Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Prof. Makame Mnyaa Mbarawa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkoani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, kwanza nami ninakushukuru kwa kunipa fursa hii kuchangia kwenye hotuba yetu hii iliyoko mbele yetu. Pili, napenda kusema kwanza ninaunga mkono hotuba hii kwa asilimia 100. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna hoja tatu ambazo zimewasilishwa kwa upande wa Wizara yetu. Hoja ya kwanza ni kuhusu ujenzi wa reli ya kisasa -Standard Gauge. Kama tunavyokumbuka reli ya kisasa Standard Gauge ilianza mwaka 2017 na ina urefu wa takribani kilomita 1,219 kutoka Dar es Salaam mpaka Mwanza. Reli hii imegawanyika katika vipande vitano. Kipande cha kwanza ni kutoka Dar es Saalam mpaka Morogoro chenye urefu wa kilomita 300, kati ya kilomita 300 kilometa 205 ni za njia kuu na kilometa 95 ni za kupishana. Kipande hiki kinajengwa kwa gharama ya takribani dola za Kimarekani bilioni 1.215 sawa na Shilingi Trilioni 2.7 za Kitanzania. Maendeleo ya ujenzi wa kipande hiki umefikia asilimi 95.72. Bei kwa kilomita moja ni takribani Dola Milioni 4.05 hii gharama inajumlisha na VAT.

Mheshimiwa Spika, wakati tunaweka mchakato wa ununuzi kwa ajili ya kipande hiki Wakandarasi wengi walichukua tender document lakini mwisho wa siku ni mkandarasi mmoja tu aliyerudisha hiyo tender document ambaye ni Yepi. Tulimpa kazi hiyo kwa kutumia kigezo chetu tulichojiwekea ambayo ni engineering estimation. Kwa vile kazi hiyo inaenda vizuri na tumefikia asilimia hiyo nategemea mwezi Mei tutaanza kufanya majaribio kwa ajili ya treni ya kwanza ya umeme itaanza kupita.

Mheshimiwa Spika, kipande cha pili ni kutoka Morogoro mpaka Makutupola chenye jumla ya kilomita 422. Kati ya kilomita hizo kilomita 336 ni za njia kuu na kilomita 86 ni njia za kupishana. Gharama ya mradi huo ni Dola Bilioni 1.923 sawa na shilingi trilioni 4.4 za Kitanzania. Ujenzi wake unaendelea na umefikia asilimia 82.68. Gharama kwa kila kilomita moja ni takribani dola za Kimarekani milioni 4.55 na gharama inaongezeka kwa sababu inategemea eneo gani tunapita.

Mheshimiwa Spika, kwa Dar es Salaam ilikuwa hali ni nzuri yaani tambarale lakini kila ukienda baadhi ya maeneo mengine kuna mito, kuna milima hiyo madaraja yanaongezeka, kuna maeneo lazima ujenge mahandaki ili kuhakikisha kwamba reli yako inakuwa salama vizuri.

Mheshimiwa Spika, lot nyingine ni lot ya tatu na rote ya nne. Lot hizi mbili tulizitangaza lakini hatukuweza kupata Mkandarasi. Kwa hiyo, tukawajibika kuja na utaratibu mwingine wa single source ambao unakubalika kisheria. Kigezo cha kwanza cha single source lazima yule Mkandarasi unaemchukua awe na uwezo na uzoefu mkubwa. Pili Mkandarasi huyo awepo kwenye eneo la site yenyewe, yaani anafanya kazi kama hiyo kwenye site hiyo. Kwa vile, katika kipande cha tatu, kipande cha Makutupora mpaka Tabora chenye urefu wa kilomita 368 tulitumia utaratibu huo na gharama ilikuwa Dola za Kimarekani Bilioni 1.908 sawa na Shilingi Trilioni 4.41.

Mheshimiwa Spika, jana tumeweka jiwe la msingi kwa ajili ya kipande hicho na sasa tumeshamlipa Mkandarasi takribani Shilingi Bilioni 609.36. Mkandarasi hapa ni Yepi na ndiyo anaanza sasa hivi kuweka vifaa, gharama kwa kilomita Moja ni takribani dola za Kimarekani Milioni 5.14. Hapa mnaona gharama inaanza kuongezeka kwa sababu tunapita kwenye milima, tunapita kwenye maeneo yenye tetemeko. Kwa vile reli yetu lazima ijengwe imara zaidi kuliko maeneo mengine ambayo hayana changamoto hizi za kijiografia.

Mheshimiwa Spika, kipande kingine ni kutoka Tabora – Isaka chenyewe kina urefu wa kilomita 168. Tumefanya utaratibu kama huu wa single source lakini mpaka sasa hatujakubaliana na Mkandarasi kwa sababu Mkandarasi ameleta bei ya juu ukilinganisha na bei tuliyojiwekea yaani engineering estimation. Bado mazungumzo yanaendelea na tunaamini Mkandarasi atashuka vizuri ili bei tutakayoipata hapa iendane na engineering estimation ambayo tuliiweka hapo zamani.

Mheshimiwa Spika, kipande cha tano ambacho kinaendelea ni kipande cha kutoka Isaka mpaka Mwanza chenye urefu wa kilomita 341. Kipande hiki kina urefu wa kilomita 249 njia kuu na kilomita 92 njia za kupishana. Kazi inaendelea na mobilization inaendelea na Mkandarasi amefika asilimia 4.46.

Mheshimiwa Spika, Mkandarasi hapa ni...

SPIKA: Kengele imeshagonga Mheshimiwa.

WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, maelezo mengi nitatoa wakati tutakapoleta bajeti yetu. Naomba tu kuunga mkono hoja kama nilivyosema kwa asilimia 100.

Mheshimiwa Spika, ahsanteni sana kwa kunisikiliza. (Makofi)