Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Eng. Mwanaisha Ng'anzi Ulenge

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE. Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa nafasi hii ya kuchangia. Pia nimshukuru Mwenyezi Mungu nwingi wa rehema mwenye enzi na utukufu. Nami naomba kuchangia kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, miaka miwili iliyopita kwa mara ya kwanza nilipochangia hapa Bungeni nilinukuu usemi wa Rais wa 35 wa Marekani John Kennedy, aliposema kwamba “uchumi wa Marekani ni mzuri kwa sababu ya miundombinu yake na wala si miundombinu ya marekani ni mizuri kwa sababu ya uchumi wake”.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali yetu inaamini hivyo pia kwa sababu imetengeneza miradi mingi ikaipa majina ya miradi inayochochea uchumi shirikishi na uchumi shindanishi na imetengeneza miradi ya vielelezo. Kwa hiyo Serikali yetu pia inaamini katika hilo. Hata hivyo tatizo kubwa nililoliona ni kwamba utekelezaji wa miradi ni lazima uhakikishe pia hauongezi Deni la Taifa iwe ni Deni la ndani au Deni la nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivi kwa sababu gani? Jambo hili linawezekana kutekeleza miradi bila kuongeza Deni la Taifa, hili linawezekana. Ila, pale tu ambapo hatuna budi ya Kwenda kukopa basi tukope mikopo ambayo ina masharti nafuu. Ambapo kama tunaipata IMF na World bank mikopo yote ile ina masharti nafuu na ndiyo tunaitumia kukopa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo nililoliona ni kwamba, tunahama sasa kutekeleza miradi yetu kwa kutokuongeza Deni la Taifa kwa kiwango kikubwa, tunakwenda kutaka kutekeleza miradi huku tukiliongeza Deni la Taifa kwa kiwango kikubwa. Kwa mfano; umetanganzwa mradi wa ujenzi wa Barabara ya Kibaha – Mlandizi – Chalinze - Morogoro kwamba utajengwa under EPC+ Finance; kwa maana ya kwamba Mkandarasi anafanya usanifu, anafanya ujenzi na analeta mleta fedha ambaye ndiye huyo Financia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jana Waheshimiwa Wabunge wameonesha kweli tunahitaji kujenga miundombinu yetu bila kuongeza Deni kubwa la Taifa letu. Mheshimiwa Shabiby jana alisema ni vizuri tukijenga miradi yetu kwa kutumia PPP. Kamati imeeleza vizuri kwamba PPP ina changamoto ya sheria yake kwamba masharti ni magumu na mtaji uliowekwa ni kiwango kikubwa. Nafikiri sasa ni wakati sahihi Serikali ikafanya haraka kuirekebisha Sheria ya PPP ili tuweze kutekeleza miradi bila kuongeza Deni la Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye PPP Mbia anajenga halafu ana-operate kwa faida baadaye anaturudishia Serikalini wakati huo huo hakuna interest ambayo sisi tumeichukua kutoka kwake. Kwa hiyo PPP ni njia sahihi n ani nzuri kwa ajili ya kutekeleza miradi yetu bila kuongeza Deni la Taifa na EPC+Finance tunahitaji tui-study vizuri sana kabla ya kuingia kwenye njia hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, njia nyingine ambayo kama Taifa itatusaidia sana kufanya miradi yetu bila kuongeza Deni la Taifa ni kwa kutumia infrastructure bond; na tumekuwa tukilisema hili mara kadhaa. Kwenye infrastructure bond tunachochea uchumi shirikishi. Wananchi wenyewe wa Tanzania wanashiriki katika kutekeleza miradi yao ya maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenye uzoefu na treasury bills wanaweza kusema hapa. Watanzania wapo wengi wenye fedha ambao wanaweza wakatoa milioni kadhaa wakaweka kwa muda wa miaka mitano,kumi au kumi na tano; na sisi kupitia fuel levy ambayo tunapata bilioni 900 kila mwaka, tunaweza kutenga bilioni 300 kila mwaka kwa ajili ya kurudisha hizi bonds za watu. Kwa nini tusitumie njia hii ambayo itatusaidia Watanzania wenyewe kuweza kujiletea maendeleo wakati huo huo deni la taifa halikui? Hata hivyo tumeitangaza barabara ile kwamba tutaijenga under EPC+Finance; je, kiuhalisia tunakopesheka sasa hivi? Mimi ninavyoona, ni kama tumeshamaliza quarter yetu yote. Sasa huyu financier anayekuja, tunaendaje kuchukua pesa kutoka kwake wakati tumemaliza quarter yetu yote?

