Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa hii. Utakumbuka tarehe 7/11/2022 niliwasilisha katika Bunge lako tukufu Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti pamoja na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa ya mwaka 2023/2024.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutumia fursa hii kukushukuru wewe mwenyewe pamoja, Naibu Spika, Wenyeviti wote wa Bunge, Kamati ya Bunge, pamoja na Waheshimiwa Wabunge wote kwa maoni ambayo wameyatoa. Nasi kama Wizara tumeyapokea. Kama ilivyo kwenye kanuni, lengo la wasilisho hili ni ili tuweze kupokea maoni na kuendelea kuboresha document hii ambayo tutaiwasilisha tena na hatua nyingine ziweze kufuata mpaka ambapo tutakuja kwenye bajeti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeyapokea maoni haya na Waheshimiwa Wabunge zaidi ya 90 wamechangia katika mjadala huu. Nawashukuru Waheshimiwa Mawaziri ambao wamekwisha kupokea mapendekezo ambayo yanaangukia katika sekta zao na kufafanua katika baadhi ya maeneo ambayo yalihitaji ufafanuzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kwamba kanuni za Bunge hili ni kupokea maoni na kama ambavyo wenzangu wametangulia kufafanua katika baadhi ya maeneo, naomba nami nifafanue katika baadhi ya maeneo ambayo yanahitaji ufafanuzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza kubwa ambalo nahitaji kulifafanua ni ile hoja ambayo ilitolewa kuwa Tanzania imeshuka toka uchumi wa kati wa chini na kwenda kwenye kundi la zile nchi masikini. Napenda nitoe ufafanuzi huu kwa sababu hoja hii imekuwa ikipotoshwa mara kwa mara. Kwanza tuna mambo mawili ambayo yanafanana ambayo tunapojadiliana lazima tuwe makini tunapoyaongelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja, kuna nchi inapokuwa imepangwa kwenye kundi fulani la kukua kwa uchumi na kipato cha watu wake; pili, kuna ule uwiano wenyewe wa kukua kwa uchumi katika nchi. Yaani hapa tunaongelea ile growth rate na kundi ambako nchi yetu imepangwa. Namaanisha nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulipopata COVID katika nchi nyingi takwimu ndogo ndogo ambazo tunazipima kwa majira mafupi mafupi, wengine wanapima kwa muda mfupi zaidi, sisi tunapima kwa robo mwaka. Takwimu ya growth rate ndiyo takwimu ambayo imekuwa na namba tofauti tofauti tunazozitoa kwa kila wakati. Yaani kabla ya COVID tulikuwa around 7%, baada ya hapo tukashuka mpaka 8%. Tulipoenda kwenye utekelezaji wa mpango wa kuondokana na UVIKO tumepanda tukaenda 9%; tuliweka projection za kurudi tena zaidi ya 5% kabla ya vita vya Ukraine, baada ya athari za vita vya Ukraine, tukarudi kwenye projection ya 4.7%. Baada ya kuweka mpango mkakati na bajeti hii tuliyoiweka, matarajio yetu tunaenda kupanda tena kuzidi 5%. Hiyo ni growth rate.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu nchi iko kundi gani la kipato, ambayo ndiyo hoja aliyoisema juzi Mheshimiwa Profesa Muhongo, kuna namna mbili za kupima na kupanga nchi katika makundi kulingana na pato la Taifa. Yaani the key measures for income per capita. Ya kwanza ni GDP per capita na ya pili ni GNI per capita ambayo zinaongelea pato la Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Benki ya Dunia (World Bank) haitumii GDP per capita kupima kundi nchi ilipo, inatumia GNI. Katika taarifa zake zote ambazo imekuwa ikitumia Benki ya Dunia huwa inatoa takwimu hizo za GNI per capita kwa nchi kila Julai mosi, kila mwezi wa Saba wa mwaka na takwimu zinazokuwa zimetolewa ni zile za mwaka uliopita. Kwa maana Julai Mosi, 2022 ilitoa makundi ya nchi kwa mwaka 2021, tarehe Julai Mosi, 2021 ilitoa makundi ya mwaka 2020 na tarehe Julai Mosi, 2020 ilitoa makundi ya nchi kwenye vipato vyao kwa mwaka 2019.