Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Francis Kumba Ndulane

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuweza kutoa mchango wangu kwenye Mpango wa Maendeleo wa mwaka 2023/2024. Mimi ningependa kujikita kwa kuanzia na sekta ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naipongeza Serikali kwa kuongeza fedha katika bajeti yake toka shilingi bilioni 294 hadi shilingi bilioni 954 kati ya mwaka jana na mwaka huu wa fedha. Na ningependa kuchangia eneo hili kwanza kwa sababu, wananchi wetu asilimia 65 ajira zao ziko kwenye kilimo, lakini pia hata Pato la Taifa ni asilimia 26 ya Pato la Taifa linatokana na mazao ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ningependa kusema kwamba, bado sekta hii haijatumika vizuri katika kuifanya nchi yetu iweze kupata mapato mengi zaidi. Ni imani yangu kwamba, kama rasilimali tulizonazo za ardhi, lakini pia kuwa na utaratibu bora wa kusimamia hiki kilimo ungefanyika basi mambo yangekwenda vizuri zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiifuatilia taarifa iliyotolwa na Mheshimiwa Waziri na ile iliyotolewa na Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti, nimeona pale tuna jumla ya hekta milioni 29 za ardhi ambazo zinafaa kwa ajili ya kilimo; lakini ni asilimia 2.75 tu ya eneo hilo ndilo linalotumika kwa kilimo hivi sasa. Kwa hiyo kuna hekta zaidi ya milioni 28 hazitumiki kwa kilimo hivi sasa. Kwa hiyo nilikuwa nafikiri kuna jambo la kufanya katika eneo hili; kwanza ni kuhakikisha kwamba, hizi pesa ambazo zimeongezwa ziendelee kuongezwa ili tuweze kuhudumia miundombinu mbalimbali pamoja na mikakati mbalimbali ya kuboresha kilimo chetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano nimeona hapa idadi ya mabwawa ambayo yatajengwa hapa nchini kulingana na ule mpango wa maendeleo ni machache sana. Nilifikiri Serikali yetu niishauri ijikite katika kuongeza idadi ya mabwawa katika mikoa yote ya nchi nzima na si baadhi tu ya mikoa, kwa sababu nafahamu katika mikoa yote karibu ina idadi kubwa ya mito ambayo inatiririsha maji katika kipindi cha mwaka mzima. Kwa hiyo, ukiondoa Dar-es-Salaam mikoa mingine yote tuna uwezo wa kujenga mabwawa na kuwafanya wakulima wetu wakaweza kuzalisha kwenye hili eneo kubwa ambalo limebaki idle halitumiki kwa ajili ya shughuli za kilimo na kufanya uzalishaji wa mazao ya kilimo, yale ya chakula na ya biashara, yaweze kuzalishwa kwa wingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii itaongeza uchumi kwa sababu, sasa hivi bei ya chakula imepanda sana. Na imepanda si kwa sababu, sisi Tanzania hatulimi, tunalima, lakini tunalima kwa kiasi kidogo na tunahuidumia hadi nchi zinazotuzunguka ambazo kwa sasa zina hali mbaya ya chakula.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia ningeomba Serikali ijikite katika vile vituo ambavyo ni vya kutolea huduma kwa wakulima. Kwanza iviongezee majukumu nje ya yale ambayo yameainishwa kwenye mpango wa maendeleo. Moja kati ya majukumu ambayo ningependekeza yaongezwe ni kufuatilia wakulima wetu, mpaka wale wadogo kabisa, ili kujua changamoto zao zikoje, lakini pia kuona namna ya kutatua hizo changamoto ambazo zinawakabili. Wapo wakulima ambao wanakosa mitaji kwa ajili ya kulima, lakini wapo wakulima wengine wana changamoto mbalimbali. Kwa hiyo zitajulikana kupitia hivi vituo. Na hivi vituo visambae si tu kwa mikoa mitano bali viwepo katika mikoa yote ambayo inalima, ukiondoa Dar-es-Salaam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya pili ningependa kuzungumzia masuala ya utalii. Tumepata mafanikio makubwa kupitia mpango ambao uliasisiwa na Mheshimiwa Rais wetu, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, wa Royal Tour kuhusu ongezeko la mapato kutokana na watalii ambao waliongezeka. Taarifa inaonesha kwamba, asilimia 114.7 iliongezeka katika mwaka wa fedha huu uliopita ukilinganisha na ule uliotangulia. Kiasi kama cha dola zaidi ya 1,000 milioni ziliongezeka kwenye pato la Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nilikuwa naomba sekta hii ya utalii imechangia kwa asilimia 17 katika mwaka wa fedha uliopita kwenye Pato la Taifa. Kwa hiyo nilikuwa naomba hii Royal Tour iwe extended.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitarajia nione kwenye mpango wa Serikali wa maendeleo uainishe basi ni wapi sasa tunakwenda baada ya mafanikio yale ambayo tumeyapata katika mwaka uliopita. Kwa hiyo nilitarajia zile hifadhi zetu mbalimbali ambazo hazijapitiwa na mpango ule wa kwanza, mbuga, mapori ya akiba, kumbukumbu za majimaji kule Lindi kwa maana ya Kilwa na Songea, lakini pia hata yale magofu ya kule Kilwa Kisiwani na Songo Mnara. Kuna wale viboko maalbino tuone waingie hata kama kwa phases.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia, tuone namna ambavyo tutaboresha miundombinu, kwa sababu hizi sekta za usalishaji zinategemeana sana na miundombinu ya barabara. Tuone barabara mbalimbali ambazo sasa zina changamoto kubwa zinakwendaje kusapoti katika uendelezaji wa hizi sekta ambazo ni za uzalishaji mali; kuna barabara ya Nangurukuru – Liwale pale kilometa 258 ipo miaka inaenda miaka inarudi, ule upembuzi yakinifu umefanyika, lakini bado haijajengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nimalizie na sekta ya elimu. Niiombe Serikali sasa iangalie pia kwa walimu. Walimu wamekuwa wakiishi katika mazingira magumu, hawana nyumba, walimu wanakaa watatu-watatu kwenye nyumba za vyumba vitatu-vitatu na familia zao kubwa. Wangalie na upande huo pia ili kuboresha elimu yetu kwa kusudio ambalo limekusudiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nasema naunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)