Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Charles Muguta Kajege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mwibara

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii. Vilevile nichukue fursa hii kumshukuru sana na kumpongeza Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri sana anayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Mwibara sasa hivi limeanza kung’ara, namshukuru sana. Pia, naomba nichukue nafasi hii kumshukuru na kumpongeza Waziri wa TAMISEMI na wasaidizi wake pamoja na Katibu Mkuu wa TAMISEMI kwa kazi kubwa na jukumu kubwa sana walilonalo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitachangia katika maeneo yafuatayo: Kwanza ni katika sekta ya afya. Huduma za afya katika Jimbo langu la Mwibara bado haziridhishi. Tunavyo tu vituo vitatu vya afya vya Kasahunga, Kisorya na Kasuguti, lakini bado huduma zinazotolewa siyo za kiwango cha vituo vya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha kushangaza ni kwamba, hivi vituo vimejengwa kwa muda mrefu sana. Kwa mfano, Kituo cha Kasahunga kina zaidi ya miaka 20, lakini bado hakijakamilika. Kituo cha Kasuguti kina zaidi ya miaka 15 bado hakijakamilika na Kituo cha Kisorya kina zaidi ya miaka saba bado hakijakamilika. Naiomba Serikali yangu sasa hivi iweze kutufikiria vizuri sana na kutupa kipaumbele iweze kukamilisha vituo hivyo vya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni kuhusia na Mfuko wa Jimbo. Naipongeza sana Serikali kwa kuongeza fedha katika mfuko huu, lakini nataka niishauri Serikali, pesa hizi naomba zigawanywe sawa sawa katika kila Jimbo.

Hakuna formula ambayo tutatumia hapa ambayo itafanya Jimbo lingine liweze kupata inavyostahili. Hakuna formula nakwambia! Fedha hizi zigawanywe kama ambavyo zimegawiwa pesa za TARURA, kila Jimbo lipate pesa sawa sawa. Tukishagaiwa hivyo sasa, kila Mbunge atakwenda kupambana na mambo yake huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo letu la Mwibara lina ardhi ya kutosha na lina maji ya kutosha, tunachohitaji ni elimu sahihi na mafunzo sahihi ili tuweze kutumia fursa zilizopo katika sekta hizo za uvuvi na kilimo. Jimbo letu tumeshaenda hatua moja mbele katika kutafuta Chuo cha VETA. Kata yetu ya Butimba imetoa ekari 57 kwa ajili ya ujenzi wa VETA hiyo. Naomba Serikali sasa itufikirie katika mgawo wa VETA katika kipindi hiki ambacho kinakuja nasi tuweze kupata Chuo cha VETA katika Jimbo letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna shule kama tatu kongwe za msingi ambazo majengo yake yameshachakaa na baadhi ya viongozi wa elimu wamekuja na wamesema kwamba, hayo majengo sasa hivi hayastahili kutumiwa tena. Naomba Serikali yetu sasa iweze kufikiria namna ya kujenga shule hizi kongwe za zamani ili ziweze kuwa salama na ziweze kuendelea kutumika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hili suala la posho za Madiwani limezungumzwa na wenzangu wengi waliotangulia. Wakati wa kampeni tunasema tunakwenda na mafiga matatu, yaani Rais, Mbunge na Diwani, lakini baada ya uchaguzi sisi wengine tunawafungia nje hawa Madiwani, tunakuwa tena hatuwatendei haki. Pamoja na mapendekezo ambayo yametolewa kwamba posho zao ziongezwe angalau ziwe shilingi 800,000/= kwa mwezi, mimi naona kama bado hazitoshi. Nashauri angalau wapate shilingi milioni moja kila mwezi ili waweze kufanya kazi nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hao Madiwani ndio first responders wetu. Ndio wanaotatua matatizo ya wananchi sisi tukiwa huku Bungeni. Vilevile tusisahau kwamba na wao wanatumika kama ATM huko majimboni mwetu. Kwa hiyo, naomba nasi tuweze kuwafikiria waweze kupata posho ya kutosha waweze kufanya kazi zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni zaidi ya miaka 13 sasa hivi tangu mradi wa ujenzi wa barabara ya Bulamba hadi Kisorya ufanyike. Kuna wananchi ambao walitoa nyumba zao zikabomolewa kwa ajili ya kupisha mradi huu, lakini bado mpaka sasa hivi hawajalipwa.

Naomba Serikali yetu sasa iharakishe malipo ya hawa wazee ambao wengi wao sasa hivi maisha yao yamekuwa magumu; wengine walipoteza nyumba zao na kwa hiyo, wameshindwa kujenga nyumba zao upya.

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Ester Bulaya, Taarifa.

T A A R I F A

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naungana na kaka yangu kwa mchango wake mzuri. Ni kweli, hiyo barabara ni ya muda mrefu na ni kweli kwamba sio wananchi tu wa upande wa Jimbo la Mwibara, hata wa Bunda Mjini mpaka kwenda kule Nyamuswa na wenyewe mpaka sasa hivi hawajapisha na wametenga maeneo yao kwa sababu Wilaya ya Bunda wanahitaji barabara ya lami ambayo itaenda kuunganika na Arusha. Ahsante.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kajege, unapokea Taarifa?

MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naichukua kabisa na kuikubali hiyo Taarifa. Nami nasisitiza tena kwamba, haya malipo yafanyike mapema sana.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niishie hapo. Naunga mkono hoja hii ya TAMISEMI. Ahsante sana. (Makofi)