Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

Hon. Charles John Mwijage

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Muleba Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

MHE. CHARLES J. P. MWIJAGE: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru. Awali ya yote napenda nitoe taarifa kwamba mimi ni Mjumbe wa Kamati hii, Kamati ya Kilimo, Mifugo na Maji au sekta za kiuzalishaji, kabla sijaendelea nizungumze waliyonituma mabosi wangu ninaowawakilisha.

Mheshimiwa Spika, wananchi wa Kata ya Rutoro wamenituma kwako nije kukushukuru, wanakushukuru kwa ushauri ulionipa wakati wa kipindi kigumu cha mgogoro wa Rutoro. Pia wanamshukuru Mwanasheria Mkuu wa Serikali, unakumbuka nilivyokuja kwako ninahema, lakini wanamshukuru na bosi wangu wa zamani Mheshimiwa Simbachawene.

Mheshimiwa Spika, unajua mgogoro wa miaka 17 uliodumu Rutoro, Mheshimiwa Rais alipokuja Kagera mwezi Agosti kwa ujasiri nilikwenda nikamweleza tatizo la wananchi, alisema Mwijage hilo tatizo nitalishughulikia.

Mheshimiwa Spika, nataka nilieleze Bunge lako tukufu Baraza la Mawaziri walikuja na helikopta, wakasema Mheshimiwa Rais anasema wananchi wakae walime na wafuge wakae kwa amani. Naitwa good boy siku hizi na sio bad boy, lakini wamenituma nikushukuru wewe.

Mheshimiwa Spika, nizungumzie hii sekta ya uzalishaji; leo tuko kwenye dhima ya tatu ya ujenzi wa dira ya Taifa ambayo inazungumzia uchumi shindani, uchumi uliojumuishi, uchumi wenye shughuli za tija kubwa na uchumi endelevu. Nimeshiriki kwenye Kamati ulikonipanga, tunakwenda vizuri, kwenye maji shughuli zinakwenda, kwenye kilimo shughuli zinakwenda na kwenye mifugo shughuli zinakwenda. Nina mambo ya kuishauri Serikali au Wizara.

Mheshimiwa Spika, tumepeleka pesa nyingi kwenye Wizara hii, lakini tumepeleka pesa ukweli ulio wazi, hakuna watenda kazi kule. Kwa hiyo hakuna watu wa kutenda kazi zile. Naishauri Serikali haraka watendakazi wenye ujuzi na weledi waajiriwe kusudi zile pesa ziweze kuleta tija.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo suala lingine la ajira; unapozungumza wafanyakazi/ajira, watu wa Serikali wanakwambia suala la bajeti. Sawa , lakizi zipo taasisi za Serikali ambazo ukizifanya Strategic Business Unit (SBU), ukamtafuta mtu mahiri ukamkabidhi badala ya wewe kumpa ruzuku atakupa ruzuku. Mojawapo ya taasisi ni NARCO, NARCO wana hekta laki sita za ardhi, hawawezi kufuga, hawawezi kuuza maziwa, sio mabingwa wa kuuza nyama, sio mabingwa wa chochote. Ardhi wanayo, tatizo lake ni under capitalization.

Mheshimiwa Spika, TAFICO, sisi tuna kilometa 1200 za bahari, tuna shirika linaitwa TAFICO - Kampuni ya Taifa under capitalization, hawana neli, hawana kasia, hawana hata mtumbwi. Kwa hiyo, tunapaswa kuleta watu kuwapa, tuwape kazi kwa masharti kusudi waweze kutekeleza na kuilipa, tuajiri watu.

Mheshimiwa Spika, kitu kingine nilichokiona katika miradi hii tumeajiri wakandarasi na wengi wenye miradi mikubwa ni wakandarasi kutoka nje; tunawalipa mamilioni ya pesa wanapeleka wao huko kwao, lakini miradi wanayofanya si ya kiajabu, si miujiza. Tunao vijana wetu kwenye taasisi za Serikali, tunao Watanzania wenzetu tuwakamate hawa watanzania kwa masharti magumu tuwakabidhi kazi, tuwaangalie watengeneze. Hauwezi kutafuta pesa ukamlipa mtoto wa jirani wakati mtoto wako anakufa njaa, tuwasimamie waweze kufanya, ndivyo walivyofanya nchi nyingine, ndivyo wanavyofanya Urusi, ndivyo wanavyofanya Rwanda na duniani kote. Mtoto wako unamrekebisha huwezi kusema mapungufu yam toto wako, Mrekebishe. Ndivyo tulivyofanya kazi kwenye Wizara ya Nishati wakati wa REA na aliiasisi Mheshimiwa Muhongo. Hawa wakandarasi mnaowaona Watanzania walitafutwa, walikuwa hawajui lolote na wakaweza kufanya kazi. Ndio maana hata ndani ya TANESCO iko Kampuni ya TANESCO inapewa kufanya kazi ambazo tungeita watu wageni waje kuifanya hiyo kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo tuliloliona katika Kamati ileā€¦

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Sekunde thelathini naambiwa kengele imeshagonga.

MHE.CHARLES P. MWIJAGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, nizungumze la mwisho la haraka. Tumepanga pesa kwa ajili ya kutekeleza miradi, lakini utaratibu wetu wa mnyororo wa manunuzi, procedure ya PPRA ya manunuzi; unakuta pesa mmepewa, mchakato wa ku-release pesa kutafuita mkandarasi unakuchukua miezi sita, mwaka umekwisha. Kwa hiyo mradi hauishi.

Mheshimiwa Spika, hizi bureaucracy, necessary devils tujaribu kuzifupisha kusudi miradi iweze kutekelezwa kwa wakati. Ikiwezekana miradi ya mwaka kesho basi tuanze leo kutafuta mkandarasi kwa sababu tunajua pesa tutazipanga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nishukuru kazi iliyofanywa na Wizara ya Kilimo ya kuendeleza Bonde letu la Mto Ngono, tunataka sasa lilimwe wananchi waweze kupewa vizimba waweze kulima na kufuga samaki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono kazi ya Kamati yangu. (Makofi)