Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Michael Mwita Kembaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. MICHAEL M. KEMBAKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia katika mada hii. Kwanza ningeanza kumshukuru Rais wetu, Mama yetu, Mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri ambayo anaifanya katika kulijenga taifa letu la Tanzania. Kazi kubwa imefanyika katika Jimbo letu na katika nchi nzima amefanya kazi kubwa ambayo imetukuka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeanza kwa kusema katika Jimbo letu la Tarime Mjini kuna jambo ambalo haliko vizuri ambalo ningependa kulisemea kabla ya kuchangia mchango wangu. Katika Mji wetu wa Tarime kumetokea tatizo pale Mgogoro wa Bugosi na Jeshi la Wananchi wa Tanzania. Mgogoro ule umepelekea ng’ombe wanafuga pale wanakamatwa, na wale ambao wanachunga wanapigishwa mazoezi kweli kweli. Mmoja wao aliniambia siku hizi amenunua buti ili akitoa ng’ombe nje aweze kufanya mazoezi, ameshaanza kuwa mwanajeshi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wale wananchi wanaishi pale na walipaswa walipwe fidia waondoke ili waweze kuendelea na shughuli zao. Sasa kama mtu anaishi pale, anafuga mifugo yake lakini mifugo haipaswi kutoka nje kwa sababu itakamatwa; na pale ambapo inakamatwa wanalipishwa faini siyo chini ya shilingi laki tano. Ningeomba Serikali ione namna gani ya kutatua tatizo hili kwa kuwalipa fidia wananchi wale ili waondoke katika eneo lile ili Jeshi liendelee na sehemu yao kama kawaida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vile vile imetolewa pesa ya kujenga barabara na Halmashauri yetu imepokea zaidi ya shilingi milioni 450 kwa ajili ya kujenga barabara. Tayari wakandarasi wamesaini mkataba na mpaka sasa barabara zile hazijaanza kujengwa. Ningeomba Serikali sasa iingilie kati ili hao wakandarasi ambao wana-sign mikataba alafu hawaingii site kujenga barabara wachukuliwe hatua ili barabara zile, kwa nia njema ya Serikali ya kutaka barabara zijengwe basi hiyo dhamira itimie kwa kuwabana hawa wakandarasi waweze kujenga barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kuelekeza mchango wangu mwingine upande wa kuajiri wafanyakazi. Taswira ya taasisi ama kampuni yoyote ni wafanyakazi wake. Wafanyakazi namna wanavyofanya kazi, lugha wanayoitumia, namna wanavyojitoa katika kufanya kazi lakini pia namna wanavyojitoa kuhudumia wateja wao inaonesha taswira kamili ya taasisi husika. Na ndipo watu wanaweza kusema kwamba taasisi hii ni nzuri au taasisi hii ina tatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa sisi Watanzania tujiulize, kwamba watumishi wa Serikali na watumishi wanaoajiriwa na Serikali wakoje? Hali ikoje katika taasisi za kiserikali? Katika hospitali watumishi hawa wakoje? Shuleni na Katika taasisi zingine kama TANESCO watumishi hawa wakoje? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lugha zinazotumika katika taasisi hizo za Serikali ikiwemo hospitali haziridhishi; na hii inasababishwa na nini? Hebu turudi nyuma namna watu wanavyoajiriwa Serikalini. Kwa mfano waliomaliza elimu mwaka 2014/2015 wamekuwa nyumbani tangu 2015 mpaka 2021 walipoajiriwa. Katika kipindi hiki chote watumishi hawa ambao wameajirwa walikuwa wanaendesha bodaboda, wengine walikuwa wafanyabiashara. Sasa wanapokuja kuajiriwa baada ya miaka sita miaka mitano unakuta knowledge yake, ufahamu wake, ujuzi wake haupo tena anaenda kuanza upya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii inasababisha utendaji kazi kwa watumishi katika Serikali yetu unakuwa chini ya kiwango; lakini pia hata lugha zile ambazo wanatumia unakuta tayari wameingia wengine unakuta ni bodaboda, wengine ni machinga; kwa hiyo anapoenda pale anaanza kujifunza upya. Mimi ningependa kushauri itungwe sheria, kwamba wahitimu wote wanaotoka elimu ya juu wajitolee katika Idara za Serikali kulingana na idara waliopo. Kwa mfano, kama ni Madaktari wakirudi kwao waanze kujitolea katika hospitali, kama ni Walimu warudi kujitolea shuleni, kama ni Ma-engineer warudi kujitolea katika maeneo yao ili kuwasaidia ku-gain ujuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kujitolea kunasaidia mtu kuweza kuongeza na kukuza maarifa. Kujitolea ni tendo la huruma, ni tendo la kuonesha fadhila kwa taifa. Lakini vile vile tukitunga sheria hii, Serikali itaondokana na uhaba wa wafanyakazi uliopo katika taasisi zetu. Kwa mfano katika Mji wetu wa Tarime madaktari sita tu kati ya 15 wanaohitajika. Lakini kuna madaktari wengi ambao wako nje ambao wamehitimu elimu lakini hawana kazi. Kwa hivyo wakijitolea, Serikali kwanza itakuwa imepata nguvu kazi itakayosaidia kulijenga taifa letu pamojan na kupunguza matatizo wanayokabiliana nayo kwenye upungufu wa watumishi katika idara mbali mbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia vijana wengi wanaohitimu elimu ya juu unakuta wametumia gharama ya Serikali kama mikopo lakini hawapati nafasi ya kurudisha ile mikopo kwa sababu hakuna ajira. Wakijitolea ninaamini watakuwa wamelipa fadhila kwa kodi ya wananchi wameitumia wakati wanasoma… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE: MICHAEL M. KENDAKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.