Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Edwin Enosy Swalle

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lupembe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa nafasi hii ambayo umenipa ili nami niweze kuchangia Wizara hii ya TAMISEMI. Kwanza kabisa nitumie nafasi hii kumpongeza sana Waziri, Mheshimiwa Innocent Bashungwa pamoja na Manaibu Mawaziri wake; Mheshimiwa David Ernest Silinde, Mheshimiwa Festo John Dugange na wataalamu wote wa Wizara hii ya TAMISEMI. Naomba ifahamike wazi kwamba, Wizara hii ni muhimu sana na ni roho ya wananchi wa Tanzania na tunawategemea sana.

Mheshimiwa Spika, nitumie pia, nafasi hii kumshukuru na kumpongeza sana Mheshimiwa Rais, Samia Suluhu Hassan, kwa uongozi wake mahiri wa mwaka mmoja ambao umekwenda kupita sasa. Tunapompongeza Mheshimiwa Rais, wako baadhi ya watu wanadhani pengine tunafanya utani.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, kwa upande wa Jimbo la Lupembe, ndani ya huu mwaka mmoja wa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, tulikuwa na Kata kama ya Ikondo ambayo tangu kuumbwa kwa ulimwengu wa dunia hii hakujawahi kuwa na kituo cha afya wala shule ya kata, lakini Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan amewafikia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tulikuwa hatuna shule shikizi kwenye maeneo kama ya Madeke na maeneo ya Itova. Ndani ya mwaka mmoja, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan amewafikia wananchi hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, siyo hivyo tu, wananchi wangu wa Mtwango pale Lunguya wamekuwa na shida ya muda mrefu ya barabara ya Lunguya kwenda Welela. Ndani ya mwaka huu mmoja tu Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan amewafikia wananchi hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia, Njombe DC tulikuwa hatuna Makao Makuu ya Halmashauri, Mheshimiwa Silinde alikuja mwaka 2021 kule; tulikuwa hatujaanza hata kujenga msingi, lakini ndani ya huu mwaka mmoja pekee, Mheshimiwa Rais ametuletea fedha shilingi bilioni 1,900 na hivi sasa ujenzi wa makao makuu upo kwenye level ya lenta. Nani kama Samia Suluhu Hassan? Kwa hiyo, Mheshimiwa Rais tunapompongeza Mheshimiwa Rais tunamaanisha na kazi anazifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaposhukuru hivi, ni ishara pia ya kuomba tena. Unaposhukuru ni kwamba, unataka kuomba tena. Halmashauri ya Njombe DC, pamoja na kazi nzuri ambazo Mheshimiwa Rais na Serikali imefanya, tunazo changamoto katika maeneo kadhaa ambayo napenda kuyabainisha. Kwanza alipokuja Mheshimiwa Silinde, Naibu Waziri, ikapendekezwa kujenga Makao Makuu ya Halmashauri. Eneo hili halina kituo cha afya. Kwa hiyo, eneo ambalo tunakwenda kujenga Makao Makuu ya Halmashauri patakuwa na watumishi wengi sana. Tunaiomba Serikali ipeleke Kituo cha Afya katika Kata ya Kidegembye.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, alipokuja Waziri wa TAMISEMI, Mheshimiwa Ummy, alituahidi kutupatia kituo cha afya kwenye Kata ya Ikuna na tulishauriwa kwamba, tusiendelee na ujenzi wa kile kituo cha afya badala yake tuelekeze nguvu kwenye ujenzi wa kituo cha afya kikubwa cha pale Mtwango kwa mapato ya ndani. Napenda kutoa taarifa, Halmashauri ya Njombe DC chini ya usimamizi wa Mkurugenzi wetu mahiri sana, Dada Sharifa Yusufu Nabarang’anya, tumeshajenga kituo cha afya kwa mapato ya ndani chenye majengo zaidi ya nane. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Halmashauri yetu imejenga kituo cha afya kwa mapato ya ndani kwa majengo zaidi ya nane, naiomba sana Serikali iwasaidie wananchi wa Mtwango, Ilunda, Welela, Sovi na Itunduma, kupata vifaatiba kwenye hospitali hii. Kama itapendeza pia wananchi hawa wangepata watumishi wa afya na vifaatiba na vifaa tendanishi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye hotuba ya Waziri amezungumza mafanikio mengi sana ambayo yamepatikana. Nilikuwa napenda kumshauri Mheshimiwa Waziri kwamba ufanisi huu wa TAMISEMI unasaidiwa pia na Wakurugenzi kwenye Halmashauri zetu. Napenda kutoa ushauri kwa Wizara, wapo Wakurugenzi ambao wamemwelewa sana Mheshimiwa Rais na wanafanya kazi nzuri sana, akiwemo Mkurugenzi wangu wa Njombe DC, dada yangu Sharifa. Nilikuwa namshauri, Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI, tunakokwenda, aanze kutoa zawadi maalum kwa Wakurugenzi wanaofanya vizuri kwa ajili ya motisha. Hili jambo litakuwa ni muhimu sana kuwatia motisha ili na Wakurugenzi wengine wajifunze kufanya kazi kwa ufasaha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia naomba kushauri kuhusu asilimia 10. Kwenye mchango uliopita hapa ndani, Mbunge wa Makete alisema kwa ufasaha kwamba fedha nyingi za mfuko za asilimia 10 hazirudishwi kwenye Halmashauri zetu. Ninayo maoni kwamba, utaratibu huu wa kutoa fedha kwenye vikundi pengine hauwezi kuwa na ufanisi sana. Nilikuwa napendekeza, hivi sasa wako wananchi wengi binafsi wenye uwezo wa kuwa na mawazo ya biashara, wanaoweza kubuni mradi, na kadhalika, badala ya kuendelea kutoa fedha kwenye vikundi vya watu watano hadi kumi, tungeruhusu hizi fedha akopeshwe mtu mmoja mmoja ambaye ana wazo zuri la biashara. Ninaamini mtu mmoja mwenye wazo zuri la biashara anaweza kuajiri hata watu 100 kuliko watu kwenye vikundi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunayo historia katika nchi hii, hizi biashara za watu wengi zimeshindikana huko nyuma. Tulikuwa na mashamba ya vijiji, tulishindwa kuyaendesha; tulikuwa na matrekta ya vijiji, tulishindwa kuyaendesha. Biashara ya watu wengi ni ngumu sana kufuatilia. Kwa hiyo, napendekeza tubadili sheria, tuanze kutoa mikopo kwa mtu mmoja mmoja mwenye ujuzi au mwenye mradi mzuri ilimradi tu ana sifa za kupewa mkopo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pale mwanzo palikuwa na hofu kwamba, kuwafuatilia itakuwa ni vigumu. Dunia inakwenda mbele. Sasa hivi tupo kwenye mchakato wa kuandikisha anuani za makazi. Wananchi wetu wana vitambulisho vya NIDA vya Taifa. Watu hawa wanajulikana waliko, tuwaamini, tuwakopeshe waweze kufanya maendeleo makubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)