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo hiki alichokisema Profesa Muhongo kwamba tumeshuka mwaka 2022, tathmini hiyo hata haijafanyika, takwimu hiyo itatolewa Julai Mosi, 2023. Kwa maana hiyo zile takwimu alizozitoa sizo na zile ambazo zilishatolewa mpaka sasa ambazo zinaongelea kwa mwaka uliopita, zilizotolewa kwa mwaka huu zinaonesha Tanzania bado tuko kwenye dola 1,140 ambayo tumeshapiga hatua kubwa sana tangu pale tulipokuwa tumepanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine ambacho niliona nikiseme, ni kwamba ile nukuu aliyosema imetoka Benki ya Dunia, mimi kwa kuwa Waziri wa Fedha nakuwa Gavana wa Benki ya Dunia. Kwenye internal memo ya Benki ya Dunia waliandika kusikitishwa nanukuu ile ambayo ilinukuliwa ikionesha imetoka Benki ya Dunia kama ninavyoweza kusoma hapa. Alisema:

“Honorable Minister we have learned with a shock that it was said Tanzanians GDP per Capita is now 990, trying to make the public of Tanzania to believe that Tanzania has slipped to lower income countries. That was refered that Tanzania is now GDP per Capita range to 990 USD.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakaitaja ile website ambayo ni trading economies.com wameiweka hapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, anasema; “It appears to be incorrect as the figures does not confirm. In any case GDP per Capita is not what we use in income classification. Besides the number they have given does not appear to be consistence. This is not from the World Bank. Please note that, some countries have slipped from middle income to lower income but Tanzania has maintained its status since becoming lower middle-income country in 2020. Please note World Bank does not GDP per Capita for income classification and this articles which was refereed is incorrect and is not from the World Bank. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo basi kwa mujibu wa taarifa hizo Benki ya Dunia haijatoa hizo takwimu na Benki ya Dunia wakati tuko kwenye vikao vilivyoisha tu vya juzi mwezi huu uliopita. Benki ya Dunia wakati wanahutubia Mawaziri wa Caucus ya huko Afrika, waliwatuma Mawaziri wengine waulize Tanzania imefanyaje kuweza ku-maintain status na kuendelea kukua zaidi na kauli hiyo ilitolewa na Rais wa Benki ya Dunia na ikatolewa na Makamu wa Rais wa Benki ya Dunia. Ni siku hizo hizo tu wasingeweza kuipongeza Tanzania na wakasema tumfikishie salamu hizo Mheshimiwa Rais na wakati ule ule pato la Tanzania liwe limeshuka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kama kuna watu ambao wanasubiri sana Tanzania ishuke kutoka uchumi wa kati kwenda wa chini, niwahakikishie wanapoteza muda wao, Tanzania haitashuka kwenda kwenye kipato cha chini, inasonga mbele. Itatoka kwenye uchumi wa kipato cha chini kwenda kipato cha kati cha