Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Nape Moses Nnauye

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mtama

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru Sana kwa kunipa nafasi na mimi nichangie kidogo. Kwanza nimpongeze Waziri wa Fedha kwa mpango mzuri aliouleta, lakini pia nimpongeze Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan na Serikali ya Awamu ya Sita kwa kujipambanua kusukuma maendeleo ya watu. Nishukuru sana kwenye mpango huu kuna mawazo mazuri na uamuzi wa busara wa Serikali kutumia TEHAMA katika kuboresha huduma mbalimbali zinazotolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kwa ujumla wake hatufurahishi sana na mahusiano yaliopo kati ya watoa huduma za mawasiliano na watumiaji wa huduma za mawasiliano, hakuna mahusiano mazuri. Kumekuwa na mashaka makubwa na kutuhumiana kukubwa sana. Sasa Serikali inachukua hatua zifua tazo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja; tunadhani kuna mapungufu kwenye kanuni zinazosimamia huduma zinazowasimamia watoa huduma na watumiaji wa huduma katika kuzipata hizi huduma, na hasa kwenye maeneo ya wajibu wa watoa huduma na wajibu wa watumia huduma. Serikali tumefanya uamuzi wa kuzipitia upya kanuni hizi ili tuone mashimo yako wapi ili mahusiano haya yarekebishwe, huduma za mawasiliano nchini ziboreshwe. Hapa niwathibitishie Waheshimiwa Wabunge mawazo yenu tumeyachukua na mawazo ya wananchi katika hili tumechukua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, wananchi wanasema tunapobadilisha bei ya bando kwa nini tunapeleka matangazo kwenye vyombo vya habari badala ya kumpelekea mtumiaji moja kwa moja? Tunadhani hii ni hoja ya msingi kwamba siku moja kabla ya mabadiliko mwananchi apelekewe taarifa moja kwa moja kwenye simu yake afanye uamuzi anaendelea na matumizi ya bando hilo au anabadilisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili tunalolifanyia kazi, tunao utaratibu, kila baada ya miaka mitano, kunafanyika tathmini ya gharama halisi za usafirishaji wa data katika huduma ya mawasiliano. Gharama ya mwisho ilifanyika mwaka 2018, tathmini ikatupa range ya shilingi mbili mpaka shilingi tisa. Sasa ni miaka mitano tunafanya tathmini hiyo, mwezi wa 12 mwaka huu, tathmini hiyo itakamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwelekeo unavyoenda, kwa sababu kuna uwekezaji mkubwa umefanyika, kuna hatua zinachukuliwa za kikodi, lakini pia kuna taratibu zinaendelea, kwa hiyo, mwelekeo unavyotupeleka, tunadhani matokeo ya tathmini yatashusha gharama za usafirishaji wa data nchini. Kwa hiyo, hayo mambo mawili ya msingi tunayafanyia kazi.

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Nape, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Getere.

T A A R I F A

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Mheshimiwa Waziri anafanya kazi nzuri, lakini wakati anaendelea, nataka kujua jambo moja; huwa inanisikitisha sana na nimelisema muda mrefu pole pole naona haliendi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nina shilingi 3,000,000 kwenye benki, mimi ni mchungaji, niko porini kule nachunga; salio limeniishia kwenye simu, nataka kutoa fedha kwenye benki kwa kutumia sim banking, wananiambia niweke salio nami sina uwezo wa ku-access hili salio, sina, nimeishiwa; kwa nini benki au hii mitandao wasifanye mawasiliano na mimi ili hela yangu inapokuwa nimeichukua bure, ikatwe kwenye benki? Yaani mimi nina hela kwenye simu, halafu inafia porini! Siwezi kutoa hela kwa sababu sina tu vocha ndani? (Makofi)

MWENYEKITI: Sasa Waheshimiwa Wabunge, hiyo ni taarifa au unachangia na wewe una hoja yako mpya kabisa umeileta ambayo haikuwa umeizungumza? Mheshimiwa Waziri naomba utiririke na yale maelezo yako, hii taarifa iweke kando kwanza, kwa sababu inaleta jambo jipya. Ni la msingi, lakini ni jambo jipya. (Kicheko/Makofi)

WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Hoja ya pili ambayo nilitaka kuichangia hapa, kumekuwa na mjadala kwamba kulikuwa na mtoa huduma ambaye aliamua kubadilisha bei ya bundle lake kabla hajabadilisha taarifa kwenye bango lake. Asubuhi nilitoa taarifa hapa kwamba Serikali tumechukua hatua, tumemwita TCRA, bahati nzuri, huyu mtoa huduma amekiri uzembe katika kutekeleza wajibu wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali tumechukua hatua zifuatazo: Moja, tathmini iliyofanyika imeonesha walioathirika na jambo hili ni watu 22,107 walitumia huduma wakati zile taarifa hazijabadilishwa. Baada ya kuling’amua hili, Serikali imemwagiza mtoa huduma: kwanza, awarudishie hawa walioathirika MB zao 200 ambazo walitakiwa wazipate kutokana na bango lake lilivyokuwa; pili, awape MB 300 kila mwathirika kama fidia ya usumbufu alioupata kwa sababu ya uzembe uliofanywa na mtoa huduma; na tatu, tumemtaka mtoa huduma awaombe radhi watumiaji wa huduma hiyo walioathirika kwa kuwatumia ujumbe kwenye simu zao kueleza uzembe alioufanya. Hii itakuwa ni hatua za mwanzo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge, Serikali tunatamani tuone kuna mahusiano mazuri kati ya watoa huduma na wapokeaji wa huduma. Sasa mahusiano haya, moja ya eneo kubwa ambalo ni muhimu tukalipitia na hli ndilo ambalo tumeanza nalo kazi, ni kutengeneza hizi kanuni. Zilizopo tuzipitie, lakini kama iko haja, tutengeneze kanuni nyingine mpya, zi-regulate mahusiano haya ili mtoa huduma ajue wajibu wake na mpokea huduma ajue wajibu wake. Tunaamini hili likifanyika, mawasiliano nchini yataboreka na matumizi ya TEHAMA yatakuwa bora na uchumi wetu utaimarika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi. (Makofi)