Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. January Yusuf Makamba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bumbuli

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa fursa ya kuzungumza na napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa hotuba nzuri aliyoitoa na kwa mipango mizuri ya Wizara.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika taasisi ambapo uongozi unafundishwa vizuri kwa nadharia na vitendo ni pamoja na jeshini na hii ni kote duniani, iwe West Point, Sandhurst au Monduli. Tangu nchi yetu ipate uhuru, viongozi wa Taifa hili tangu Baba wa Taifa mpaka Rais Magufuli wameenda jeshini kuchota katika kisima cha hazina ya uongozi iliyopo jeshini ili kusaidia kuongoza nchi yetu. Askari wetu wote walioombwa au walioteuliwa kutumikia nafasi za uongozi katika nchi na katika siasa kutoka jeshini wamefanya kazi nzuri na kubwa na mifano iko mingi, Jenerali Kimario, Jenerali Sarakikya, Jenerali Luhanga na wengineo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivi kwa sababu katika hotuba ya Kambi ya Upinzani, ukurasa wa 12 kuna hoja imetolewa pale, kwamba ili kulinda na kusimamia maadili ya kazi ya jeshi, Wanajeshi wasihusishwe kabisa na kazi za siasa iwe wapo kazini au wamestaafu. Wanaendelea kusema kwamba kwa kuwateua kushika nafasi za siasa wanapostaafu, kunaweza kuwafanya wale wengine waliopo kazini kutozingatia maadili yao ya kazi na kuanza kujipendekeza kwa watawala. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika ngazi kumi za uafisa jeshini, ngazi saba Rais ndiye anayepandisha vyeo. Kwa hiyo, kama kuna hoja ya kujipendekeza kwa Askari wetu, isingekuwa kwenye ngazi za siasa hata kule kule waliko jeshini kama tunaamini kwamba kwa weledi wao na mafunzo yao wametengenezwa na wamefundishwa katika hulka za kujipendekeza ingekuwa tunaiona kuanzia sasa kwa sababu bado Rais anapandisha vyeo jeshini. Kwa hiyo, nadhani kwamba ni kuwadhalilisha Askari na Maafisa wetu kwa kusema kwamba wanajipendekeza kwa watawala ili wapate nafasi.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Naibu Spika, Jeshi letu limewekwa chini ya mamlaka ya kiraia na sisi viongozi wa kiraia tunapigiwa saluti wakati mwingine na Askari. Leo wakati tunapitisha bajeti hii, wamekuwepo Askari na Maafisa wengi na wameshuhudia jinsi tunavyoendesha mambo yetu, nadhani baada ya kupitishwa bajeti hii na naamini itapita, tutakapokuwa tunarudi nyumbani kwetu tutafakari kama waliyoyaona tunayafanya Askari wetu leo hapa kama kweli watatupigia saluti huku ndani ya mioyo yao wakiwa hawaamini kama tunazistahili kama watakuwa wanakosea. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu wa Spika, naomba nimalizie kwa kuwashukuru Askari wetu wote, Maafisa na wale wanaowaongoza kwa kuendelea kuifanyia kazi nzuri nchi yetu. Napenda kuwashukuru binafsi kwa kutuongoza na kufanya kazi vizuri. Napenda makusudi kabisa niwataje kwa sababu huwa hawatajwi hasa viongozi wale, Mkuu wa Majeshi yetu Jenerali Mwamunyange, ahsante sana. Mnadhimu Mkuu Lieutenant General Mabeyo, ahsante sana. Mkuu wa Kamandi ya Jeshi la Nchi Kavu, Meja Jenerali Mwakibolwa ahsante sana. Mkuu wa Kamandi ya Jeshi la Wanamaji, Rogastian Laswai, ahsante sana. Mkuu wa JKT, Brigedia Jenerali Isamuhyo, ahsante sana. Mkuu wa Kamandi ya Jeshi la Anga, Brigedia Jenerali Ingram, ahsante sana. Mnastahili shukrani zetu sana kwa kazi nzuri mnayoifanya, kwa sacrifice mnayoichukua kulinda mipaka ya nchi yetu, kulinda amani ya nchi yetu na wakati mwingine maneno ambayo yanasemwa humu ndani ya kuwadhalilisha hamuyastahili na Watanzania wote wako nyuma yenu, ahsanteni sana.