Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, kwa namna ya pekee ninaomba kuungana na Watanzania wenzangu kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, kwa kutimiza mwaka mmoja wa kuongoza nchi yetu akiwa Rais wa Awamu ya Sita wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Tumeshuhudia mafanikio makubwa katika kuimarisha miundombinu hususan barabara, reli, viwanja vya ndege, bandari, huduma za kiuchumi na kijamii kama vile ujenzi wa madarasa, hospitali, zahanati na vituo vya afya, huduma za maji, utawala bora pamoja na kuhamasisha uwekezaji na utalii. Pia naomba nimpongeze Mheshimiwa Dkt. Philip Isidor Mpango, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi nzuri iliyotukuka ya kumsaidia Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Spika, napenda kumshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mawaziri na Naibu Mawaziri katika Ofisi ya Waziri Mkuu kwa uongozi wao na utendaji uliotukuka. Tathmini zinathibitisha mafanikio mazuri ya utekelezaji na usimamizi wa Mpango wa Kwanza na wa Pili kupelekea Taifa letu la Tanzania kufanya vizuri mno kuinua uchumi katika kipindi hiki kigumu. Kutokana na taarifa za Benki ya Dunia, ni Tanzania pekee ambayo uchumi wake umekua kwa asilimia 4.9, wakati nchi karibu zote za Afrika Mashariki zimekua na ukuaji hasi (negative GDP growth).

Mheshimiwa Spika, napenda pia kutumia fursa hii kukupongeza wewe binafsi na Naibu Spika kwa kuchaguliwa kwa kura zote asilimia 100. Pia napenda kupongeza uongozi wote wa Bunge kwa uongozi mahiri na wenye ubunifu wa hali ya juu katika kuongoza Mhimili wa Bunge.

Mheshimiwa Spika, napenda kumpongeza Waziri Mkuu kwa hotuba nzuri iliyojaa ubunifu mkubwa na imedhihirisha utayari wa Taifa letu katika ya ushindani wa kimataifa (National Competitiveness). Bajeti hii inaenda sambamba na dhima ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2021/2022 – 2025/2026 ambayo ni Kujenga Uchumi Shindani na Viwanda kwa Maendeleo ya Watu.

Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha Julai, 2021 mpaka Februari, 2022 Serikali imeendelea kutekeleza miradi ya kimkakati kwa mafanikio mkubwa sana na utekelezaji huu unaonekana mpaka kwenye ngazi ya Halmashauri zetu. Mafanikio makubwa yamejikita kwenye uboreshaji wa miundombinu ya barabara, reli, bandari, mtandao wa mawasiliano na uboreshaji wa usafiri wa anga. Napongeza Serikali kwa hatua nzuri za utekelezaji wa mradi wa kihistoria wa ujenzi wa reli ya kisasa ya SGR na ujenzi wa Mradi wa Kufua Umeme wa Maji wa Julius Nyerere (megawati 2,115). Miradi hii miwili ya SGR na umeme, ni nguzo imara ya kiushindani katika uchumi wetu na nchi za Maziwa Makuu na hata za Kusini mwa Afrika na Kati.

Mheshimiwa Spika, pamoja na mafanikio hayo, uchumi wa dunia umekumbwa kwa kiasi kikubwa na athari za UVIKO-19 na hivi sasa kuathirika zaidi na vita ya Urusi na Ukraine. Kwa mujibu wa Taarifa ya Shirika la Fedha la Kimataifa ya Januari, 2022 kasi ya ukuaji wa uchumi wa dunia inatarajiwa kupungua hadi kufikia asilimia 4.4 mwaka 2022 ikilinganishwa na asilimia 5.9 mwaka 2021. Hali hiyo inatarajiwa kusababisha kuvurugika zaidi kwa mnyororo wa uzalishaji na usambazaji wa bidhaa na huduma na athari hizo zinaikumba hata Tanzania. Hivi karibuni kumekuwepo na taarifa za uhaba na upandaji wa bei kwenye bidhaa za petroli, ujenzi, vyakula, nishati na hata pembejeo za kilimo.

Mheshimiwa Spika, kutokana na athari za UVIKO-19 na vita ya Urusi na Ukraine, Serikali inatakiwa kuchukua hatua za kibajeti kukabiliana hasa na mfumuko wa bei na kuporomoka kwa thamani ya shilingi dhidi ya dola ya Marekani na sarafu kuu zingine. Kwa kuzingatia kuyumba kwa uchumi wa dunia, dajeti hii ijielekeze kuchukua hatua za kuimarisha pato la Taifa kupitia sekta za kilimo, madini, utalii na uchukuzi. Hatua hizi ziende sambamba na kuimarisha mazingiara ya uwekezaji hasa kwenye sekta ya kilimo na madini. Kutokana na mfumuko wa bei kwenye bidhaa za petroli na mtikisiko wa thamani ya shilingi, kutapelekea mahitaji zaidi ya fedha za kigeni na hivyo msukumo uwepo kwenye kuongeza uzalishaji wa madini na mazao ya kilimo. Hatua hizi ni muhimu kuimarisha uhimilivu wa deni la Taifa hasa kwenye kigezo za ulipaji wa deni la nje kwa kulingamisha na uuzaji wa bidhaa nje (mapato ya fedha za kigeni).

