Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Innocent Edward Kalogeris

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi ys kuchangia Mpango wa Taifa wa maendeleo. Nitumie nafasi hii kumpongeza sana Mama yetu, Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kubwa anayoifanya katika kuiendeleza nchi yetu. Nitumie nafasi hii na mimi nitoe mchango wangu kwa Taifa kwenye sekta ya utalii. Sisi wote ni mashuhuda, Mama amefanya kazi kubwa kupitia Royal Tour, watalii wamekuwa wengi na kuna kila sababu ya sasa kuelekeza maeneo mengine yenye utalii ili kusudi tuweze kuongeza pato kwenye Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa hivi utalii upo katika Nyanda ya Kaskazini, lakini nchi yetu imepata bahati ya kuwa na vivutio vingi vya kitalii hata katika sehemu zote za Tanzania. Kuna mradi mkubwa ambao unafanyika wa kuendeleza utalii na kuendeleza rasilimali kusini ya nchi ya Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna Mbuga ya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere lakini kuna Mbuga ya Mikumi, kuna Mbuga ya Uduzungwa zipo katika Mkoa wa Morogoro. Vile vile kuna Mbuga ya Ruaha Mkoa wa Iringa na kuna Mbuga ya Katavi Mkoani Katavi. Katika mpango huu wa REGROW tuna kila sababu ya kudhani kwamba, kama Serikali itasimamia kikamilifu mpango huu tuna uhakika wa kupata mapato mengi kwenye mbuga katika Ukanda wa Kusini na kuongeza mapato makubwa katika Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niombe tu kupitia mpango huu Serikali isimame na ihakikishe kwamba kuna fedha nyingi, najua zimepelekwa, zikasimamiwe inavyopaswa ili ziweze kuleta matokeo chanya. Yakajengwe madaraja kwenye hifadhi zetu, zikajengwe barabara kwenye hifadhi zetu, lakini vile vile zikatumike kufanya promotion ya utalii ili kusudi tuongeze pesa katika sekta ya utalii na kuweza kupata mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini, sambamba na hilo katika mbuga ya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ambayo iko Wilayani Morogoro, niiombe Serikali, ili kuweza kuwafanya watalii waweze kufika kwa haraka lakini vile vile kwa wepesi na kwa wingi barabara ya Digwa-Kisaki iko katika mpango wa ujenzi. Bajeti iliyopita imetangazwa, tuliahidiwa mpaka kufikia Mwezi wa Tisa itakuwa tayari imeshatangazwa kwenye TANePS kwa ajili ya kumpata mkandarasi. Hata hivyo, mpaka muda huu tunaozungumza jambo hili halija-tick. Nikuombe tu Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana ya ujenzi lakini Waziri wa Fedha najua fedha ipo basi kazi hii ifanyike ili kusudi suala hili likamilike tuweze kuongeza utalii. Tukiweza kuongeza watalii kwa upande wa kusini ni imani yangu kwamba tutakuwa tumepata fedha nyingi za utalii na tutaweza kusaidia kusukuma maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hili, nitumie nafasi hii kuipongeza Kamati ya Bajeti, tumeona ujenzi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere. Bwawa la Mwalimu Nyerere lipo katika Halmashauri ya Morogoro Vijijini, Jimbo la Morogoro Kusini ambalo mimi nipo kule, lakini vile vile lipo katika Halmashauri ya Rufiji. Bwawa hili likikamilika litaweza kuleta matokeo makubwa sana katika uchumi wa nchi yetu. Niombe Serikali ikasimame katika mazingira yanayotakiwa kuhakikisha kwamba linakwisha kwa muda na wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati ya Bajeti imesema, mradi ulikuwa unatakiwa kukamilika tarehe 15 mwezi Juni mwaka huu, lakini wameongezewa mpaka tarehe 15 mwezi Juni mwaka unaokuja. Ombi langu kwa Serikali, wakandarasi, na mimi mwenyewe ni mkandarasi, kuna ujanja na ubabaishaji; wanaweza wakafika mahali wakataka kutucheleweshea mradi wetu ambao kwetu sisi tunauhitaji kwa kiasi kikubwa. Tuhakikishe kwamba muda huu waliopewa kwa mujibu wa utaratibu kazi iwe imekamilika; kwa sababu; moja, inaonekana, vile vile Kamati yetu imesema, wameongezewa mwaka mmoja lakini mpango kazi wa mkandarasi huyu unaonekana kwamba atamaliza kazi hiyo mwaka 2023.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mimi niombe, wenzetu ambao wanasimama TANESCO wakahakikishe kwamba wanasimama kikamilifu kuhakikisha mradi huu unakamilika ndani ya muda ili yale matumaini ya Watanzania kupata umeme wa uhakika lakini uliokuwa salama uwe umekamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini, katika suala hili la mradi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere kuna suala la CSR. Halmashauri ya Morogoro Vijijini na Halmashauri ya Rufiji mpaka tunafikia asilimia 75 ya ujenzi wa Bwawa hili bado hatujapata fedha yetu ya CSR kwa mujibu wa mkataba unavyosema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbaya zaidi napata mashaka, kupitia Kamati ya Bajeti, TANESCO kwa mara ya kwanza walipeleka kwa mkandarasi ujenzi wa uwanja wa michezo Dodoma. Mkandarasi akakataa kwa sababu haikidhi vigezo vinavyotakiwa. Lakini tayari katika Kamati ya Bajeti nimeona, safari hii TANESCO tena wamepeleka miradi ambayo haihusiani na wananchi wa Morogoro Vijiji na Halmashauri ya Rufiji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiuhalisia kuna ujenzi ambao unaambiwa unataka kujenga chuo cha umeme na gesi asilia Lindi, sitaki wala sina mashaka na Serikali kufanya hivyo. Kuna ujenzi wa kituo cha TEHAMA – Kigoma, sina mashaka na Serikali kufanya hivyo, lakini kuna ujenzi wa kituo cha Afya au Zahanati Dodoma sina mashaka na hilo lakini vilevile Tanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Morogoro hata sisi Halmashauri ya Morogoro Vijijini wanahitaji huduma hizo. Kama ni suala la Chuo cha Umeme, gesi asilia, kwa nini kisijengwe Morogoro au kikajengwa Pwani? Ninaishukuru Kamati ya Bajeti imeliona hilo na imesema, tunaomba fedha ya CSR ambayo iko ndani ya Halmashauri mbili; ya Morogoro Vijijini na Halmashauri ya Rufiji ije kwetu wananchi wenye halmashauri hizo kama vile utaratibu wa mkataba unavyosema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la kilimo. Kilimo ndiyo uti wa mgongo na katika hili umeshuhudia hapa mchana leo kutwa nzima Waheshimiwa Wabunge wakizungumza suala la upungufu wa chakula na tatizo la mvua. Tumefanya kazi kubwa kwenye mbolea, mbegu, viuatilifu na kila kitu. Nadhani ni wakati muafaka sasa hivi tukajipanga katika bajeti yetu ijayo katika kilimo cha umwagiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania ina maeneo makubwa ya kulima kilimo cha umwagiliaji. Mfano katika Mkoa wetu wa Morogoro, tuna zaidi ya hekta 2,000,000 zinazofaa katika kilimo cha umwagiliaji, lakini kila mwaka Serikali inapokuja inaendelea kuleta bajeti kwenye maeneo ya miradi midogo midogo tu ya umwagiliaji. Nadhani ni wakati muafaka kwa Serikali katika bajeti ijayo, kuangalia miradi mikubwa ambayo italeta tija na wingi wa chakula katika nchi, kitoshe nchini na ikiwezekana tusambaze kwa kuuza nje ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hili, naiomba Serikali, katika mwaka unaokuja iangalie uwezekano wa kuvuna maji ya mvua. Nilishalizungumza katika bajeti karibu mbili. Kipindi cha mvua, pale Mbande, kuna eneo linaitwa Matoroli, maji yanavuka mpaka juu ya barabara. Pia kipindi cha mvua, pale Mtanana karibu na Kibaigwa, maji yanavuka hadi juu ya barabara. Dumila vile vile mpaka yanafanya uharibifu mkubwa kwenye miundombinu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile tuna mabwawa katika station ya reli Msaganza-Kidete. Nadhani ni wakati muafaka kwa Serikali katika bajeti inayokuja ikaelekeza kufukua mabwawa yale, lakini tukachimba mabwawa katika maeneo haya niliyoyasema ili tuvune maji ya mvua, tufanye kilimo cha umwagiliaji ambacho ndicho chenye uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la maji. Niendelee kuipongeza Serikali kwa kazi kubwa ambayo inaifanya katika suala la maji. Karibu tumepata taarifa, maji yamefika vijijini kuna mahali asilimia 80, asilimia 75, lakini uhalisia ni kwamba bado changamoto ya maji ni kubwa katika nchi yetu. Naishauri Serikali yangu, katika bajeti inayokuja, hebu ijielekeze kwenye kufanya miradi mikubwa ya maji yenye uhakika ili iweze kusambaza maji katika maeneo mengi na tukaondokana na adha hii ya maji, kuliko hii miradi midogo midogo ya kuchimba visima, halafu ndani ya kipindi kifupi visima vimekauka; kuchukua maji kwenye mito midogo midogo wakati tuna maziwa makubwa katika nchi hii ambayo tukiyatumia yanaweza kupunguza kero ya maji nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile naomba kwa Serikali yangu, ijitahidi kwa kiasi inachoweza kufanya kufanikisha haya yote ili kuleta tija na mafanikio kwa Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Huo ndiyo ulikuwa mchango wangu. (Makofi)