Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Asia Abdulkarim Halamga

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili kuweza kuchangia katika Mpango wa Bajeti wa Mwaka 2023/2024. Nitaanza kuchangia katika Sekta ya Maliasili na Utalii. Sekta hii ndani ya Taifa letu inachangia pato la Taifa kwa asilimia 17.6, pia inachangia fedha za kigeni kwa asilimia 28. Sekta hii inafanya vizuri sana na tunaona kabisa katika pato la Taifa ni sekta muhimu kwa Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mapendekezo yafuatayo katika sekta hii ya Maliasili na Utalii. Kwenye bajeti iliyopita tuliamua kwamba ndege zetu tuongeze VAT, kwenye hili naomba tulipitie upya kwa sababu ukizingatia Sekta ya Maliasili na Utalii ilikumbwa na janga la Covid 19 na iliweza kuathiri kidogo uchumi na hasa ukiangalia mataifa ya jirani kupitia ndege hizi za kukodi kuna kitu cha kujifunza kupitia tozo hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuendelea kutatua migogoro kati ya wananchi na hifadhi, lakini mapori yetu tengefu, tutakuwa tumefanya jambo kubwa sana, kuondoa migogoro ili kuhakikisha kwamba hifadhi hizi zinaendelea kufanya vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze Serikali kwa kuweza kuanzisha na kuipa TANAPA, kutoka hifadhi 16 hadi kufikia hifadhi 22 na Hifadhi hizo zikiwa Nyerere, Burigi, Ibanda, Kyerwa, Rumanyika, Kigosi na Mto Ugala. Wote sisi ni mashihidi kazi kubwa ambayo ameifanya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa kutangaza filamu ya Royal Tour na wote ni mashuhuda wakubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo ukifika Mkoa wa Kilimanjaro, Arusha, Manyara, kanda zote ambazo zina utalii tunashuhudia kabisa hoteli zimejaa, ziko booked, zingine mpaka mwakani. Kwenye hizi hifadhi mpya ambazo tumeziongeza tukiweza kuweka malango kila hifadhi, ili tukatangaze utalii, sio tu kwa kanda ya kaskazini, tukaongeza na kanda zingine ili kupitia filamu hii ya Mheshimiwa Rais, ambayo imeonesha tija kwa muda mfupi na maeneo mengine yakiweza kupandishwa utalii wao, basi tutapandisha mapato katika nchi yetu na hasa kwa kupata fedha za kigeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi karibuni kupitia fedha za UVIKO, Wizara ya Maliasili na Utalii wameweza kupata vifaa mbalimbali, mfano, Miradi ya REGROW, wameweza kupata vifaa vya kuweza kutengeneza barabara na leo watu wanaopita barabara ya Arusha kwenda Serengeti ni mashihidi wakubwa namna ambavyo barabara zimenyooka na zinaweza kufikika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya mradi huo kukamilika, Miradi ya REGROW, tunaomba bajeti iangalie vizuri sekta hii ili miradi hiyo basi tutakapokuwa tumebaki nayo sisi, iweze kuwa na tija na tuweze kuiendesha. Sio tu mradi unapokamilika tushindwe kuuendesha na hasa tukizingatia tija ambayo imeonesha kwa muda huu mfupi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado tuna kazi hifadhi yetu ya Nyerere kule tumeweza kuianzisha, askari kule wako zaidi ya 120, lakini nyumba zao ziko 30. Tuna kitu cha kufanya ili kuendelea kuhakikisha kwamba sekta hii tunaisimamia vizuri na inaendelea kuleta tija kwa Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuchangia hayo katika Maliasili, naomba niende Wizara ya Kilimo. Katika Ilani yetu ya Uchaguzi ya Mwaka 2020 - 2025, tunaona katika ukurasa wa 42(4) imeongelea suala kubwa la kusaidia nchi yetu katika suala la kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ilani imeongelea kutoka tani 63,000 hadi kufika 2025 tunatarajia kuwa na tani zaidi ya 200,000 za zao la ngano. Zao la Ngano kwa sasa ndani ya nchi yetu tunatumia fedha kubwa za kigeni kuagiza zao hili nje ya nchi na hasa Nchi ya Ukraine. Bahati mbaya sana wote tunajua hali halisi ya Ukraine kwa sasa, najaribu kujiuliza na kutafakari, je, vita ikizidi kuendelea Ukraine sisi tutakuwa na hali gani, ilihali tuna mashamba makubwa katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikitolea mfano wa shamba la NAFCO lililopo Wilaya ya Hanang ambayo lipo chini ya Mwekezaji anayeitwa Ngano Limited. Nimemfuata kaka yangu Bashe sio chini mara moja wala mara mbili, mtu huyu ana hekari takribani 40,000 ambazo hazina tija kwetu sisi Watanzania kwa sababu hakuna anachokizalisha. Inasadikika wamemwongezea tena hekari 10,000, tuna kila sababu ya kuiangalia eneo hili kwa jicho la pili ili tuweze kusaidia nchi yetu katika kukuza ngano na hasa tukizingatia Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya 2020.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtu yule pamoja na kumpa hekari 40,000 pamoja na kutokuzalisha kwake, bado anaendelea kuvamia maeneo ya wananchi wadogo wadogo na anaendelea kusababisha migogoro, kati ya Serikali na wananchi, huku tukizingatia hana chochote ambacho anaingiza kwenye nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo mashamba makubwa mengi katika nchi yetu KTPL yako kule Morogoro, yapo mashamba saba ya maua na mbogamboga kule Arusha, yako mashamba makubwa Songea ya NAFCO. Mashamba haya yana tija gani kwa Taifa letu. Nashauri mashamba haya makubwa yaondolewe chini ya Wizara ya Fedha na yaweze kukabidhiwa Wizara ya Kilimo na iweze kuyasimamia mashamba haya ili tuone tija kwa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo mashamba makubwa wenzetu wanajeshi wanalima kilimo, lakini miundombinu hatuwawezeshi tunaendelea kutengeneza malalamiko, migogoro na kuona wenzetu hawafanyi kazi ambayo inayostahili. Tunaomba mashamba yote makubwa kwenye nchi hii tuweze kuwakabidhi Wizara ya Kilimo na waje na majibu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano leo, JKT vijana wanafundishwa silaha, wanafundishwa kufanya kazi, wanafundishwa kilimo. Tuna mashamba makubwa katika Taifa letu, lakini tujiulize leo tunanunua ngano Ukraine, leo tunanunua alizeti nje ya nchi na bado vijana hawa hawana ajira. Serikali imejipangaje kutumia nguvu kazi ya vijana katika kuleta uchumi katika nchi yetu na hasa rasilimali tuliyokuwa nayo, rasilimali ya ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kusisitiza mwekezaji anaitwa Ngano Limited katika Wilaya ya Hanang, naomba mkataba ukapitiwe upya, hana manufaa yoyote katika Taifa letu kwa sababu hana anachokizalisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa siku ya leo, mchango wangu unaishia hapa. Nakushukuru kwa kunipa nafasi. (Makofi)