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile huyu financier siyo yale mashirika makubwa ya dunia kama vile African Development Bank, IMF na World Bank, tuna uhakika gani na riba yake kama haitakuwa kubwa kuliko ya World Bank na IMF? Kwa sababu tumekuwa tukitekeleza miradi ya design and build kwa kutumia mtindo wa kwamba tuna design tuna-build halafu tunaomba mkopo World Bank au IMF au African Development Bank, halafu tunaulipa kwa riba ndogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunarudi kwenye EPC plus finance ambako vile vile Mkandarasi anabuni na kujenga, lakini anakuja na financier. Je, huyu financier riba yake itakuwa ndogo kama ya World Bank? Itakuwa ndogo kama ya African Development Bank? Itakuwa ndogo kama ya IMF? Kwa hiyo, mimi na-discourage EPC plus finance, we better tukaamua kukaa chini na kuiangalia vizuri infrastructure bond. Wenzetu wameweza kufanya haya, kwa nini sisi Tanzania tunaogopa kuingia kwenye infastracture bond?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ghana wanatekeleza miradi yao kwa kutumia infrastructure bond, Kenya imetengeneza sheria ya kufanya hivyo kwa kutumia infrastructure bond, sisi tunaogopa nini? Tunahitaji uchumi shirikishi na infrastructure bond inamwezesha Mtanzania kuweza kujenga barabara zake na yeye kuchangia maendeleo yake. Inakuwaje tuna- hesitate kuingia katika njia hii? Shida iko wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria yetu ilivyo sasa hivi, mwenye mamlaka ya kukopa ni Wizara ya Fedha peke yake. Wenzetu South Africa wanatekeleza EPC+Finance lakini wameipa Road Authority mamlaka ya kukopa. Maana yake ni kwamba inapotokea hali kama hii ya sasa kwamba quarter yetu tumeimaliza, Road Authority ana mamlaka ya kukopa; lakini sisi sasa hivi hatuwezi kutekeleza under EPC+Finance. Kwa nini tusitumie infrastructure bond kutengeneza uchumi shirikishi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa katika nchi zote za SADC, ni Tanzania peke yake ndiyo haina toll road so far. Ni dhana tu ambayo imejengeka kwamba toll road ni mpaka zijengwe na hela za mbia labda IPP ndiyo tutengeneze toll roads, siyo kweli. Nchi kama Zambia hata madaraja yao ikiwa na span zaidi ya 100 tu inakuwa ni toll, watu wanalipia. Unaona! Kwa hiyo, pale pale tunakuwa tuna-generate mapato ya ndani kuweza kuendeleza miundombinu yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi huko nyuma miaka ya 1990, nimejaribu kutafuta na kupitia, tuliwahi kuwa na toll gates Ubungo, Chalinze, Makambako na Segera. Magari yalikuwa yanasimama na yanalipia, lakini sasa hivi tumetengeneza mentality ya kwamba mpaka tujenge under PPP ndiyo tunaweza tukaweka toll roads, siyo kweli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiingia Zambia, ukisoma Road Authority yake kwenye annual report inaonesha wazi kwamba wana-operate na both. Wanafanya toll roads na vilevile wanatumia fuel levy. Kwa nini sisi tushindwe kwenda kama nchi za wenzetu za jirani? Nimemaliza hapo na-insist tujenge kwa kutumia infrastructure bond ili tuweze kuwa na uchumi shirikishi na vilevile tuweze kupunguza deni la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuchangia kuhusiana na TAA. Kwa mujibu wa malengo yaliyowekwa kwa kuanzisha TAA, imepewa jukumu la kuendeleza miundombinu na vilevile kwa maelezo ya ICAO (International Civil Aviation Organization) inataka kila Mamlaka ya Viwanja vya Ndege iwe na chanzo cha mapato; na sisi tumeweka Passenger Service Charge ambayo tunapata Shilingi bilioni 65 kila mwaka ili iweze kuendeleza viwanja vya ndege, lakini hii Shilingi bilioni 65 yote inachukuliwa na TRA na mamlaka iliyozalisha haipati hata Shilingi moja; je, tutaendelezaje viwanja hivyo vya ndege?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumefanya kazi nzuri, Mheshimiwa Rais amefanya kazi kubwa sana kupitia Royal Tour, lakini so far viwanja vya ndege vina hali duni. Tuwarudishie TAA pesa yao ili waweze kuboresha viwanja vya ndege kwa mujibu wa vikao.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)