Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Sylivia Francis Sigula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. SYLVIA F. SIGULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia katika Hotuba ya Waziri Mkuu. Kwanza na mimi niungane na wenzangu kumpongea Rais wetu mpenda Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya ya kutuletea maendeleo Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nimepitia Hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu inayohusiana na vijana, ajira na watu wenye ulemavu; na mimi ningependa sana nijikite kwenye ajira. Changamoto kubwa ya vijana ni ajira na sisi wawakilishi wa vijana ajenda yetu namba moja ni suala la ajira kwa vijana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni wazi kabisa kuwa hatuwezi kutatua matatizo au kero ya ajira kwa kutegemea asilimia nne za mikopo ya halmashauri, haiwezekani. Kwa hiyo Wizara hii imepewa jukumu kubwa la kusimamia ajira za vijana. Nilitarajia kuona tuna mpango maalum wa namna gani tunakabiliana na hii changamoto ya ajira kwa vijana (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma ukurasa wa 62 wa Hotuba ya Waziri Mkuu, anasema kwamba asilimia 87.8 ya vijana wana ajira; ajira rasmi na ajira zisizo rasmi, either wamejiajiri au wameajiriwa. Sasa utaona kama asilimia 87 wana ajira na waswahili wanasema no research no right to speak nadhani wataalam wataelewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka kuzungumzia nini hapa? Unaposema asilimia 87 wana ajira ninaamini kabisa ajira ambazo zinakuwa nyingi hapa ni ajira zisizo rasmi. Unapozungumzia ajira zisizo rasmi ziko nyingi, kuna ajira nyingi bodaboda, kuna mama ntilie, kuna baba ntilie, kuna mmachinga na wafanyabiashara wengine wadogo, hawa wanaingia kwenye ajira zisizo rasmi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nina ushauri kwa Serikali. Kwamba, tunapotaka kukabiliana na hii changamoto ya ukosefu wa ajira kwa vijana natamani sana kuona tunawekeza nguvu kubwa katika ajira zisizo rasmi kwa sababu ndizo zinazoajiri watu wengi. Ninaonge haya na nitatoa reference kwa kutumia bodaboda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bodaboda ambazo tumeingiza nchini kuanzia 2017 mpaka leo 2022 ni bodaboa Milioni 1,279,455 na tumeweza kuipatia Serikali zaidi ya bilioni 117. Hapa nataka kuzungumza nini, ukifanya takwimu ya vijana ambao wamejiari kwenye bodaboda kwa Mkoa wa Dar es Saalam tu wako vijana 136,431. Ukija Mkoa wa Mwanza wako vijana 86,218. Ukija Mkoa wa Dodoma wako vijana 58,316. Ukija Mkoa wa Kigoma wako vijana 36,411. Sasa, unapofanya rafli ya hawa vijana wa bodaboda nchi nzima ni zaidi ya 2,090 na kuendelea huko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama sekta hii inaweza ikaajiri vijana wengi namna hii, naona ni muda mwafaka sasa wa Serikali kuweka kipaumbele katika sekta hii. Sekta hii ya bodaboda imeachwa, imeachwa vijana hawanufaiki wanateseka lakini imeachwa Serikali pia haipati mapato kupitia bodaboda. Na hapa nataka nielezee kitu gani? Unapozungumzia vijana milioni 2,092 ambao wamejiajiri kupitia bodaboda hawa ni vijana mchanganyiko; wako vijana ambao wana elimu na ambao hawana elimu.

Hapa kinachotokea kitu gani? Changamoto yao kubwa ni suala la leseni. Ili kijana apate leseni anahitaji kuwa na 83,000. Hali mtaani ni ngumu vijana wanalia, ajira hakuna, abiria hakuna, hiyo 83,000 anaipata wapi huyu kijana? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kukosa hiyo 83,000 lakini anapokuwa hana hiyo 83,000 hana leseni lakini hajapaki yuko barabarani. Nini kinatokea hapa? Badala ya Serikali kukusanya mapato kupitia hizo leseni Serikali haipati mapato na kijana anaishia kutoa elfu tano tano, elfu mbili mbili kwa Askari ili aendelee kuwa barabarani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu kwa Serikali is either tupunguze hii bei ya leseni ni kubwa sana, tunaweza kufanya leseni ikawa 40,000 na Serikali ikapata mapato kuliko hivi tunavyofanya sisi, kuwaachia wenyewe wajifanyie. Au tunaweza tukatengeneza mfumo hawa vijana wakalipia leseni kwa installment na Serikali ingeweza kupata mapato mengi na vijana wangeweza kunufaika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma Tax Administration Act inamtambua mlipa kodi. Unapokuwa na biashara inayoingiza zaidi ya milioni nne unatakiwa usajiliwe kama mlipa kodi. Lakini wapo watu wanafanya biashara hizi za bodaboda, ana bodaboda tatu mpaka nne; lakini kwa sababu Serikali imeacha wazi hawa watu hawalipi kodi na Serikali inazidi kupoteza mapato na vijana wengi wanaendelea kunyanyasika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ustawi wa taifa letu ukisoma ukurasa wa 55 unatambua kabisa kwamba vijana ndio nguvu kazi ya taifa hili kwa asilimia 55. Sasa kama vijana ni nguvu kazi, embu tuwasaidie kuwaokoa na hali wanayopitia. Bodaboda kwa sababu wameachwa wazi tunapata majeruhi wengi Serikali inaingia gharama kuwatibu lakini inaendelea kupoteza nguvu kazi ya taifa. Kwa kuwa tumeshindwa kusimamia suala la bodaboda Serikali inapoteza mapato na bodaboda wanazidi kuteseka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, natambua Serikali imetoa bilioni tano kwa ajili ya machinga lakini tunatoa bilioni tano kwa ajili ya miundombinu. Je, tunashindwa kuwapatia mikopo hiyo miundombinu tunayoianzisha ni nani atakayeenda kuitumia kama vijana hawa hawana mikopo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tusidanganyane hapa hatuwezi kuhamasisha vijana wajiari kama hatutawapatia mikopo. Vijana wanahitaji mitaji ili waweze kujiari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia sasa hivi ukiangalia hospitali nyingi zina wodi maalum kwa ajili ya majeruhi wa bodaboda. Mimi niiombe Ofisi ya Waziri Mkuu isimamie sekta hizi. Bado Wizara ya Mambo ya Ndani haijafanya kazi yake vizuri zaidi ya kutengeneza ugomvi kati ya bodaboda na Askari. Lakini pia kuna haja ya Wizara ya Uchukuzi kusimamia jambo hili ili kutengeneza kwa sababu hata bodaboda hii iko sehemu ya uchukuzi. Uchukuzi siyo ndege tu na meliā€¦ (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. SYLVIA F. SIGULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.