Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Prof. Joyce Lazaro Ndalichako

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kasulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii na mimi nichangie hoja ya Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, nianze tu kusema kwamba naunga mkono hoja hii ambayo Mheshimiwa Waziri Mkuu ameiwasilisha kwa umahiri mkubwa sana.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ni mara yangu ya kwanza kuchangia nikiwa kama Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, naomba niruhusu nimshukuru kwa dhati Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuniamini na kuniteua katika nafasi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba pia nimshukuru Makamu wa Rais, Mheshimiwa Dkt. Philip Isdor Mpango na Waziri Mkuu Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, kwa miongozo ambayo amekuwa akinipatia ambayo imekuwa chachu ya ufanisi katika kazi zangu. Nampongeza Mheshimiwa Dkt. Hussein Ally Mwinyi Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kwa kazi kubwa ambayo anaifanya.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo hayo naomba nishukuru Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kwa maoni na ushauri waliotupatia na niwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote ambao wamechangia katika eneo la kazi, vijana na ajira na wenye ulemavu naomba nitoe sasa ufufanuzi katika hoja chache ambazo wamezichangia.

Mheshimiwa Spika, nitaanza na hoja ya Kamati na Waheshimiwa Wabunge wengine walichangia kuhusiana na program ya kukuza ujuzi nchi ambayo program hii inalenga katika kujenga ujuzi na kuondoa changamoto ya ajira kwa vijana. Waheshimiwa Wabunge wameona kuna changamoto ya watu wanaopata ujuzi, kwanza wanakubali kwamba program hii inatoa ujuzi ambao ni mzuri na muhimu kwa vijana lakini changamoto inakuwa namna ya kutumia ujuzi kwa sababu ya mitaji.

Mheshimiwa Spika Serikali inafanyia kazi jambo hili na kwa hatua ya kwanza tumewatambua vijana wote ambao wamepata ujuzi huu na orodha hiyo tumeikabidhi Ofisi ya Rais - TAMISEMI ili katika ile mikopo ya asilimia 10 wapewe kipaumbele, vilevile tunawapa kipaumbele katika fursa za uwekezaji ambazo zinajitokeza. Niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba Serikali itaendelea kutafuta fursa zinazopatikana ili iendelee kuwawezesha vijana ambao wanapata mafunzo haya.

Mheshimiwa Spika, niliambie Bunge lako Tukufu baadhi ya vijana ambao wamepitia katika program hizi wameweza kupata kazi katika miradi ya kimkakati kama ujenzi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere, ujenzi wa reli ya kisasa, pia alishiriki katika miradil ile ambayo ilikuwa inafadhiliwa na Mfuko wa UVIKO-19. Tutaendelea kutoa ujuzi na tutaendelea kutafuta fursa kwa vijana ili waendelee kunufaika na ujuzi unaoupata.

Mheshimiwa Spika, hoja nyingine imetolewa ya kuhusiana na gharama za vitalu nyumba kwa wale vijana ambao wanapata mafunzo ya kujenga vitalu nyumba na kilimo kwa kutumia vitalu nyumba. Tumepokea ushauri wa Waheshimiwa Wabunge na tutaendelea kufanya tafiti kuangalia namna ya kupata vifaa vyenye gharama nafuu ili ujuzi wanaoupata waweze kuenda kuuendeleza.

Mheshimiwa Spika, vilevile tutaendelea kutoa vifaa na mikopo kadri fedha zinapopatikana za kufanya hivyo ili ujuzi wanaoupata waweze kuutumia.

Mheshimiwa Spika, kuna hoja ambayo imetolewa kuhusiana na ufanisi wa mafunzo kwa vitendo. Kamati imependekeza kwamba tushirikiane na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia katika kuhakikisha kwamba mitaala inaboreshwa na inakuwa inawajengea ujuzi ili kupunguza gharama ya kuwa na program baada ya wahitimu.

