Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kuniona. Awali ya yote, nichukue fursa hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu aliyeniwezesha kuwepo jioni hii kuchangia mjadala huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile napenda kutoa shukrani za dhati kwa Wanaliwale kwa kuniamini na niko tayari kuwatumikia. Vilevile napenda kuwapongeza wapiga kura Wanaliwale kwa kuiweka CCM kuwa Chama cha Upinzani Jimboni. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mjadala wangu nitaulekeza katika maeneo yafuatayo. Kwanza kabisa, msingi wa Mpango. Msingi wa Mpango tumeambiwa ni amani, utulivu lakini nataka nitoe angalizo hapa ni lazima tutofautishe uvumilivu wa watu wachache na amani. Nataka nitumie neno ukondoo, ukondoo wa Wazanzibar tusiuchukulie kama ni kigezo cha amani. Nataka nilihakikishie Bunge lako Tukufu kwamba ukondoo huu tusitegemee kwamba utakuwa ni wa kudumu. Kama tunakusudia huu Mpango utuletee matunda tunayokusudia ni lazima tuhakikishe kweli tunapambana kuhusu suala la amani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mpango huu tumeambiwa kuna kuimarisha elimu, mimi nitajielekeza kwa upande wa elimu. Hatuwezi kuimarisha elimu tukiwasahau walimu. Walimu wetu maisha yao ni duni sana. Hapa nataka niongelee jambo moja. Walimu wanapewa kazi nyingi sana, mimi naomba tufike mahali hawa walimu tuwapunguzie kazi. Nitoe mfano walimu hawa ndiyo wasimamizi wa uchaguzi nchi hii inapofika kwenye uchaguzi na madhara wanayoyapata ni pale ambapo Chama cha Mapinduzi hakijapita, huyu mwalimu aliyesimamia, aidha ni Mratibu au Mwalimu Mkuu ajira yake iko hatarini. Natoa mfano huu katika Jimbo langu la Liwale leo hii wako walimu ambao waathirika kwa matukio haya. Sasa hatuwezi kuboresha elimu iwapo walimu hawana utulivu, walimu wanaidai Serikali, naomba tuliangalie hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja kwenye sekta ya afya. Tusitarajie mpango huu unaweza ukafanikiwa iwapo watu wetu hatujawajenga kiafya. Kwa upande huu wa afya nafikiri siasa imekuwa nyingi kuliko utekelezaji. Kama ambavyo watangulizi walivyosema nchi yetu watu ni wapangaji wazuri sana na mimi nasema huu Mpango tukiamua kuuza kwa nchi yoyote wakiutekeleza miaka mitano ijayo watakuwa mbali sana, lakini kwa Watanzania Mpango huu hatuwezi kufanikiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, nchi yetu imekuwa na mipango mingi sana na kitu kikubwa sana nachokiona mimi ni kwamba nchi yetu inaongozwa na mawazo ya watu wachache. Leo hii tukibadilisha Waziri hapa Wizara hiyo itabadilika kwa kila kitu, hatuna common goal kwamba nchi inataka kwenda wapi, hilo ndiyo tatizo letu. Leo hii tukibadilisha Rais anakuja na mambo mengine. Mheshimiwa Mkapa alikuja na Mtwara Corridor baada ya Mkapa kuondoka Mtwara corridor ikafa. Mheshimiwa Kikwete alikuja na maisha bora na yenyewe sijui kama itaendelea. Pia alikuja na Bandari ya Bagamoyo na sijui kama kwa utawala huu kama hiyo bandari bado ipo.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Sasa kwa mtindo huu hatuendi kwamba kila Waziri, kila Rais atakayekuja na la kwake hatuna common goal kama Taifa. Hili limeshatuletea matatizo sana, nitoe mfano kwenye Jumuiya ya Afrika Mashariki tulipozungumzia habari za reli tulilalamika hapa, sisi tulikuwa walalamishi wakubwa sana, watu wa Uganda na Rwanda walipoamua kuondoka kujiunga kutengeneza reli tukaanza kulalamika, mnalalamika nini? Mnachelewa wenyewe halafu mnategemea wao wawasubiri hatufiki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijielekeze kwa upande wa reli, sidhani kama kweli tuna dhamira nzuri kuhusu hiyo reli ya kati. Hivi unampaje mtu kusimamia reli ya kati ana malori ya usafirishaji zaidi ya 5000, hayo malori ayapeleke wapi? Ana malori ya usafirishaji 5000 halafu mnamwambia asimamie reli ijengwe halafu yeye malori apaleke wapi akafugie kuku? Tuache utani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakumbuka Mheshimiwa Rais alipokuwa kwenye Bunge hili kama Waziri wa Miundombinu alisema Sera ya Taifa letu ni kuunganisha mikoa yetu kwa barabara za lami. Nisikitike kusema sisi Mkoa wa Lindi hasa Wilaya ya Liwale inaitwa Wilaya ya pembezoni, kwa mawazo yangu nikajua Wilaya ya pembezoni maana yake ni Wilaya inayopakana na nchi nyingine, lakini ndani ya Tanzania kuna Wilaya za pembezoni. Sisi Liwale tunapakana na Mkoa wa Morogoro, Ruvuma niambieni kama kuna barabara inayotoka Morogoro kuelekea Liwale, hakuna. Hatuongelei barabara za lami tunaongelea hata barabara za changarawe, kutoka Liwale kwenda Tunduru hakuna barabara. Wilaya ya Liwale leo iko pembezoni inapakana na nchi gani? Halafu mnasema tunaweza kwenda sambamba na huu mkakati, huu mkakati nasema kwamba hauwezi kwenda. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, narudi kwenye upande wa amani, tumewapa kazi Polisi kwamba wao ndiyo walinzi wa amani, lakini nipende kusikitika kwamba hao polisi tunaowategemea wanaishi kwenye viota na mtaani. Hivi wewe polisi unakaa mtaani mwanangu anauza gongo utamkamata?
