Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Luhaga Joelson Mpina

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisesa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa wa mwaka 2023/2024 pamoja na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya mwaka 2023/2024.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ninaipongeze Serikali kwa hatua iliyofikia katika ujenzi wa Bwawa la Kidunda ambapo sasa wamepata Mkandarasi sasa tunaenda kupata majawabu ya tatizo la maji katika Mkoa wa Pwani, Morogoro pamoja na Dar es Salaam, lakini wahakikishe kwamba ule mradi wa Ziwa Viktoria kwa Mkoa wa Simiyu ambao karibia Wilaya zote za Busega, Bariadi, Itilima, Maswa, Meatu zote zinahusika na huu mradi na wananchi wanausubiri kwa hamu. Wananchi wa Jimbo langu la Kisesa wanausubiri kwa hamu sana mradi huu kumaliza tatizo la maji ya kunywa, maji ya mifugo, maji ya kilimo na maji ya shughuli mbalimbali zingine za kiuchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala la scheme za umwagiliaji, Wizara inayohusika isisahau kwamba hata huko Simiyu na hata huko Kisesa kuna maeneo mazuri tu kwa ajili ya shughuli za kilimo cha umwagiliaji, hata pamba inawezekana kufanyiwa scheme za umwagiliaji.

Mheshimiwa mwenyekiti, ili tuweze kuwa na mipango mizuri na tuweze kupiga hatua za maendeleo, tunahitaji sana uwekezaji mkubwa kwenye eneo la utafiti. Tunatakiwa tupeleke fedha nyingi COSTECH, TARI, TAFIRI na TAWIRI ili tuweze kupata majawabu ya maendeleo yetu kwa wakati. Mpango huu pia usisahau kutenga fedha za daraja la Mwamhuge kule Jimboni kwangu mpakani mwa Meatu na Maswa ni daraja la muda mrefu na limeahidiwa na Serikali pia daraja la Mto Sanjo ambao ni mpakani mwa Itilima na Meatu, hilo ni daraja la muda mrefu sana kwa hiyo Wizara inayohusika itenge fedha kwa ajili ya hilo daraja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna daraja la Mwambuzo mpakani mwa Meatu na Igunga na Kishapu, hili daraja nalo litengewe fedha ili kuweza kupiga hatua za maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana na wenzangu wamezungumza hapa, Serikali imepiga hatua kubwa sana katika kutafuta masoko ya mazao yetu na huu ndiyo uelekeo tunaoutaka. Mazao ya korosho, parachichi, pamba na mpunga. Kwa kweli katika hili eneo, ninaishukuru sana Serikali kwa sababu wananchi wetu watakapofanya uzalishaji kwa wingi wanapata soko la uhakika. Hili tunaendelea kumpongeza sana Rais wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, kwa kazi nzuri anayoifanya ya kuifungua nchi yetu na kutafuta masoko makubwa Tanzania, kuitafutia nchi yetu masoko makubwa ili kuiunganisha na dunia ili wakulima wetu waweze kulima na kuuza, waweze kuzalisha na kuuza mazao ya samaki, mabondo, tumeona mikataba ya mazao ya mabondo, tumeona mikataba ya samaki na mikataba mingine ambayo ni makubaliano ya masoko mapya. Hiyo ni hatua kubwa sana kwa Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mradi wa kufua umeme wa Bwawa la Mwalimu Nyerere. Mpango umezungumza na Kamati imezungumza. Hapa kwenye Bunge lako nilipendekeza kwamba iundwe Kamati Teule ya Bunge ili kufuatilia ukweli juu ya jambo hili, kwa sababu mara nyingi tumekuwa tukiletewa taarifa ambazo zina mkanganyiko. Leo hii Kamati ya Bajeti imeenda kuthibitisha hilo kwamba taarifa zenye mkanganyiko zimewasilishwa. Mpaka sasa hivi mkataba baina ya TANESCO na Arab Contractors haujulikani kwamba huo muda uliyoongezwa ni muda gani. TANESCO wanasema ni mwaka mmoja (miezi 12) wameongeza. Maana yake kufukia Tarehe 15, Juni 2023 mradi huu utamalizika lakini Contractor pamoja na Wizara na hapa Bungeni tumeambiwa huu mradi utaisha Julai mwaka 2024, miaka miwili kwa maana ya miezi 24, sasa Bunge lako lishike taarifa gani ya kufanyia kazi juu ya hili jambo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati imeeleza kwamba, mkataba huu umeongezwa