Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Joseph George Kakunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sikonge

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana kunipa nafasi ili nami nichangie hoja ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Nianze kwanza kwa kuwapongeza Viongozi wetu wa Chama cha Mapinduzi na Serikali chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuongoza vizuri nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kihistoria daima tutawaenzi baba zetu 13 na Mama yetu mmoja kwa kuiongoza nchi hii vizuri tangu tupate uhuru. Baba zetu wanane wameiongoza Serikali ya Mapindu Zanzibar na baba watano na mama yetu mmoja wameongoza Jamhuri ya Muungano wa Tanzania vizuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niweke katika historia ya kumbukumbu. Daima tutamkumbuka baba wa Uhuru na Umoja wa taifa hili, Marehemu Mwalim Julius Kambarage Nyerere, tutamkumbuka baba wa mageuzi ya kiuchumi na kisiasa Mzee Ally Hassan Mwinyi, tutamkumbuka baba wa Sera za Uwazi na Ukweli Muasisi wa sera na mikakati ya kuondoa umaskini Tanzania, Mzee Benjamin William Mkapa ambaye alituachia Dira ya Maendeleo ya Taifa inayotekelezwa tangu mwaka 2000 mpaka mwaka 2025.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna wenzangu waliwahi kutamka hapa kwamba hatuna dira wala maono. Tunayo Dira ya Taifa ya Maendeleo ambayo tumeendelea kutekeleza kwa mipango ya miaka mitano mitano na mipango ya mwaka mmoja mmoja kama huu ambao tunajadili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vilevile tunamkumbuka baba wa siasa za maridhiano ya Kitaifa Mzee wetu Jakaya Mrisho Kikwete na pia tunamkumbuka baba wa ujenzi wa miundombinu na umiliki wa rasilimali za Taifa Marehemu Daktari John Pombe Joseph Magufuli. Na sasa tunaye Mama yetu ambaye ameithibitishia Dunia, narudia, ameithibitishia Dunia huruma yake kwa kila mtanzania kupitia kazi zake zinazopeleka maendeleo kila pembe ya nchi, hata maeneo ambayo yalikuwa hayajawahi kuona darasa jipya sasa mwaka jana yameona darasa jipya. Wanachi wa Uswada kule Kitunda, wananchi wa Idimbwa kule Kitunda sasa wameona darasa jipya kwa sababu ya juhudi za Mama Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Rais wetu kesho ataondoka nchini kwenda Marekani kwenda kuzindua filamu ambayo inatangaza utalii wa Tanzania. Nikiri wazi kwamba mwanzoni sikuelewa filamu hii itakuwa na manufaa gani, lakini baada ya kudadavua takwimu ambazo zinaweza zikaletwa na utalii utakaongezwa kupitia filamu hiyo, ninampongeza sana Rais wetu kwa kwenda kesho Marekani kuzindue hiyo filamu, na tunategemea mafuriko ya watu kuja kuiangalia nchi hii, kwenda kuangalia vivutio vya utalii katika nchi hii. Na utalii umekuwa na mchango mkubwa sana kwenye pato la Taifa, kwa hiyo siyo jambo ndogo alilolifanya Mheshimiwa Rais wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na nchi hii ina orodha ya Viongozi wa kujivunia hawastahili kubezwa hata Kiongozi mmoja, tumefanya vizuri sana. Naomba historia zao ziandikwe katika vitabu watoto na wanafunzi wasome shuleni na vyuo vikuu ili taifa hili liendelee kuuliziwa kupitia Uongozi wao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mambo ya msingi ya kushauri. Jambo la kwanza ni mfumko wa bei. Yamesemwa mambo mengi sana kuhusu mfumko wa bei. Leo nilikuwa nasoma the Washington Post kuhusiana na inflation ya Marekani, linasema hivi, nanukuu “The consumer price index is expected to come in at hooping 8.4 percent this April. America hasn’t witnessed inflation levels above 80 percent since 1981.