Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia Mpango wa Serikali 2022/23. Kwanza nipongeze kazi nzuri anayoifanya Mheshimiwa Rais, kwa kweli ameonesha uwezo mkubwa kama Kiongozi wa Nchi, kila mmoja ni shahidi. Pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Fedha pamoja na timu yake kwa Mpango mzuri ambao wametuletea na leo tunaujadili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaanza kuchangia ninalo swali kwa Mheshimiwa Waziri ambalo anaweza akatujibu wakati anahitimisha Mpango huu. Tumekuwa tukipitisha mipango, tumekuwa na Mpango Mkubwa wa Miaka Mitano, lakini leo hii tuna mpango wa mwaka mmoja ambao ni Mpango wa Tatu; swali langu kwa Mheshimiwa Waziri, ni vizuri tukajiuliza mipango ambayo tumeipitisha hii miaka mitatu tumefanikiwa au bado hatujafanikiwa? Na kama hatujafanikiwa ni kitu gani ambacho tunatakiwa tukifanye ili Mpango huu tunaoujadili leo usije ukashindwa kama mipango mingine?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa tukipitisha mipango na tumekuwa na Mpango mkubwa wa miaka Mitano lakini leo hii tunao mpango wa mwaka Mmoja ambao ni mpango wa Tatu, swali langu kwa Mheshimiwa Waziri ni vizuri tukajiuliza mipango ambayo tumeipitisha hii miaka Mitatu tumefanikiwa au hatujafanikiwa? kama hatujafanikiwa ni kitu gani tunachotakiwa tukifanye ili mpango huu leo tunaoujadili usije ukashindwa kama mipango mingine? Ninaamini hili ninalosema kila Mbunge analo jibu, kwa kweli kwa sehemu kubwa bado hatujafanikiwa kile ambacho tumekipitisha kwenye mpango uliopita. Kwa hiyo, Mheshimwa Waziri hilo ni suala ambalo naomba utujibu kama Wabunge kwa sababu tusiwe tunapitisha mipango mizuri, Wabunge wanatoa ushauri mzuri lakini mwisho wa siku majibu yanayotoka ni asilimia Thelathini, Hamsini hatufiki hata asilimia Sabini Tano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nipongeze sana Serikali, tumesoma kwenye mpango kwa habari ya SGR, SGR ni mradi mzuri sana kwa Taifa kwa sababu umeeleza unavyoenda kuunganisha nchi ya DRC na huko ndiko kwenye biashara kubwa. Ushauri wangu ni kwamba, ili SGR iwe na faida kubwa ni lazima tuwe na mzigo wa kutosha, hatuwezi tukajenga SGR lwa mabilioni halafu hatuna mzigo ambao tutaweza kuupitisha na kurudisha fedha hii ambayo tumekopa. Ili tuweze kuwa na mzigo wa kutosha wakati tunaendelea na mpango wa kujenga kufika kwenye hizo nchi ni lazima tuje na mkakati wa kuboresha bandari yetu. Bandari yetu ya Dar Es Salaam ndiyo tunayoitegemea kwa sehemu kubwa ili tupate mzigo ambao tutapitisha kupeleka nchi jirani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine kwa upande wa bandari, pamoja na uboreshaji unaoendelea bandari ya Dar es Salaam imezidiwa. Bandari ya Dar es Salaam hatuna eneo lingine ambalo tunaweza tukapanua na kuwa na Bandari kubwa, lazima tuje na mpango kabambe wa kuhakikisha tunajenga Bandari ya Bagamoyo. Bagamoyo ndiyo Bandari muhimu itakayoenda kuinua uchumi wa nchi hii. Mimi naamini tukiwa serious tukakubali kukaa kwenye meza tukapanga mipango mizuri na tukaisimamia Bandari ya Bagamoyo itainua Taifa hili. Kwa hiyo niombe sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kujenga Bandari ya Bagamoyo lazima tuongeze ufanisi, ni lazima wakati tunaboresha Bandari yetu ya Dar es Salaam tuangalie hawa washindani wetu ambao kwetu Mungu ametujalia, tunayo mazingira mazuri, tumezungukwa na nchi nyingi