bila sababu za msingi, mkataba wa Bwawa la Mwalimu Nyerere baina ya Contractor umeongezwa bila sababu za msingi na bila kufanya tathmini, bila kubaini gharama za ongezeko pia gharama hizo za ongezeko la muda zitabebwa na nani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa tukiyauliza haya lakini mara inaelezwa kwamba wako kwenye mvutano, hivi wanavutana jambo gani? Mradi umeshafikia asilimia 75 mnavutana nini? Ni hatari sana kwa mradi uliofikia hatua hiyo halafu mkaingia kwenye mvutano. Tumeuliza hapa mara nyingi hatuelezwi na Kamati nayo imelalamika, mkataba wetu unasema lazima walipe CSR Shilingi Bilioni 260, ailimia Nne ya mkataba mpaka sasa hivi tunaendelea kuwalipa hawa zaidi ya asilimia 70 sasa, lakini hizi fedha hazikatwi na maelezo hayatolewi, tatizo ni nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, Kamati zote zimeshasema, Kamati ya Nishati na Kamati ya Bajeti, kwamba sababu za ucheleweshaji zimesababishwa na Mkandarasi mwenyewe kwa uzembe wake. Sasa kama sababu ni hizo, mkataba wetu unasema, ucheleweshaji wa uzembe ni asilimia 10 ya thamani ya mradi. Asimilia 10 ya trilioni 6.4 ni shilingi bilioni 650, anachelewesha kwa miaka miwili ambayo ni trilioni 1.3, hizi fedha mbona haziombwi? Hakuna mahali popote ambapo Wizara utaiona hata hapa Bungeni ikizungumza kwamba tumeenda kumchaji hizo fedha hakuna hatuelezwi! Zaidi Wizara imekuja hapa inamtetea Mkandarasi, unajua zilikuwa ni sababu za UVIKO-19 lakini Kamati zote zimeshakataa kwamba sababu siyo UVIKO-19, huu ni uzembe wa Mkandarasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini huyu Mkandarasi anabebwa kwa kiwango hicho? Sababu za kubebwa huyu mkandarasi ni nini? Sasa hivi kama tumefikia 70%, hizi fedha tutakuja kuzi-recover na nini? Tunamdai shilingi trilioni 1.3 kwa ucheleweshaji wa mwaka mzima, tunamdai shilingi bilioni 260 kwa ucheleweshaji wa miaka miwili, tunamdai shilingi bilioni 260 za CSR, hizi fedha hazijalipwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napendekeza seriously kwamba hili jambo kama Serikali kila leo imekuwa ikipiga danadana kulifanya, basi iundwe Kamati Teule ya Bunge tuende tukaujue ukweli. Jambo la pili, Bunge liiagize Wizara ya Nishati ikazidai zile fedha, shilingi trilioni 1.56 tunazihitaji kwa ajili ya maendeleo ya Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Deni la Taifa. Deni la Taifa takwimu zinaonesha hapa kutoka Aprili 2021 na kufikia Aprili 2022 limeongezeka kwa shilingi trilioni 8.7, hili ni ongezeko la asilimia 14.4. Hili ongezeko linaongezekaje kwa kiwango hicho wakati deni wakati huo tulili-service kwa shilingi trilioni 7.2, maana yake Serikali katika kipindi hicho imekopa shilingi trilioni 15.92. Hapa Bungeni tuliiruhusu Serikali ikakope shilingi trilioni 10.5, kwa nini Serikali imeenda kukopa zaidi ya kiwango kilichoruhusiwa na Bunge? Kama miradi iliyoidhinishwa na Bunge hapa kwa kasma ya kiwango kilichoruhusiwa kwenda kukopwa pamoja na mapato ya ndani, hizi fedha za ziada zilizokopwa na Serikali zilienda kutekeleza miradi gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa ukiangalia trend ya ongezeko la Deni la Taifa, Deni la Taifa lilikuwa linaongezeka kwa asilimia saba mwaka 2019/2020, lakini ilipofika mwaka 2020/2021, Deni la Taifa likaongezeka kwa wastani wa asilimia 13.7 na mwaka 2022 limeongezeka kwa asilimia 11. Ongezeko hili ni karibia mara mbili, sasa tumefikaje hapa na bahati mbaya sana niliuliza kipindi cha bajeti hili jambo sikupewa majibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ongezeko hili la Deni la Taifa kwa speed kubwa, uwezo wetu wa kukusanya mapato kwa Pato la Taifa ni 11.4%, nchi jirani ya wenzetu wa Kenya ni asilimia 13.7 lakini nchi ya Rwanda ni asilimia 15.9, madeni haya tumefikia hapa. CAG afanye uchunguzi kwenye hili eneo na Serikali itoe maelezo ya kina kuhusu jambo hili. (Makofi)