Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Kasalali Emmanuel Mageni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sumve

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi hii. Pia namshukuru Mwenyezi Mungu kwa uzima na afya njema. Kabla sijaenda mbali sana, naomba nitoe haki kwa viongozi wa Wizara ya TAMISEMI, nikimaanisha Waziri, Mheshimiwa Bashungwa, Manaibu wake, Mheshimiwa Dugange na Mheshimiwa Silinde. Kwa nini nimesema nitoe shukrani na pongezi kwa hawa watu?

Kwa uzoefu wangu nadhani na Wabunge wengine, hakuna Mawaziri rahisi kuwapata kama hawa jamaa. Ukiwa na shida yako ni rahisi sana kuwapata hawa Waheshimiwa (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba niwapongeze sana. Wamekuwa ni watu, wasikivu na ni wepesi wa kujibu shida za Wabunge. Ninapoleta shida TAMISEMI nakuwa na amani kwa sababu ya watu wanaosimamia Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani ni wakati muafaka kwa watu wengine kujifunza pia. Kuna Waziri mmoja mpaka nilimwandikia message nikamwambia Mheshimiwa Waziri nikitaka kukupata ninafanyaje? Kwa sababu huwezi kumpata. Ndugu zangu, zichonganishi lakini ninasema ukweli, mmekuwa watu wema sana, mnatusaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nijielekeze kwenye kuwashauri hawa ndugu zangu wema. Wizara ya TAMISEMI ni Wizara kubwa sana, inasimamia vitu vingi sana. Mheshimiwa Rais amewapa kazi kubwa sana ya kusukuma maendeleo. Mheshimiwa Rais anatafuta fedha, analeta kwenye maendeleo. Sisi sote ni mashahidi na nchi ni shahidi, kama kuna wakati miradi ya maendeleo imepelekwa vijijini kwa watu, ni wakati huu wa Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan. Sasa ninyi TAMISEMI ndiyo mna jukumu la kusimamia hizi fedha Mheshimiwa Rais anazotupelekea kwenye maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wasimamizi wa hizi fedha, leo ninarudia, kwenye bajeti iliyopita nilisema, nashukuru Serikali sikivu ilinisikia, ikahamisha posho za Madiwani katoka kulipwa kwenye Halmashauri zikaanza kulipwa na Serikali Kuu; kwenye Bajeti iliyopita tulisema kuhusu Madiwani kutokulipiwa Bima zao za Afya, tunashukuru Serikali sikivu ya CCM imeamua sasa kuchangia Bima za Afya za Madiwani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, kada ya Udiwani ni muhimu sana kwako. Naweza kukwambia, inawezekana hawa ndio walinzi wa nyumba yako. Fedha zote zinazopelekwa Halmashauri, wanaozilinda ni hao Madiwani lakini walinzi wako hawana vifaa vya kulindia fedha. Unapeleka mabilioni ya fedha kwenye Halmashauri, lakini unawalipa watu shilingi 300,000 walinde mabilioni, siyo sawa na tunajidanganya. Fedha zetu zitaendelea kuliwa na kuibiwa kwenye Halmashauri mpaka siku tutakapotambua umuhimu wa Madiwani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nataka nichangie hili kwa uchungu kwa sababu wakati nipo Diwani, mfano nilipokuwa nikienda kwenye kikao, Halmashauri zetu hazifanani. Halmashauri ya Dar es Salaam na Ilala na Kwimba ni tofauti, inabidi mimi niende nikalale Ngudu kutoka Lyoma.

Kwa hiyo, siku ninapoenda kwenye kikao nilikuwa nalipwa night, nikiamka naenda kwenye kikao, kesho yake naenda kwenye kikao cha Kata, kesho yake kikao cha Full Council, siku inayofuata nitatoka jioni, nitalala, kesho yake naondoka. Nilikuwa nalipwa siku nne. Nashangaa sijui huu utaratibu umetoka wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi karibuni utaratibu umebadilishwa, Diwani anaambiwa yule anayelala, alale siku mbili; haya makabrasha wanayapitia saa ngapi? Ndugu zangu kama mnahudhuria vikao vya Madiwani yanakuja mabuku makubwa hivi, yanahitaji muda wa kuyapitia. Sasa wanayapitia saa ngapi? Cha ajabu siku za karibuni, na nilikwenda kumwona Mheshimiwa Waziri pale nikamwambia; Madiwani wameanza kulipwa, lakini wengi hawalipwi fedha za kulala, wanaambiwa aende arudi. Huu uzoefu ni wa wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Jimbo la Wilaya ya Kwimba kuna Kata ipo kilometa kama sita kutoka Halmashauri, inaitwa Kata ya Mwang’halanga, kuna mto pale wa Mahiga, ukijaa maji, Diwani kama kalala kwake, hahudhurii vikao. Kwenye Jimbo la Sumve, Kata ya Wala tunamshukuru Mheshimiwa Samia Suluhu amejenga daraja baada ya kumeomba. Diwani akilala kwake, ni kilometa kumi tu, hawezi kuhudhuria kikao. Nyambiti kuna Mto Solwe haupitiki mvua ikinyesha, ndio maana Madiwani walikuwa wanatakiwa wakakae kwenye Halmashauri wamalize vikao halafu waondoke.? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii akili ya kuanza kuwaambia Madiwani wahudhurie vikao warudi nyumbani, mmeitoa wapi? Otherwise mmeamua Halmashauri iwe shamba la bibi. Tutaibiwa kweli kweli, nakuhakikishia Mheshimiwa Waziri. Utakuja na bajeti hapa, tutakuwa tumepigwa, mtafukuza watu, mtasimamisha watu, lakini kama hamwelewi kuwawezesha Madiwani posho yao ya mwezi, unamlipa mtu shilingi 300,000/= unasema asimamie mabilioni; Mheshimiwa Waziri naomba sana, wewe ni msikivu, ni wakati sasa umefika Serikali kuelewa umuhimu wa Madiwani. Kama hamtaki kuelewa, mtaendelea kuibiwa, tutaendelea kukamata watu, kufukuza watu na tutakuwa hatujaisaidia nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu wa msingi kabisa ulikuwa ni huu. Nakushukuru sana. (Makofi)