juu. Hii si kwa maneno ni kwa hatua ambazo Mheshimiwa Rais na Serikali anayoongoza inachukua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namba zinaongea, huwezi kwenye nchi ambayo unajenga bwawa kubwa la umeme kwa ajili ya grid stabilization utegemee ukishamaliza mradi huo eti ushuke kutoka pale ulipokuwa uende chini. Huwezi kwenye nchi ambayo unaboresha bandari kwa ajili ya kufungua shughuli kubwa kubwa kwenye lango la nchi ambazo hazina huduma ya maji, ukishamaliza miradi hiyo eti uchumi wako ushuke. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huwezi kwenye nchi ambayo imeweka bajeti kubwa kwenye historia inayokwenda kwenye shughuli za uzalishaji, bajeti ya kilimo inaenda kwenye umwagiliaji, haya si maneno ni scheme ambazo zitaonekana na watu watazalisha na ambao ndio wengi katika Taifa hili. Huwezi ukamaliza kujenga irrigation schemes ukaondoka kwenye kutegemea mvua ukaenda kulima kwenye uhakika kwa kutumia mbegu bora, halafu ukishamaliza hapo GNI yako na kipato na position ya nchi yako iweze kushuka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika nchi hiyo hiyo, huwezi ukaendelea kuboresha viwanda, mashamba kama ya Mkulazi, Mbigili, Bagamoyo Sugar ambayo na sukari za kwanza zimeshaanza kutokea ni miradi mikubwa mikubwa, ujenzi wa reli ya kisasa ambayo itafungua uchumi na ni uti wa mgongo wa uchumi, halafu ukishamaliza kuijenga tu nchi ishuke pale ilipokuwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huwezi ukatekeleza mradi mkubwa kama wa LNG injection yake ni ya billions, trillions, halafu ukishamaliza kuutekeleza na uka-take off ajira zitakazotengenezwa pia na production zitakazofanyika halafu baada ya hapo nchi hiyo ishuke kwenye nafasi ilipokuwa iende upande wa chini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uwekezaji unaofanyika kwenye elimu, miundombinu ya barabara kutoka kwenye uzalishaji, nyie Waheshimiwa Wabunge ni mashahidi kwa Wabunge ambao wameshakaa zaidi ya kipindi kimoja watasema. Fedha zilizokwenda kwenye TARURA kufungua barabara kutoka kwenye uzalishaji kwenda kwenye feeder roads ni nyingi kuliko katika kipindi chochote kile cha historia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, uwekezaji katika sekta nyingine, kwa mfano, imenunuliwa mitambo kwa ajili ya kuchimba mabwawa. Mabwawa yale yatanusuru mifugo iliyokuwa inakufa. Watu mifugo yao ikanusuriwa wakaanza kufuga kisasa, hawawezi wakarudi nyuma, wale watu watasonga mbele. Hivyo hivyo mitambo ile itaenda kutengeneza schemes ndogo ndogo ambazo zitaenda kuongeza uzalishaji katika maeneo husika. mazingira bora ya uwekezaji na kuvutia mitaji kazi kubwa ambayo Mheshimiwa Rais ameifanya na wawekezaji wanatiririka, yatatengeneza ajira, tutapunguza unemployment, hao watu wote wataenda kuwa na vipato vyao. Watu wengi wa aina hiyo wakishakuwa na vipato vyao nchi haiwezi ikashuka ilipokuwa kwenye daraja lile kwenda chini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliona nilisemee lile na niwaombe Watanzania kama ambavyo Chief Whip amesema hapa. Ni vyema tukaipenda nchi yetu na wala tusichanganye, mambo mengine ni ya kitaalam. Kwa mfano, kuna watu wana…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Waziri dakika tatu, malizia kengele ya pili imeshagonga.