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Liwale imekuwa Wilaya mwaka 1975 mpaka leo hawana Kituo cha Polisi. Kituo cha Polisi cha kwanza kilikuwa kwenye gofu la mkoloni, NBC walipojenga nyumba yao wakahamia huko, ile nyumba ilikuwa ni ya mtu binafsi leo hii inamwaga maji kila mahali, mafaili yanafunikwa na maturubai halafu polisi hao hao ndiyo tunategemea walinde amani, hapo tunacheza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile naomba nijielekeze kwa upande wa sekta ya viwanda. Sekta ya viwanda hasa kwa sekta binafsi huku ndiyo tumekwama kabisa. Kama tumefika mahali tunawaacha vijana wetu wahangaike na hawa matajiri wakubwa, eti ndiyo wa-bargain mishahara. Mimi nasikitika jambo moja, sielewi imekuwaje. Zamani nilisikia wale ma-TX walikuwa na vibali vya kuishi miaka miwili leo hii tuna ma-TX kwenye viwanda vya watu binafsi mpaka wafagizi na madereva, sijui Uhamiaji wanafanya kazi gani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi mpaka naingia hapa Bungeni nina miaka 30 kwenye sekta ya watu binafsi, nimetembea zaidi ya viwanda sita, usiniulize kwa nini nimebadilisha viwanda vyote hivyo, ni kwa sababu nilikuwa sitaki kunyanyaswa. Haiwezekani leo hii tuna ma-TX, mtu ana cheti cha uinjinia ni dereva, ana cheti cha uinjinia anasimamia upakizi wa mizigo kiwandani, hii nchi imeoza, ni kama vile haina mwenyewe. Ndiyo maana nikasema kama ni kutunga sheria sisi tunaongoza kwa kutunga sheria nzuri sana na kama kwa mipango sisi tunaongoza lakini utekelezaji zero. Kama walivyotangulia kusema wenzangu, Waheshimiwa Mawaziri mliopewa dhamana nafuu msikilize Wabunge wa Vyama vya Upinzani wanasema nini, lakini mkiwasikiliza wa huko mtapotea na kama majipu ninyi mtakuwa wa kwanza. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijielekeze upande wa kilimo. Kilimo ndugu zangu hakiendeshwi na ngojera hizi za kilimo kwanza wala kilimo uti wa mngogo, tuna matatizo ya masoko. Nikupe mfano Mkoa wa Lindi, Wilaya ya Liwale, sisi tunalima korosho, ufuta, mbaazi lakini wakulima wetu sasa hivi bado wanahangaika. Mwaka juzi mbaazi ilipanda bei watu wakajikita huko, mwaka huu korosho zimepanda bei, ufuta umeshuka. Kwa hiyo, watu bado wanahangaika yaani wanalima kwa kubahatisha kwamba ukilima ufuta ikikuangukia bahati umepanda bei ndiyo unanufaika, ukivuna korosho mwaka huu imepanda bei ndiyo umenufaika. Hizi ngonjera za Kilimo Kwanza bila kutafuta masoko ya mazao yetu hatutakwenda huo mkakati ni wa kufeli. Mimi sijaona kwenye mpango huu wapi kumeelezwa suala kuimarisha masoko. Natoa angalizo hatuwezi kuimarisha kilimo kwa ngojera ya kilimo kwanza wala kilimo uti wa mngogo ni lazima tufanyekazi. (Makofi)
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.