majirani, ni kitu gani kinachosababisha wengine wakimbilie Mombasa wengine wakimbilie kwenye nchi nyingine ambako ni mzunguko mkubwa kupeleka mizigo kwenye nchi zao? Hivyo ni lazima tuingie kwenye ushindani na biashara ni ushindani, lazima unapofanya biashara uangalie mwenzako ameboresha wapi ili na wewe uweze kufanya vizuri zaidi. Kwa hiyo, niombe sana hilo tuliangalie kwa ajili ya kuboresha Bandari ya Dar es Salaam ili SGR isije ikawa ni mzigo umekaa tu, kwa sababu kama SGR tunategemea kupeleka abiria tu hakuna chochote ambacho tutafanikiwa, Kwa hiyo niombe sana Mheshimiwa Waziri hili mliangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine niongelee kilimo, kilimo ni biashara, kilimo ni maisha na kilimo ni uchumi. Mungu ameijalia nchi hii mpaka wakati mwingine huwa najiuliza hivi kweli tunaona hii fursa ambayo Mungu ametupatia na tunaitumia ilivyo? Ukiangalia nchi hii imejaliwa vipindi virefu vya mvua, pamoja na mvua bado tunayo maji ya kutosha kwenye maziwa na kwenye mito, hizi fursa na hii neema ambayo Mungu ametupa tunaitumiaje? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumetokea COVID, imetokea vita ya Urusi na Ukraine kule hii fursa tumeitumiaje? Tungekuja na mpango kabambe wa kilimo cha umwagiliaji, tukatenga Kanda. Nimpongeze Mheshimiwa Bashe kule kwetu ameanza na mazao haya ya kimkakati kuanza kuzalisha miche, lakini lazima tutenge kikanda, tuseme Kanda hii itazalisha mpunga, Kanda hii ni korosho na Kanda hii ni mahindi halafu haya mazao tunayoyapata ndiyo tuende kuyauza kwa majirani zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano, Kyerwa peke yake tunailisha Uganda ndizi, yaani ni foleni ndizi iliyokuwa inauzwa shilingi 3,000 leo ni 20,000! Sasa hizi fursa lazima tuziangalie na tuzifanyie kazi, siyo kila siku kinakuja hiki kinaisha, kinakuja hiki hakiishi tunakatia katikati tunakwenda. Kwa hiyo, niombe sana tutumie fursa hii ili tuweze kuboresha kilimo chetu kiwe na tija lakini ili tuwe na kilimo ambacho ni kizuri lazima wakulima hawa tuwaboreshee mazingira. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mmeeleza kwenye mpango kuhusu kuboresha barabara zetu za TARURA, ni kweli barabara zimeanza kuboreshwa lakini bado lazima tujue wakulima wengi wako vijijini, unaongelea barabara 25,000 ambazo Serikali tayari imeshaziboresha. Sehemu kubwa barabara nyingi Waheshimiwa Wabunge ninyi ni mashahidi ni za udongo. Serikali iwekeze kwenye barabara za changarawe ili hawa wananchi ambao ni wazalishaji wakubwa waweze kupeleka mazao yao sokoni na mazao yao yanapokwenda sokoni Serikali inaongeza kipato. Kwa hiyo, ninaiomba sana Serikali kwenye mpango huu ili tuboreshe kilimo tunahitaji barabara nzuri, tunahitaji mazingira mazuri kwa wakulima wetu na ili tuboreshe kilimo kiwe kizuri na tuweze kupata kipato ni lazima tuwe na soko la uhakika. Kwa hiyo ninaomba sana Serikali iliangalie jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nilisemee, tunalo janga la Kitaifa sijui wenzangu mnaliona, mabadiliko ya tabianchi lakini pia na uharibifu unaoendelea tunaoufanya sisi kwa kuharibu vyanzo vya maji, kukata miti na kuchoma mkaa, nchi hii inaenda kuwa jangwa. Serikali lazima ije na mpango kwa kila Halmashauri kuzalisha miti na kuigawa kwa wananchi ili tuende kuboresha yale mazingira ambayo yameharibika vinginevyo tunakoelekea hali ni mbaya. Ninakushukuru. (Makofi)