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna wakati watu wanachanganya cost of living na standard of living na kipato nchi ilipo. Haya mambo ukilinganisha nchi na nchi utaweka phenomenon nyingi za kiuchumi, ni lazima ukitaka kulinganisha sawasawa uweke na purchasing power kwa sababu zile exchange rate za nchi na nchi zinatofautiana. Mtu anaweza akawa analipwa vizuri sana, ana kipato kizuri sana, kama eneo alipo na yule mwingine aliko bei za bidhaa zinaenda tofauti yule pamoja na kuwa kipato kikubwa yeye atakuwa na maisha magumu kuliko yule mwingine ambaye huenda ana kipato kidogo, lakini bei zake ziko tofauti. Kwa hiyo haya mambo lazima mara zote tuwe tunafahamu undani wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine walisema ukomo wa deni la Taifa. Wanasema Bunge labda liwe linaweka ukomo wa kukopa. Hata sasa Bunge limeweka ukomo wa kukopa, kwa sababu nchi yetu kila mkopo tunakopa kwa mradi na kila mradi tunapitisha kwa bajeti. Hakuna sehemu ambako tunakopa bila mradi na hakuna sehemu tunakopa bila bajeti. Tumeweka kwenye kila mwaka ukomo wa kukopa ndani, kukopa nje, misaada, makusanyo, hivyo ndivyo bajeti inavyokuwa. Kwa maana hiyo hakuna siku ambako inaenda inakopwa holela tu kwamba ni open cheque, haijawahi kutokea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mikopo yote inakopwa kwa mradi, na busara inayotumika ni kupeleka kwenye miradi ambayo italeta tija kubwa, itafungua uchumi. Fedha zote hizo zinazokopwa zinakwenda kwenye uwekezaji. Wengine wakiona mkopo umetajwa labda dola bilioni mbili labda trilioni nne inakuwa program labda na multilateral ambayo inachukua si mwaka mmoja na fedha hizo huwa zinakwenda kwenye mradi mahususi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa wengine wanaangalia mradi ni endelevu, wanadhani kama mradi ni endelevu deni litabaki lilelile. Hebu niambieni kama fedha ya kwanza iliyoingia ilikuwa ya lot one hivi tunaweza; lot one imeishia Morogoro, hivi tunaweza tukafika mpaka Mwanza sasa deni likabaki lilelile la lot iliyokuwa imeishia Morogoro? Haiwezekani! You can’t eat the cake and have it.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisema unataka ukusanye kamoja kamoja ndio upeleke kwenye lot ukaimalizie utachukua miaka 100 mpaka 120, ni mkandarasi gani atakayekusubiria tu ukusanye kila mwezi umpelekee? Tunachukua cha jumla tunatekeleza mradi uishe haraka ili tuweze kurejesha pale tulipochukua na hizo ndizo tathmini za kitaalam zinazofanywa kuweza kupima kwamba huyu anaweza akakopesheka. Nchi zozote ambazo zinakua ndizo ambazo madeni yao yanakua. Chukueni tathmini si vizuri kutaja sana nchi, chukueni nchi zile mnazozifahamu ambazo hazina uchumi kabisa muangalie kama zina deni. Maskini yeyote hadaiwi, anadaiwa atalipa kitu gani? Ukiona nchi inayodaiwa sana ni nchi inayokua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa hivi mwekezaji yeyote, mtoa fedha yeyote anaiangalia Tanzania kwa sababu wale wengine hawana cha kuwalipa, ndio maana unaweza ukaona hata miradi inagombaniwa. Hiyo tunatakiwa tuone kwamba tuna fursa kubwa na hizi fursa zitafungua uchumi, zitafungua ajira ili tuweze kuhakikisha kwamba tunajenga nchi yetu na Watanzania wanapata ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiwa tunawaza kila wakati, kuangalia na hilo ndio tatizo kubwa sana…

MWENYEKITI: Malizia Mheshimiwa Waziri.

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa leo tulikuwa tunapokea tu maoni, niwahakikishie yote tumeyapokea, Dira ya Taifa mpya, kazi inaendelea kuiandaa na inaandaliwa ikiwa na mwendelezo wa hii itakayokuwa imeisha. Miradi ya EPC+F imefanyiwa tathmini na tunaelekeza nguvu kubwa kwenye PPP kama nilivyosema kuweza kuhakikisha kwamba maeneo ambayo Private Sector inaweza ikashiriki kikamilifu Private Sector ipewe fursa ishiriki kikamilifu ili iweze kutengeneza ajira kwa vijana wetu na kuweza kuongeza kipato kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuyasema hayo, naomba sasa kutoa hoja na nirejee kauli ya mwanzo ambayo niliwasilisha kwamba nimewasilisha maandalizi ya Mpango wa Bajeti kwa Mwaka 2023/2024 na Mwongozo wa Maandalizi ya Bajeti pamoja na Mpango wa Maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imepokea Maoni na Ushauri wa Bunge kwa mujibu wa Kanuni ya 113(5)(c).

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha. (Makofi)