiuzwa nje kwa uwazi hiyo ruksa inamnufaisha nani? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho, uwekaji wa mazingira ya wananchi wanaozalisha chakula na hapa nikisema chakula namaanisha wavuvi, wafugaji na wakulima. Nadhani tuna kazi ya ziada ya kuboresha mazingira ya wananchi wa aina hii. Kwa nini tumeshindwa kudhibiti lumbesa? Lile tamko la Serikali la kuruhusu mwananchi asafirishe vyakula kwenda sokoni bila kusumbuliwa ili mradi havizidi uzito wa tani moja lipo au halipo?

SPIKA: Sekunde thelathini, malizia.

MHE. BALOZI DKT. BASHIRU A. KAKURWA: Mheshimiwa Spika, la mwisho hilo, je, haki ya ardhi ya wakulima na wafugaji imelindwa kwa kiasi gani na wana uhakika kwa kiasi gani kuitumia ili kujilisha wao wenyewe na kulilisha Taifa?

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)