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana yake nini? Ina maana Marekani wanalia inflation, Uingereza wanalia inflation. Na sababu za mfumko wa bei Kimataifa ziko tatu, sababu ya kwanza ni lockdown, sisi hatujaona lockdown ndiyo maana tunashangaa wenzetu Marekani na nchi nyingine walifungia watu wao ndani na hakuna kutoka, halafu wakaanza kugawa fedha za bure hazina jasho. Matokeo yake demand ya vitu vya matumizi ya nyumbani ikaongezeka, hasahasa demand ya vyakula na bidhaa za umeme. Na hiyo ndiyo imesababisha inflation Dunia nzima. Sisi tunahangaika na imported inflation. Mtawaparura bure Mawaziri hapa wakati ambapo inflation zingine zimeletwa kutoka nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sababu ya pili ni kufungwa kwa viwanda vya uzalishaji kulikosababisha bidhaa kupungua, hasa mbolea, na ndiyo maana bei ya mbolea bado ipo juu sana. Halafu ya tatu ambayo imegongelea msumari ni vita ya Urusi na Ukraine ambayo vimeongeza chumvi kwenye kidonda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuna haja ya kugomba kwa sababu ya inflation inayotuathiri kwa sasa hivi, sababu zinajulikana. Naomba tuungane na Serikali na kuhakikisha kwamba hatua ambazo zinachukuliwa na Serikali tunaziunga mkono.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina ushauri katika maeneo machache. Eneo la kwanza ni kuhusu Benki ya Kilimo (TADB) mwaka jana Benki Kuu ilitoa fedha Shilingi trioni moja ili zipewe Mabenki waweze kukopesha wananchi. Mojawapo ya ambayo Benki tulitegemea ipate hizo hela ni TADB, lakini haikupata hata senti moja kwa sababu Benki hii ya TADB, Benki ya Maendeleo ya Kilimo haikuwa na vigezo vya kuweza kupata hizo fedha, matokeo yake haikupata hata senti tano. Ninaomba Serikali na kuishauri Serikali yangu sikivu wekezeni kwenye TADB ili ipate vigezo vya kukopesheka nayo iweze kukopesha wakulima maana hii ni Benki ya wakulima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wa pili ni muhimu sana Serikali iwe na buffers of fund, fedha ambazo ni maalum kwa ajili ya kununua mazao endapo soko la mawazo litakuwa si nzuri kwa wakulima wetu ili wakulima waweze kupata jasho lao vizuri, thamani ya jasho lao. Ushauri wa tatu Mfuko wa Pembejeo, naomba Mfuko wa Pembejeo usitumike kukopesha tu mikopo midogo midogo. Mfuko wa Pembejeo utumike vilevile kuweka fedha za ruzuku kwa ajili ya mahitaji muhimu kama pembejeo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wa nne, naomba Wizara ya Kilimo iangalie mazao mengine. Kwa mfano kule kwetu zao la pilipili limeanza kulimwa na watu wengi. Ninaomba msaada wa Wizara ya Kilimo ilete wataalam kuwashauri wananchi namna gani walime zao pilipili ambalo litaongeza pato kutoka kwenye pato la tumbaku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu wa tano, ninaomba Serikali itunge haraka sera ya ufuatiliaji na tathmini ili kuimarisha ufuatiliaji na tathmini. Ni ufuatiliaji na tathmini katika nchi nyingine ndio unapunguza maswali ya ukaguzi, ukaguzi wa ndani na ukaguzi wa nje unapunguzwa na M&E. Sasa ninaomba Serikali hapa Tanzania itunge haraka Sera ya ufuatiliaji na tathmini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wa sita, Serikali iuangalie mfumo wa Ajira. Mfumo wa ajira umeanza kukosa imani wanaotafuta ajira. Kila siku sasa imeanza wanaamini kwamba bila kiongozi hawezi kuajiriwa, bila Mbunge hawezi kuajiriwa, bila Waziri hawezi kuajiriwa. Mfumo huu uangaliwe vizuri ili wanaotafuta ajira warudia kuuamini, wauamini vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu wa mwisho, yametajwa sana kuhusu MSD, lakini mimi nataka nishauri Meja Jenerali Gabriel Sauli Mhidize ambaye ndiye Mkurugenzi Mkuu wa MSD ni miongoni mwa wazalendo wakubwa wachache waliowahi kupatikana Tanzania. Ninaomba Serikali isitoe uamuzi wa haraka haraka fanye uchunguzi, fanyeni uchunguzi wa kina mtagundua kwamba Jenerali Mhidize ni mzalendo ambaye anataka kusaidia Watanzania. Na mkikamilisha uchunguzi huo naamini mtampa tuzo.

Mheshimiwa Mwenyekiti huyu mtu amejaribu kutaka kuwasaidia wagonjwa wa figo, amekwenda mpaka kwenye viwanda anasema viwanja vinazalisha chombo ambacho kitarahisisha wagonjwa wa figo wapunguziwe gharama. Kutoka shilingi laki tano mpaka laki moja na 30. Sasa kwa nini tusimuunge mkono mtu kama huyo? Tatizo kubwa lililopo pale ni kwamba kuna wafanyabiashara ambao wanafaidika na biashara ya dawa na wana cartel zao ndiyo ambao wanahakikisha huyu Jenerali Mhidize hafanikiwi katika… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)