Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi jioni hii, kuchangia Mpango wa mwaka 2023/2024.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa kutengeneza mpango ambao unaendana na Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya Mwaka 2020 - 2025. Pamoja na kufuata ilani, lakini kwa mpango wetu huu nimenifurahishwa mno kitendo cha kuwepo miradi ya Liganga na Mchuchuma pamoja na reli ya Mtwara, Mbamba Bay.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumza suala la Bandari ya Mtwara, tumefanya uwekezaji mzuri, lakini bado hatuna mipango, namna ya kuitumia Bandari ya Mtwara. Njia pekee ya kuitumia hii ni kutekeleza miradi miwili ya Liganga na Mchuchuma sambamba na reli ya kutoka Mbamba Bay kwenda Mtwara pamoja na njiapanda zake za Mchuchuma na Liganga. Tukitekeleza miradi hii, Bandari ya Mtwara itatumika ipasavyo na itaweza kuleta uchumi na kukuza uchumi wa nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kutekeleza miradi hii, kwa sasa hivi kule Ngaka kuna makaa ya mawe ambayo yanaenda Mtwara karibu kila siku zaidi ya magari 300 mpaka 400 na mengine yanapita hapa hapa Dodoma kwenda Nairobi, Burundi na Arusha. Ni kwa sababu y barabara ile imekuwa nzuri, na ni ya lami. Kama tungeweza kujenga Reli ya Mtwara -Mbamba Bay - Liganga na Mchuchuma nadhani ingekuwa rahisi zaidi na mzigo mwingi ungeweza kutumia Bandari ya Mtwara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Wizara watakapokuja na mpango kazi huu ambao wameuzungumza, isiwe wimbo wa kila siku kwamba kila mwaka tunasema tutajenga, tutatekeleza Mradi wa Liganga na Mchuchuma, tutatekeleza kwa PPP, suala la ujenzi wa reli ya Kusini, hili jambo litakuwa halina maana. Hili jambo huwezi kulitenganisha; utatekeleza Mradi wa Liganga na Mchuchuma, hakuna namna ya kusafirisha chuma. Njia sahihi na rahisi ni ya kutumia reli peke yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ikiwa tutaanza mapema, tunatakiwa lazima tujenge barabara inayounganisha Mkiu kwenda Madaba ambayo magari yataendaa moja kwa moja mpaka kufika Mtwara. Njia hizi bila kufanya, kwa kweli hali ya miradi hii, hata wawekezaji wanapokuja, moja ya changamoto ya Liganga na Mchuchuma kwa wawekezaji wa ndani ni hali ya mahali ilipo na usafiri wa kwenda mahali pale. Shahidi atakuwa ni Mbunge wa Ludewa; barabara yao, sisi tumefika pale, siyo nzuri na siyo rafiki kwa kuweza kuendesha ule mradi. Nadhani wakati umefika, pamoja na kutekeleza huu mradi, basi tutengeneze huu mradi pacha ambao ni wa kutengeneza reli ya Kusini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuzungumza hayo, nitazungumzia mpango na Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya Mwaka 2020 ambayo ilieleza kwamba, tutatengeneza barabara kwa kiwango cha lami kutoka Mtwaro - Pachani Nalasi kwenda Tunduru Mjini. Eneo hili kwa kweli lina vijiji 77. Vijiji 30 kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru, vijiji 47 kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Namtumbo. Ni maeneo ambayo ni mazuri, yana uchumi mkubwa wa korosho, ufuta, mbaazi pamoja na mahindi. Kwa hiyo tunaomba kwenye mpango ujao, na sasa hivi ni mwaka wa tatu huu, hakuna dalili yoyote ya kuonesha sehemu hii itatengenezwa kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru Serikali kwamba kila mwaka inatoa siyo chini ya Shilingi bilioni mbili kwa ajili ya kutengeneza barabara ile kwa kiwango cha changarawe, lakini kwa sababu ya mvua nyingi zinazonyesha katika maeneo yale, kila mwaka barabara ile inakuwa inatengenezwa na haina mafanikio kwa sababu ya hali ya milima na maeneo korofi yanasababisha wananchi kuweza kushindwa kupeleka mazao yao sokoni ili waweze kupata tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Serikali kwenye mpango ujao waone namna angalau katika kilometa zile 300 waanze kupunguza maeneo yale korofi, kuyatengea bajeti ili barabara ile iweze kutekelezeka na watu waweze kupunguza kero za usafiri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo, suala la barabara kutoka Songea - Njombe mpaka Makambako, hili jambo ni la muda mrefu, barabara imechoka. Kama nilivyozungumza mwanzo, inapitisha malori makubwa ya makaa ya mawe kutoka Ngaka. Ile barabara ina mzigo mkubwa, ni ya muda mrefu, imekamilika mwaka 1984, mpaka leo ile barabara kwa kweli hali ni mbaya. Ina mashimo, ukienda ovyo unaweza ukakuta unaingia korongoni kwa sababu ya makorongo ambayo yapo kwenye barabara hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwenye mpango huu, tunapofikiria kutengeneza Liganga na Mchuchuma, basi barabara hii itengewe fedha ili ijengwe upya, siyo kuweka viraka kama wanavyofanya sasa kwa sababu haina manufaa na inachelewesha mizigo ya watu kufika sokoni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)