Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Mwenyekiti,nashukuru sana. Nami nianze kwa kumpongeza Waziri wa Fedha na Mipango kwa kuwasilisha vizuri Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2023/2024. Nianze pia kwa kutambua juhudi za Serikali ambazo inafanya kwa kuhakikisha kwamba miradi mbalimbali inatekelezeka ikiwepo miradi michache tu ambayo nitaitaja:

Tunajenga barabara, tunaboresha viwanja vya ndege, tunaboresha ununuzi wa ndege, kuna shule tunajenga, maji, barabara za vijini, ya Mikoani vyote hivyo ni kazi nzuri ambayo Serikali yetu inafanya. Kwa hiyo, niipongeze sana Serikali na niombe waendelee kukusanya fedha ili hii miradi iishe ikamilike kama tulivyopanga kwenye mpango wa 2022/2023 tupate heshima yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu utajikita kwenye sekta ya kilimo mifugo na uvuvi. Nianze kwa kuipongeza Serikali na Bunge hili lako Tukufu kwa kuongeza bajeti ya kilimo kutoka Shilingi Bilioni 294 mpaka Bilioni 954 na ile ya Wizara ya Mifugo kutoka shilingi bilioni 168 mpaka Shilingi Bilioni 268 ijapokuwa imeongezea Haba na haba hujaza kibaba siyo mbaya sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niishauri Serikali, huu ulikuwa ni uthubutu wa hali ya juu kabisa kuongeza hizi bajeti za hizi sekta mbili tuendelee kuhakikisha kwamba wanapokea hizi pesa ili yale mafanikio ambayo tunategemea wakulima wetu wayaone kule yaweze kuwafikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mapendekezo yangu kwenye mpango nitaanza na kuongelea suala la utafiti kwenye vituo vyetu vya utafiti wa kilimo, ngoja nianze na kilimo. Tumekuwa na mikutano mingi na watafiti wa TARI na pia tumetembelea vituo vya utafiti TARI, tulichokiona kule kunasikitisha, miundombinu ya hivi vituo vya utafiti iko taabani. Tanzania tuna vituo vya utafiti 17 ambavyo miundombinu ya ofisi haijakaa vizuri, ukienda kwenye maabara ni almost hazipo kabisa, ukija kwenye nyumba za kulala za watumishi haziko vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaishukuru Serikali angalau kwa TARI wamewatengea Shilingi Bilioni 39 kwenye mpango huu wa mwaka huu na mambo yanakwenda vizuri. Wameongeza kutoka Bilioni 11 mpaka Bilioni 39. Kwa hiyo tunaishukuru sana Serikali. Niombe kwenye huu mpango kama alivyosema Mheshimiwa Dkt. Thea Ntara kwamba bila utafiti hakuna mahali tutakapokwenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi nyingi zimefanikiwa Duniani kupitia utafiti. Kwa hiyo, tukiwaongezea kwenye huu mpango Watafiti wetu pesa ya kutosha ili waweze kufanya utafiti wa kuzalisha mbegu. Utafiti wa kubuni mbinu bora za kuongeza tija kwenye kilimo tutafika mahali ambapo na sisi tutanufaika na utafiti wetu. Kwa hiyo, kwenye huu mpango niombe ikiwezekana walikuwa wanasema wakipata Shilingi Bilioni 75 watu wa TARI wangefika mahali ambapo watafanya kitu ambacho kinaonekana. Kwa hiyo niombe tufikirie kuwasaidia watu wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu wa pili ni kwenye mpango wa pembejeo. Tunaishukuru sana Serikali yetu ambayo imeshawekeza pesa karibu Shilingi Bilioni 100 kwenye pembejeo za ruzuku hasa ya mbolea. Tunaweza tukatoa mbolea kwa wakulima wetu lakini kama hujawapa mbegu na viuatilifu anaweza asizalishe akafikia pale tunapotaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niishauri Serikali kwenye huu mpango mpya wahakikishe kwamba tunaweka pesa ya kutosha ili tuwapatie wakulima wetu mbegu, mbolea na viuatilifu ili uzalishaji uweze kukamilika kwa sababu bila hivi vyote vitatu kwenda pamoja nafikiri hatutafika mahali pazuri na kama pesa haitoshi ya ruzuku ninapendekeza kwamba tuwe na Mfuko maalumu tuipatie Benki yetu ya kilimo pesa ya kutosha ili waweze kupatia wakulima wetu mikopo nafuu, waweze kununua hivi vitu ambavyo haviwezi kutoka kwenye ruzuku. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu wa tatu kwenye kilimo ni Kilimo cha Umwagiliaji. Kama sote tunavyoona mabadiliko ya tabianchi yamesababisha shida kubwa sana na kuna upungufu wa chakula karibia dunia nzima. Kwa hiyo, sisi kama Taifa tuna bahati nzuri kwamba tuna maeneo mengi na maji ya kutosha kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze Wizara ya Kilimo kwamba ina miradi karibia 36 ambayo ipo inaendelea wanajenga skimu mpya. Niwaombe katika mpango huu tuhakikishe kwamba tunajenga miradi ya umwagiliaji kwenye maeneo ambayo kuna maji ya kutosha ili tuweze kunufaika na hiki kilimo cha umwagiliaji, kikubwa napendekeza pia kwenye huu mpango waongezewe pesa za umwagiliaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la Nne ni kilimo cha bustani, hivi karibuni tumezindua Mpango wa Taifa wa Kilimo cha Bustani, niombe kilimo cha mboga mboga ndiyo kitu ambacho kinaweza kikalikwamua Taifa letu kwa sababu mboga mboga zina bei mahali pote. Kwa hiyo, niiombe Serikali kwenye huu mpango wahakikishe wanafuatilia ule mpango ambao umezinduliwa, mpango wa Kitaifa ili tuweze kutekeleza pamoja na tuhakikishe kwamba wananchi wanazalisha mboga na matunda ya kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu wa nne ni kwenye sekta ya mifugo na uvuvi. Nitazungumzia pia suala la utafiti kwenye hii sekta ya mifugo na uvuvi. Pale mifugo shirika linalo-deal na utafiti pale linaitwa TALIRI, kwenye mwaka wa 2021 walipokea Shilingi Milioni 522.5. Hizi pesa ni ndogo sana kwa watafiti wa mifugo kwamba hii pesa Milioni 500 na tunategemea tupate kitu kikubwa kwa hawa watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, TAFIRI, watafiti wa samaki walipokea Shilingi Bilioni 1.7 mwaka huohuo ambao nimeutaja, angalau siyo mbaya sana lakini wenzao wa TARI mwaka huohuo walipokea Shilingi Bilion 11. Nashauri kwenye mpango huu Serikali ihakikishe kwamba hizi taasisi za utafiti za mifugo na uvuvi zinapatiwa fedha za kutosha ili waweze kutekeleza azma yao ya kuzalisha nyama ya kutosha, waweze kuzalisha ngozi za kutosha, maziwa ya kutosha, kuku wa broiler wa kutosha na samaki wa kutosha. Tusipofanya hivyo tutakuwa hatuwatendei haki na tutakuwa tunawalaumu bure tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa kwenye hii sekta ya uvuvi ni meli ya kufanya utafiti. Tuseme ukweli hawa watu wana-operate katika hali ngumu sana. Meli ya kufanya utafiti hawajanunuliwa ilishaagizwa lakini mpaka sasa hivi haijapatikana. Ninaiomba Serikali tujitahidi angalau tuwapatie hawa watu meli moja ili waweze kufanya utafiti kwenye Bahari Kuu, kule nina hakika kuna fedha nyingi sana ambazo Taifa linaweza kupata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naomba kuunga mkono hoja.