Mheshimiwa Spika, nikuhakikishie Wizara yangu inafanya kazi kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu na hata program hizi ambazo tunaziendesha mitaala yake imeandaliwa kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu na tunatoa msisitizo wa mafunzo kwa vitendo kwenye program ya wanagenzi kwa mfano; asilimia 60 ya muda wa mafunzo unaelekeza kwenye mafunzo kwa vitendao na asilimia 40 inakuwa ndio nadharia.

Mheshimiwa Spika, pia tunashirikiana na waajiri katika kuhakikisha kwamba wanatoa fursa kwa vijana kwenda kufanya mafunzo kwa vitendo. Kupitia Bunge lako Tukufu naomba nitoe wito kwa waajiri nchini, kuwapa fursa vijana, yakufanya mafunzo kwa vitendo kwa sababu yale ni muhimu katika kuhakikisha kwamba ujuzi wanaoupata katika mafunzo yao unaendana na soko la ajira.

Mheshimiwa Spika, na wanapokuwa katika mafunzo kwa vitendo kuna kuwa na mwanya wa kurekebisha kama kuna mapungufu ambayo yanajitokeza katika mafunzo yao. Kwa hiyo, niwasihi sana, waajiri hapa nchini wenye viwanda, waendelee kutoa fursa kwa vijana wetu kwenda kufanya mafunzo kwa vitendo.

Mheshimiwa Spika, nikuhakikishie kwamba tutashirikiana kikamilifu na Wizara ya Elimu katika jukumu hili ambalo wamepewa sasa hivi na Serikali ya kuhakikisha wanapitia mitaala, kuhakikisha mitaala yote nchini kuanzia elimu ya awali mpaka vyuo vikuu inajikita katika kujenga ujuzi. Kwa hiyo, kwa sababu Wizara yetu pia imekuwa na program za kukuza ujuzi tutafanya kazi kwa pamoja ili kuhakikisha kwamba yale ambayo tumekuwa tunawafundisha vijana baada ya kuhitimu yaingie katika mitaala ili wanapomaliza shule au vyuo wawe na ujuzi stahiki.

Mheshimiwa Spika, hoja nyingine ambayo Waheshimiwa Wabunge wameizungumzia ni kuhusiana na Serikali ina mpango gani wa kuboresha kima cha chini cha mshahara katika sekta binafsi. Nikuhakikishie Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan inatuambua umuhimu wa maslahi kwa wafanyakazi na kwa kutambua hilo, tayari Serikali imeshaunda Bodi ya Kima cha Chini cha Mishahara kwenye sekta binafsi na Bodi hiyo nimeizindua jana tarehe 12 Aprili, 2022. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Bodi hiyo inapaswa kufanya utafiti ili iweze kuishauri Serikali kuhusiana na kima cha chini cha mshahara. Nitumie nafasi hii kuwasihii waajiri wote nchini pamoja na wafanyakazi kutoa ushirikiano unaotakiwa kwenye bodi hii ili iweze kufanya kazi yake ya utafiti na hatimae iweze kutoa mapendekezo kwa Serikali kuhusiana na kima cha chini cha mishahara katika sekta binafsi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ambalo limezungumziwa ni kuhusiana na Mabaraza ya Wafanyakazi kwamba Mabaraza haya kwanza katika kuna baadhi ya taasisi na waajiri wengine hawaundi Mabaraza ya Wafanyakazi na hata wengine ambao wameyaunda Mabaraza haya hayafanyi kazi kwa kuzingatia vikao ambavyo vimewekwa kwa mujibu wa sheria.

Mheshimiwa Spika, naomba niwakumbushe waajiri hapa nchini kwamba Mabaraza ya wafanyakazi yapo kwa mujibu wa sheria. Kwa hiyo niwasihi ninawataka waajiri wote nchini kuhakikisha kwamba Mabaraza ya Wafanyakazi yanaundwa na wanafanya vikao vyao kwa mujibu wa sheria. Mabaraza haya ni muhimu katika kuhakikisha kwamba kunakuwa na maelewano katika maeneo ya kazi na kutatua migogoro ambayo inaweza ikajitokeza.