Mheshimiwa Spika, pamoja na msukumo kwenye kilimo, madini na utalii, Serikali inatakiwa kuwekeza hasa kwenye miundombinu ya usafirishaji ikiwemo barabara, reli, bandari na usafiri wa anga hasa kwa mizigo. Katika Halmashauri zetu tumekuwa tunakabiliwa na changamoto hasa kwenye miundombinu ya barabara. Katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, barabara zinazohudumiwa na TARURA kwa asilimia zaidi ya 80 zipo kwenye hali mbaya sana kutoka na mafuriko. Maeneo mengi ya vijijini barabara hazipitiki kutokana na madaraja kusombwa na mafuriko. Naomba Serikali ichukue hatua za haraka kunusuru hali hii ili wananchi waweze angalau kusafirisha mazao yao.

Mheshimiwa Spika, naomba Serikali iweke msukumo zaidi kwenye kuboresha miundombinu ya barabara kurahisisha usafirishaji wa mazao ya kilimo. Kutokana na fursa za uzalishaji mkubwa kwa mikoa ya Nyanda za Juu Kusini, napendekeza muendelezo wa uboreshaji wa barabara za TANZAM kipande cha Igawa - Tunduma; barabara ya bypass ya Uyole - Songwe; barabara ya Mbalizi – Shigamba – Isongole kutokana na uzalishaji wa mazao ya kilimo; barabara ya Mbalizi – Galula – Makongorosi kutokana na uzalishaji mkubwa wa mazao ya kilimo na madini; na pia barabara ya Isyonje – Kikondo – Makete ambayo ni muhimu sana katika kusafirisha mazao ya kilimo ikiwemo maua, parachichi na viazi kwa soko la nje. Uboreshaji wa barabara hizi pamoja na uwanja wa ndege wa Songwe ni muhimu sana kwa usafirishaji wa mazao yetu kwa soko la ndani na nje, na kwa kiasi kikubwa utaongeza mapato ya fedha za kigeni.

Mheshimiwa Spika, pamoja na changamoto za vita ya Urusi na Ukraine, bado kuna fursa kubwa kwa Tanzania hasa kwenye uzalishaji wa ziada wa mazao mbalimbali na hasa nafaka kuziba pengo la nafaka kutoka Urusi na Ukraine kwenda nchi kadhaa za Afrika na mabara mengine. Serikali iimarishe upatikanaji wa pembejeo bora kwa bei nafuu na kuimarisha upatikanaji wa masoko ya uhakika. Kutokana na jitihada walizofanya Wizara ya Kilimo kuwapatia vitendea kazi Maafisa Ugani, ichochee kuongeza tija na uzalishaji wa mazao ya kilimo kutoka uzalishaji wa sasa ambao upo chini sana ikiwemo uzalishaji wa kilo 1,000 za mahindi kwa eka mpaka kilo 4,000 kwa eka ya mahindi.

Mheshimiwa Spika, kwa lengo la kuvutia wawekezaji na kuongeza pato la fedha za kigeni, napendekeza Serikali kuchukua hatua kuharakisha uwekezaji kwenye mradi wa madini ya Niobium ikiwa ni pamoja na ujenzi wa kiwanda cha Ferroniobium (FeNb) ambacho kitakuwa cha kwanza Afrika na cha nne duniani. Kutokana na mahitaji makubwa ya ujenzi wa reli, madaraja yakiwemo reli ya SGR, kuna mahitaji makubwa ya vifaa vya chuma ambavyo ni imara, lakini vyepesi na vyenye ubora wa kimataifa. Kwa kutumia sheria zetu za uwekezaji, Serikali itumie fursa za kipindi hiki ili kuvutia wawekezaji kwenye madini ya viwandani ili yaongezwe thamani hapa kwetu na pia kuvutia malighafi ya madini toka nchi zingine ili yachakatwe hapo kwetu. Tanzania imebahatika kuwepo kwa madini ya Niobium ambayo inapatikana milima ya Panda Hill Wilaya ya Mbeya, na mahitaji ya Ferroniobium (FeNb end product) ni makubwa duniani na hapa kwetu pia. Kwa kutumia rasilimali zetu za madini, Serikali inaweza kutengeneza fursa nyingi na kupitia Mradi wa Niobium na Kiwanda cha Ferroniobium, ajira 2,000 zitakazozalishwa wakati wa ujenzi na pia kutakuwepo ajira za kudumu zaidi ya 600 na indirect jobs 7,000.

Mheshimiwa Spika, mradi utazalisha mapato kila mwaka shilingi bilioni 500 (dola za Kimarekani milioni 220) ambapo mapato kwa Serikali kila mwaka shilingi bilioni 50 (dola za Kimarekani milioni 22) uhai wa mgodi ni zaidi ya miaka 30. Hiki kitakuwa kiwanda cha kisasa cha kwanza Afrika (Modern Manufacturing Plant and Smelter). Pamoja na kuingiza teknolojia hii adimu na ujuzi (skills transfer) pia itakuwa itachangia huduma za kijamii (Corporate Social Investment in Community) na chanzo cha fedha ya kigeni.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.