Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nimpongeze Mheshimiwa Waziri Mkuu pamoja na Mawaziri walio kwenye Ofisi yake kwa jinsi wanavyotekeleza majukumu yao. Nimpongeze yeye binafsi kwa kuwasilisha vyema hotuba ya bajeti na kwa usimamizi mzuri wa shughuli zote za Serikali.

Mheshimiwa Spika, mchango wangu utajikita kwenye hatma ya wavulana kielimu kutokana na uwepo wa shule chache zilizojengwa maalumu na mahsusi kwa ajili ya kuwawezesha wavulana.

Mheshimiwa Spika, hapa nchini Tanzania mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetoa fedha za kujenga shule moja maalumu ya sayansi kwa ajili ya wasichana katika kila mkoa. Ujenzi huu haujafanyika kwa wavulana.

Mheshimiwa Spika, pamoja na upendeleo nilioeleza hapo juu, hapa nchini kuna uwekezaji mkubwa sana kwenye shule bora za wasichana. Uwekezaji mkubwa umefanywa na taasisi za dini na watu binafsi. Kutokana na uwekezaji huu, shule hizi za wasichana zina ufaulu mzuri sana kwenye matokeo ya kidato cha nne na sita. Mfano wa shule bora binafsi zenye ufaulu mkubwa ni pamoja na St. Fransis Girls - Mbeya, Barbo Johansson Model Girls - Dar es Salaam, St. Christian Girls - Tanga, Loretto Girls - Mwanza, Samaritan Girls Secondary School - Shinyanga, Anwarite Girls Secondary- Kilimanjaro, Precious Blood - Arusha, Bethel Sabbs Girls Secondary School, St. Theresa of Avila Girls Secondary, Hekima Girls Secondary School - Kagera, Visitation Girls School - Kilimanjaro, Kandoto Science Girls Secondary - Kilimanjaro, Marian Girls - Pwani, Feza Girls - Dar es Salaam, Kibosho Girls Secondary - Kilimanjaro, Mazinde Girls - Tanga, Kifungilo Girls - Tanga, St Mary’s High School - Dar es Salaam, John the Baptist Girls Secondary School - Dar es Salaam, Kunduchi Girls Islamic High School - Dar es Salaam, Bethsaida Girl’s Secondary School - Dar es Salaam, St. Marie Eugenie Girls Secondary School - Kilimanjaro, Joyland Girls Secondary School - Kilimanjaro, St. Christina Girls Secondary School - Tanga na St. Clara Girls Secondary School - Kilimanjaro.

Mheshimiwa Spika, idadi ya shule binafsi za wasichana ni kubwa, na hapo juu nimetoa mifano michache.

Kwa upande wa wavulana, uwekezaji wa kimkakati ni mdogo sana. Shule zinazomilikiwa na kuendeshwa na taasisi na watu binafsi zenye majina makubwa ni chache. Ninazoweza kuzitaja ni zile za seminari, Marian Boys, Feza Boys, Tengeru Boys na nyingine chache ambazo sijazitaja.

Mheshimiwa Spika, kwa ujumla, idadi kubwa ya wasichana wanaosoma katika hizi shule binafsi nilizotaja hapo juu hufaulu vizuri na wengi wao hufanikiwa kujiunga na vyuo vya elimu ya juu hapa nchini. Kwa kifupi, mazingira ya kuwasaidia wasichana kujiendeleza zaidi ni mazuri kuliko ya wavulana.

Mheshimiwa Spika, tusipochukua hatua za kimakusudi kusaidia watoto wa kiume kwa kuwajengea shule maalumu, huko mbele ya safari uwepo wao katika vyuo vya elimu ya juu utakuwa na walakini. Dalili za awali zinaonesha kuwa idadi ya wavulana wanaojiunga na vyuo vya elimu ya juu inapungua na ya wasichana inaongezeka.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo ya hapo juu, ninaishauri Serikali yafuatayo; kwanza ijenge shule maalumu za sayansi za wavulana kila mkoa kama walivyofanya kwa wasichana na pili, iwasiliane na wadau wa maendeleo na kuwashawishi wajenge shule maalumu zenye hadhi kubwa kwa ajili ya wavulana.

Mheshimiwa Spika, kwa kufanya hivyo, wavulana watakuwa wametendewa haki kama ilivyofanyika kuwajengea watoto wa kike shule maalumu katika kila mkoa.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo yangu hapo juu, naunga mkono hoja.