Mheshimiwa Spika, kunapokuwa na utulivu mahali pa kazi kunapokuwa na mahusiano mazuri kuna kuwa na tija zaidi na ufanisi. Kwa hiyo, ninawasihi waajiri kuhakikisha kwamba Mabaraza yanaundwa na yanafanya kazi kwa mujibu wa sheria.

Mheshimiwa Spika, tumepokea pia maoni kuhusiana na Mifuko ya Hifadhi ya Jamii na hapa maoni yamejikita katika maeneo tofauti, kwanza kuna maoni kwamba baadhi ya Wastaafu wanapostaafu wanachelewa kulipwa mafao yao na wanapata usumbufu wa kutakiwa kupeleka barua na nyaraka mbalimbali au wakati mwingine wanaambiwa kwamba hawawezi kulipwa kwa sababu mwajiri hakupeleka michango yao kwa miezi kadhaa.

Mheshimiwa Spika, ni kweli jambo hili limekuwa usumbufu kwa wastaafu lakini nikuhakikishie kwamba Serikali inalifanyia kazi kikamilifu na katika hatua ya kuanzia tunaboresha mifumo ya TEHAMA, changamoto inayokuja ni kwamba watu walioajiriwa miaka ya nyuma kabla ya mifumo ya TEHAMA haijawa imara kumbukumbu zao zilikuwa zinatunzwa katika nakala ngumu, kwa hiyo wakati mwingine Watumishi hasa wale ameajiriwa kabla ya miaka 1999 ambao waliingizwa kwenye mifuko baada ya kuwa ameshaajiriwa baadhi yao kumekuwa na changamoto ya kupata taarifa zao.

Mheshimiwa Spika, jambo hili linafanyiwa kazi kikamilifu na tutahakikisha kwamba tunaondoa hiyo kero. Mimi mwenyewe nimejiwekea dhamira ya kufuatilia kwa ukaribu ili nipande kwa undani malalamiko hayo ya Wastaafu kwa sababu ni jambo ambalo halipendezi hata kidogo.

Mheshimiwa Spika, hao Wastaafu wameitumikia nchi yetu kwa moja mkunjufu, wamejituma kwa nafasi yao wamelijenga Taifa letu, kwa hiyo wanapomaliza utumishi wao ni lazima wapate stahiki zao kwa wakati na bila usumbufu wowote. Kwa hiyo, Serikali itaendelea kufuatilia kwa karibu suala hili na kuchukua hatua kuhakikisha usumbufu kwa wastaafu unaondolewa.

Mheshimiwa Spika, jambo jingine ambalo limezungumzwa ni kuhusiana na Mfuko wa Maendeleo ya Vijana. Kuna fedha ambazo Serikali imetoa kiasi cha Shilingi Bilioni Moja kwa ajili ya kuwawezesha vijana na mpaka kufikia Februari fedha hizo zilikuwa zimetumika kwa takribani Shilingi Milioni 245.

Mheshimiwa Spika, naomba uchelewaji wa kutoa fedha kwa mwaka huu wa fedha umetokana na kwamba kulikuwa na uboreshaji wa mwongozo wa utoaji wa mikopo ambao ulitokana na maoni ya Waheshimiwa Wabunge. Nikuhakikishie kwamba tunatambua kilio cha vijana, tunatambua kwamba vijana wengi kama nilivyosema wanapata ujuzi lakini hawana mitaji, vijana wengi wanaomaliza vyuo vikuu wengine wameanzisha startup zao lakini hawana mitaji. Kwa hiyo nikuhakikishie kwamba tutafanyia kazi suala hili kuhakikisha kwamba fedha zinapopatikana zinatoka ziende kuwanufaisha wanufaika.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo hayo mimi ninakushukuru sana kwa nafasi hii na ninaunga mkono hoja ya Mheshimiwa Waziri Mkuu.Ahsante sana. (Makofi)