Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Abdulhafar Idrissa Juma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mtoni

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. ABDUL-HAFAR IDRISSA JUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru nami kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika mpango huu wa Serikali. Kabla ya kukushukuru wewe namshukuru Mwenyezi Mungu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeusikiliza mpango na nimeusoma kwa umakini na nimeurejea mara kadhaa. Naomba nijiridhishe kwamba Mpango huu umeakisi yale ambayo tuliyaelekeza katika Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi mwaka 2020/2025. Ni chama chetu ndicho ambacho kimemuweka Rais madarakani na sehemu kubwa ya Wabunge tuliomo humu ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo yale yaliyoandikwa kwenye mpango nimeona dhamira ya kuendelea kukamilisha madaraja yale ambayo tumeyaahidi, nimeona dhamira ya kuendelea kuboresha sekta ya afya, nimeona dhamira ya kuendelea kutoa ruzuku kwa wanufaika wa TASAF zaidi ya milioni moja nchi nzima. Kwa hiyo, yale yale ambayo tuliyaahidi kwenye Ilani yetu yanaendelea kutekelezwa na Mama Samia katika Awamu yake ya Sita na kweli kazi inaendelea. Kwa hiyo, hili nimejiridhisha na kwa nafasi hiyo naunga mkono mpango huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme jambo moja, mpango wowote ni kukusanya na kutumia. Mpango wa kutumia umekaa vizuri sana, mpango wa kukusanya unaelekea kukaa vizuri, lakini usimamizi wa yale yaliyokusudiwa kutumiwa bado tuna tatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa naweza nikarudia Taarifa za Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali za miaka takribani miwili au mitatu iliyopita. Kila mwaka katika Ripoti ya Mkaguzi wa Hesabu za Serikali, fedha za wananchi zinapotea katika mazingira tofauti. Fedha hizo tukiweza kuzizuia, tunao uwezo wa kufanya mengi makubwa kwa ajili ya wananchi wetu na hivyo tukaisaidia Serikali yetu kuweza kufanya vizuri zaidi huko mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, umetolewa mfano wa marejesho ya fedha zinazotolewa kama kukopesha wananchi 10% ile ambapo 4% kwa vijana, 4% kwa akina mama na 2% kwa walemavu zaidi ya shilingi bilioni 80 nchi nzima. Shilingi bilioni 80 kama ikisimamiwa vizuri inaweza Kwenda kwa vijana na ikaleta matokeo na kila mwaka fedha zinaongezwa. Lakini tumeona kwenye Ripoti ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali namna fedha hizo wakayi mwingine zinakwenda, zinapotea na hazionekani nini zimefanya. Hatuwaoni vijana waliotajirika kwa fedha hizi katika Halmashauri zetu, hatuwaoni akina mama waliotajirika na wala wenzetu wenye ulemavu waliotajirika. Kuna umuhimu Wizara ya Fedha katika mpango huu mhakikishe mnakwenda kuweka macho katika nafasi hii na maeneo mengine mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba nizungumze jambo lingine kuhusiana na Muungano. Taifa letu ni la Muungano, nchi hii ni Tanzania ni Muungano wa Tanganyika na Zanzibar. Mpango huu umezungumza masuala ya kimuungano katika masuala ya tabianchi. Kuna manufaika na umeelekeza kwamba kutapelekwa fedha na sehemu nyingine iliyozungumzwa ni katika kujenga au kuboresha nyumba ya Makamu wa Rais, Tunguu, napongeza kwa haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna umuhimu wa kutenga fedha maalumu za kufanya utafiti za Muungano wetu mara kwa mara kutokana na mahitaji yake. Katika mpango huu tukiweka fedha maalumu, tukazitenga ambazo zitakuwa kazi zake ni kufanya tafiti tu ya Muungano wetu. Kuna watu wanahoji kwa nini kuna Muungano wa Serikali mbili mpaka leo? Lazima tuwe na tafiti ambazo zitasaidia kuboresha na kuondosha manung’uniko ya kimuungano. Kwa sababu bado wafanyabiashara wa Zanzibar wanaendelea kunung’unika kuhusiana na mambo wanayotengenezewa katika bandari. Sijaona mpango huu ukielekeza ni kipi kifanyike katika kuhakikisha manung’uniko ya wafanyabiashara hasa wadogo wadogo wa Zanzibar wamaweza wakaondolewa vikwazo ili wanufaike na fursa za Muungano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu wakati akija kufanya majumuisho Mheshimiwa Waziri atambue kwamba miongoni mwa fursa ambazo wafanyabiashara wadogo…

MHE. SALIM MUSSA OMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa.

T A A R I F A

MHE. SALIM MUSSA OMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe taarifa mzungumzaji anayezungumza kwa kukazia ukweli juu ya suala la manung’uniko ya wafanyabiashara kutoka Zanzibar hususani kwa kadhia wanazozipata katika bandari ya Dar es Salaam. Hata juzi kuna mfano wa haluwa ya shilingi laki moja tu raia amebanwa pale na kutakiwa kuilipia nusu ya ile bei aliyonunulia. Kwa kweli ni kilio na lazima liangaliwe kwa jicho pevu kabisa, ahsante sana.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Idrissa.

MHE. ABDUL-HAFAR IDRISSA JUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee na nimeipokea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa haya tunayaondoaje? Ni kwa kufanya tafiti tu, ndio maana nashauri Mheshimiwa Waziri akija kuleta majumuisho atuambie na aone umuhimu wa kuwa na fedha maalumu zitakazopelekwa katika Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano kufanya utafiti wa hali ya Muungano wetu kwa sasa, changamoto zilizopo na kutafuta ufumbuzi wa kudumu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi bado najiuliza labda kukiwa na utafiti utaniletea uthibisho mzuri. Kwa nini mpaka leo kama suala la afya sio suala la Muungano? Lakini tukiwa na utafiti unaweza ukatusaidia labda tukiendelea kuwa suala la afya sio suala la Muungano kunaweza kukawapa fursa nyingi zaidi Watanzania, lakini kama likiwa la Muungano litaleta fursa nzuri zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninachoshauri ni umuhimu wa uwepo wa fedha maalumu za utafiti juu ya Muungano wetu, wala tusione aibu kufanya hivyo kwa sababu ndio Muungano pekee, kielelezo cha umoja katika bara la Afrika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nashukuru sana.