Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa fursa hii nitumie nafasi hii. Kwanza kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kutupa nafasi hii kuweza kujadili mambo mbalimbali yanayotugusa na yanayogusa jamii yetu. Nimshukuru sana pia Mheshimiwa Rais na kumpongeza kwa kazi kubwa sana anayoifanya kwa ajili ya kuleta maendeleo kwenye taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ya pekee nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Mkuu na timu yake yote kwa hotuba nzuri iliyowasilishwa ambayo kwa ujumla wake inaota muelekeo wa nini kimefanyika nini kinapaswa kifanyike. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nafasi hii nitachangia kwenye maeneo machache. La kwanza, mwaka 2020 Mheshimiwa Waziri Mkuu alifanya ziara pale Ukerewe; haya ni yanayohusu jimbo langu. Tukiwa kwenye Kisiwa cha Ilugwa tuliwasilisha ombi letu kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kutambua changamoto za afya zilizo kwenye eneo lile, tukaomba tusaidie Serikali iweze kutujengea kituo cha afya kwenye Kisiwa cha Ilugwa. Nitumie nafasi hii kuishukuru sana Serikali, kwa hatua ya awali tumepata Milioni 250 na kituo kile kimeanza kujengwa kwa hiyo, tunashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vile vile tuliwasilisha ombi la kusaidia kupandisha hadhi ya Hospitali yetu ya Wilaya ya Nansi pamoja na ile ya Kisiwa cha Ukara. Ombi lile Mheshimiwa Waziri Mkuu alilichukua ,na nashukuru vilevile Serikali imeweza kulifanyia kazi; na hatua iliyopo sasa kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Nansio tayari mkandarasi amepatikana na Serikali imetupa pesa takriban bilioni tatu, jambo ambalo litasaidia sana kusaidia wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe tu Serikali itusaidie, kwamba maadamu wakandarasi wamepatikana basi mkataba usainiwe haraka na kazi ifanyike kwa mapema ili ianze kutoa huduma kwa wananchi ambao wanaathirika sana na jiografia ya eneo lile kuweza kupata huduma kwenye maeneo ya Mwanza Mjini na kadhalika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tulimueleza Mheshimiwa Waziri Mkuu alivyokuja pale. Aliyekuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Hayati Dkt. Magufuli mwaka 2018 tulimueleza tatizo la barabara kilometa 14 kutoka Lugezi kwenda Nansio Mjini, na akatoa maelekezo barabara ile ijengwe kwa haraka. Alipokuja Mheshimiwa Waziri Mkuu tulimueleza jambo hili akasema atalichukua ili iweze kufanyiwa kazi kwa haraka. Niombe sana Serikali itusaidie kilometa 14 hizi ziweze kujengwa kwa kiwango cha lami zinazotuunganisha kati ya Bunda na Nansio ili kuweza kuboresha uchumi wa watu wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kupitia Ilani ya Uchaguzi, Ilani ilielekeza, na wakati Mheshimiwa Waziri Mkuu anakuja Ukerewe tuliwaahidi wananchi wetu kwamba tutafanikisha upatikanaji wa vivuko, kivuko cha kutoka Bwiro kwenda Bukondo na vilevile kutoka Rugezi kwenda Kisolya. Niashukuru kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ukurasa wa 47 Serikali imedhamiria mwaka huu kulifanyia kazi jambo hili. Lakini niombe tu, pamoja na haya bado kuna maeneo mengine ambayo yanahitaji msaada wa haraka sana. Usafiri wa kutoka Bukindo kwenda Ilugwa pamoja na kutoka Kakukuru kwenda Kisiwa cha Gana ni muhimu sana ukafanyiwa kazi haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu kwenye hotuba ya Waziri Mkuu ni kwenye maeneo mawili sana sana. Kwanza eneo la Afya. Tukiangalia hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ukurasa wa 51 inaonesha namna gani Serikali yetu imefanya kazi kubwa sanaya kujenga vituo vya afya. awamu ya tano vimejengwa vituo zaidi ya 300, awamu ya sita mpaka sasa vimejengwa zaidi ya vituo 200, kwa hiyo utakuta kwamba tuna vituo karibu 600. Lakini bado kuna zahanati nyingi zimejengwa; na kwa sera yetu tuliyonayo tunatakiwa tujenge kituo cha afya kila kata, zahanati kila kijiji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nilikuwa nina wazo mbadala. Kwamba, badala ya kuendelea kujenga vituo vya afya na zahanati ilhali hizi ambazo tayari zimejengwa hazitoi huduma zile tulizozitarajia kwa wananchi wetu ninaona kama litakuwa si jambo jema sana. Ushauri wangu, ningeshauri kwamba maadam tayari tumejenga vituo hivi zaidi ya 500 tuna zahanati nyingi lakini bado hakuna watumishi, hakuna vifaa tiba na kadhalika, angalau tungeweka pending kwa mwaka mmoja ili ile pesa ambayo tungeendelea kujenga vituo hivi vya afya tuweze kuboresha vituo hivi ambavo tayari tumejenga ili vipate vifaa tiba kwa mfano x-ray machines, ultra-sound, darubini na kadhalika. Pia vipate watumishi wa kutosha ili wananchi wetu waliopo kwenye maeneo haya waweze kupata huduma, na baada ya hapo sasa tufanye tathimini nini kinatakiwa tena kiweze kujengwa kama ni kuendelea basi yale maeneo ambayo ni strategic area yaweze kuendelea kujengewa vituo vya afya wakati huo haya ambayo tayari yamekwisha pata vituo, vituo hivi viwekwe katika mazingira ambayo yanaweza kusaidia watu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini eneo lingine ambalo nilitamani kuchangia nii kwenye eneo la elimu. Nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa pesa zile za UVIKO 1.3 trillion angalau kwenye maeneo ya sekondari imesaidia. Sasa niombe, kwamba kilichofanyika kwenye eneo la sekondari kifanyike vilevile kwenye eneo la primary kwa kuwa kuna shida kubwa sana kwa sababu hakuna madarasa hakuna nyumba za walimu ikifanyika kwa namna hiyo one time investment inaweza kusaidia sana kuondoa changamoto zilizopo vilevile kwenye eneo la shule za msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana.