Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Kasalali Emmanuel Mageni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sumve

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa hii nafasi uliyonipatia. Awali ninaipongeza Wizara ya Fedha kwa huu mpango ambao wameuleta hapa, ni mpango ambao unaonesha matumaini kwenye uchumi wetu lakini kwa kuutazama na mimi nimeona walau niongeze mchango wangu ili kuboresha katika maeneo machache.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sote tunafahamu na wachangiaji wa mwanzo wamechangia na kuzungumza kuhusu umuhimu wa Sekta ya Kilimo. Sekta ya kilimo, Watanzania tumekuwa tukisema ndiyo uti wa mgongo wa uchumi wetu. Sekta ya Kilimo kwa taarifa ambazo zipo na zimeandikwa kwenye taarifa ya Waziri wakati anatoa mpango ni kwamba bajeti imepanda kutoka bilioni 254, mpaka zaidi ya bilioni 900. Sekta hii inatoa ajira asilimia 65 na zaidi ya Watanzania. Kwa hiyo sekta ya kilimo ni sekta ya muhimu sana na kama tunataka kutoka hapa tulipo twende pazuri zaidi ni lazima tuongeze nguvu kwenye sekta ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya kilimo inayo maeneo mengi ya msingi lakini nitazungumzia eneo moja la usafirishaji wa mazao ya kilimo. Mazao yetu ya kilimo mengi yanatoka maeneo ya vijijini, wakulima wetu wanapolima mazao yao wanatumia gharama kubwa sana kuyasafirisha. Jambo ambalo limekuwa likisababisha bei ya mkulima kuwa chini lakini bei ya mazao kwa mlaji inakuwa juu. Naishauri Serikali kwamba iwekeze zaidi kwenye kuhakisha barabara zilizoko vijijini ambako ndiko kwa wakulima wenyewe zinaboreshwa ili ziweze ku- accommodate usafirishaji wa mazao haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naweza nikatoa mfano kwa sababu mimi pia ni Mbunge ambaye ninatoka kwenye Jimbo ambalo asilimia kubwa ni wakulima na wafugaji, Jimbo la Sumve. Katika Jimbo zima la Sumve hakuna barabara ambayo inaruhusu gari la zaidi ya tani kumi kupita. Ina maana ili ubebe mazao ya pamba kwa mujibu wa sheria za barabara zetu zilivyo unatakiwa utumie canter au magari mengine madogo madogo ukishatoka Sumve ndiyo utafute magari makubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa utaratibu huu wa kuwa na barabara mbovu kwenye maeneo ya uzalishaji hatumsaidii mkulima, lazima Wizara ndugu yangu Mwigulu Nchemba Waziri tufikirie hili jambo kwa undani wake. Ndiyo maana kila muda tunaposimama tuataka kushauri kuhusu maendeleo ya nchi hii, tunaotoka huko vijijini tunalia na miundombinu ya usafirishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani umefika wakati sasa Serikali ichukue hatua kwa ajili ya kukuza uchumi wetu. Tunapata taabu sana kwa mazao yetu kufika Mjini yakiwa na bei kubwa na wakulima wetu kupata bei ndogo kwa sababu ya matatizo ya usafiri, halafu tunasema tunaboresha barabara za mijini wakati sisi wa vijijini kila siku tunazungumzia barabara zetu. Hili jambo nilitaka Serikali iliangalie kwa jicho la pili kwa ajili ya kukuza uchumi wa vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo limezungumzwa sana hapa na michango iliyopita ni kuhusu tunapanga Bajeti hapa, tunapeleka pesa kwenye Halmashauri zetu kwa ajili ya pesa zile kutumika kuleta maendeleo kule lakini pesa zile zimekuwa hazifanyi kazi iliyopangwa. Pesa hizo zinafika kule zinapotea mwisho wa siku unakuta Waziri wa Idara kama TAMISEMI, unakuta kazi yake yeye ni kutumbua kushughulika na wezi kutengeneza Tume za kuchunguza na mwisho wa siku badala ya ile pesa kufanya kazi tunahangaika kufunga watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mimi nafikiri tunatakiwa mpango wetu wa maendeleo huu uangalie hilo kwa jicho la pili. Lazima tujiulize kwa nini pesa nyingi zinazopelekwa kwenye Halmashauri zinakwenda zinaibiwa? Kwa nini iko shida kule? Halmashauri mfumo wake ukiuangalia umewekwa vizuri sana kisheria, Halmashauri zinasimamiwa na Mabaraza ya Madiwani, hawa Madiwani kwa mujibu wa sheria ndiyo walinzi wa Halmashauri zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Halmashauri tunapeleka Mabilioni ya pesa halafu kwenye mpango huu tumepanga wale walinzi wetu tunawalipa kiduchu ndiyo walinde hizo pesa. Kila siku tutatengeneza tume tusipofahamu siri ya wizi. Kwenye Halmashauri imefika wakati sasa hivi Madiwani hawafanyi hata ziara, yaani wale Watumishi wanatumia loophole ya Madiwani kutokuenda, mipango yetu na nyaraka zetu na maelekezo ya Mawaziri imefika wakati Madiwani wale wanaolinda mali zetu tunazopeleka kule, wanakutana kwenye Kamati kujadili makabrasha makubwa ambayo hawajajua hata hiyo miradi ikoje. Ziara za Madiwani za Kamati, zimefutwa, wanasema ni maelekezo ya Wizara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, inafika wakati utendaji kule umekuwa chini, kwa hiyo hawa walinzi wetu hawafanyi kabisa kazi vizuri, kwa hiyo mwisho wa siku ukiwa na walinzi dhaifu wanashirikiana na mwizi kukuibia. Kwa hiyo, kila siku tutakuwa tunapeleka pesa kule, tutakuwa tunakaa hapa tunapanga mabilioni kama hatujaangalia namna gani tunalinda pesa tulizozipeleka kule. Tutaendelea kuwapa kazi Mawaziri ya kutumbua, kazi ya kusimamisha, TAKUKURU kagua, anafika Mheshimiwa Waziri Mkuu kule anakuta yaani miradi mpaka afike Waziri Mkuu ndiyo ionwe wakati huo kuna wasimamizi kule ambao ni Madiwani, nadhani hili jambo tunatakiwa tuliangalie kwa jicho la pili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi yetu itaendelea kuibiwa ni lazima Serikali ije na mpango wa kulinda mali tunazopeleka kwenye Halmashauri. Halmashauri ndiyo chanzo cha maendeleo ya watu wetu. Nadhani hata Wabunge ni mashahidi. Hapa Wizara zinazotembelewa mara nyingi na Wabunge ni TAMISEMI. Sasa TAMISEMI huko ndiko kapu la pesa zinazowahusu wananchi wetu zinaenda kule, huu mpango tunapanga pesa nyingi tunapeleka kule. Sasa kule hakuna walinzi tumeweka watu tu wa kushirikiana na wengine kuiba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtu unapompa pesa humwekei mlinzi unamshawishi kuziiba ni lazima tuwe na mpango wa kulinda hizi pesa zetu vinginevyo…

MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

T A A R I F A

MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naomba nimpe taarifa mzungumzaji, ndani ya huu mwaka tu mmoja zipo Halmashauri ambazo zimepokea Nyaraka Mbili tofauti zinazotoka TAMISEMI, juu ya Madiwani. Mwanzo waliongezewa posho zao lakini ikatokea tena waraka ndani ya huu mwaka mmoja wamepunguziwa posho zao. Kwa hiyo naungana kabisa nahoja ya Mheshimiwa, hawa walinzi wetu wanakaa hawaelewi kesho wataamka wako katika hali gani.

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa hii naipokea na ninasisitiza ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge Serikali hili jambo tulipeni umuhimu wake ili pesa tunazozipanga na kuzipeleka huko zitumike vizuri. Nakushukuru sana. (Makofi)