Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Michael Constantino Mwakamo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibaha Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kunipatia nafasi na mimi ya kuchangia mpango huu. Niombe kwanza kuipongeza Wizara kwa kutuletea mipango mara zote ambayo huwa inapokelewa vizuri kwa Wabunge, pia inapokelewa vizuri kwa wananchi na wanakuwa na matumaini makubwa ya kuona yanayopangwa yanakwenda kutekelezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimepitia mpango, nimeusoma, nimesikiliza pia mapendekezo ya Wizara, nimesikiliza mapendekezo ya Kamati yetu muhimu kabisa inayochambua mpango kwa kina, nimeona vipaumbele vya Serikali, lakini kwa kweli nimevutiwa sana na kipaumbele hiki cha kusukuma na kuimarisha sekta ya uzalishaji. Katika maeneo haya, nami nimeona nitoe mchango wangu kidogo kwa kutazama maeneo yafuatayo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona kwamba, Serikali imeweka mpango kwenye suala zima la sekta ya kilimo na wamezungumzia kwenye sekta ya kilimo eneo la kilimo cha pamoja. Ni jambo jema na niseme hili jambo si geni sana, kwa wale wakongwe wa miaka mingi, enzi za Mwalimu walikuwa na kilimo cha pamoja. Maeneo mengi ya vijiji yalikuwa na kilimo cha bega kwa bega na yaliwasaidia wananchi kwenye kuhakikisha kwamba, wanalinda kwa pamoja, wanavuna kwa pamoja na wanafanya mambo yao vizuri. Ni wazo jema leo Serikali imeona irudi kule na ifikirie kilimo cha pamoja kwa ajili ya kukuza uchumi wa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna jambo hapa liendelee kutazamwa. Tumefikiria kuanzisha kilimo cha pamoja, lakini tumeenda kuanza kwenye maeneo ambayo upatikanaji wa maji ni wa kutegemea mvua. Yapo mabonde ambayo kwa hakika kabisa kama Serikali itatupia jicho huko, yana mabonde ya asili ambayo maji yanatiririka kwa muwa mrefu; tuna mabonde ya Mto Ruvu, tuna mabonde ya Mto Rufiji, tuna mabonde makubwa ambayo maji yake yapo miaka yote miaka nenda miaka rudi. Ni mpango tu wa Serikali kuwekeza nguvu kule na kuwasaidia wananchi waliopo maeneo yale kulima kulingana na maji yale yanavyopatikana kwa maana ya kuwapelekea pembejeo za kutosha, kuwapelekea mitambo inayoweza kufanya uzalishaji wa kisasa zaidi ili kuwaondoa kwenye kilimo cha jembe la mkono na uzalishaji ukawa mkubwa sana. Tukifanya hivi uzalishaji utakuwa mkubwa na Taifa hili linaweza kwenda kujiongezea kipato na linaweza kwenda kufanya mambo makubwa sana kwa sababu, wananchi wake watakuwa wamejitosheleza kwa chakula na wanaweza sasa kufanya utaratibu mwingine wa matumizi ya fedha inayobaki kama bakaa kwenye shughuli nyingine za Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona kwamba, kuna suala zima limezungumzwa kwenye mipango kule la miradi ya kimkakati. Miradi hii ya kimkakati mingi inatekelezwa kwenye maeneo ya Halmashauri, lakini tangu tuanzishe hii program, sera hii ya miradi ya kimkakati ni miradi michache ya kimkakati imetekelezwa kwenye Halmashauri hizi. Kwa nini inatekelezwa michache?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu, vile vigezo vinavyowekwa kufikia kutekeleza hii miradi ya kimkakati, Halmashauri nyingine zinashindwa. Ukiangalia kwamba, Halmashauri nyingi nchini zina kipato kidogo, wako chini ya mapato yao ya ndani ya Bilioni 1.5 au Bilioni Mbili. Ukiangalia moja ya sharti ambalo wanalo wanatakiwa watengeneze mpango wao, wapitishe kila kitu kwenye ngazi yao, kwa gharama zao ndiyo waweze kupewa pesa hizi za Serikali kuendesha hii miradi ya kimkakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeishauri Serikali kupitia hili eneo, ingewezekana Serikali pale Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, wangekuwa na timu maalum ya kutengeneza miradi, kwa sababu Halmashauri nyingi hazina wataalam wa kutosha, badala ya kutumia mapato machache ya Halmashauri kuwatafuta wataalam wa kuwatengenezea maandiko kungekuwa na timu maalum ipo pale Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa ambayo inakwenda kwenye zile Halmashauri zinazofahamika zina kipato kidogo kabisa, kwenda kuwasaidia kutengeneza mipango yao, ili ile mipango yao iweze kuwezeshwa na Serikali na iweze kuwasababishia kuwaongezea kipato kwenye maeneo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, badala ya kutumia mapato kidogo ya Halmashauri kuwatafuta wataalam wa kuwatengenezea maandiko, kungekuwa na timu maalum tu pale TAMISEMI ambayo inakwenda kwenye zile halmashauri zinazofahamika zina kipato kidogo kabisa kuwasaidia kutengeneza mipango yao ile iweze kuwezeshwa na Serikali na iweze kuwasababishia kuwaongezea kipato kwenye maeneo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tukibaki na hii sera, kwamba halmashauri ambayo haina kipato yenyewe ndiyo ijiandalie andiko ilhali hawana wataalam, wanachukua kilekile kidogo ambacho wamezalisha wanakwenda kumlipa mtaalam wa nje ili awatengenezee andiko. Sasa kwa kitendo kile, badala ya kutumia kipato kidogo kwa ajili ya kuendeleza shughuli za halmashauri wanakitoa tena kufanya shughuli nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaishauri Serikali, hasa pale TAMISEMI, kuwe na timu. Inawezekana kabisa kukawa na timu moja pale iliyoandaliwa ya watu wachache, watalaam wazuri wa kuandika maandiko, wakawa wanakwenda katika halmashauri moja moja wanadaa maandiko na wanayafanyia kazi, hizo halmashauri zinaendelea kuzalisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na kwa kitendo hicho cha kuzalisha maana yake sasa uchumi wa eneo hilo utakuwa, kwa maana ya kwamba halmashauri itakuwa na mapato ya kutosha, lakini vilevile wananchi watakuwa na mapato ya kutosha. Na kwa kufanya hivyo basi Serikali itakuwa inakusanya kodi vizuri na Pato la Taifa litaweza kuongezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo ninaomba nilizungumzie ni suala zima la utekelezaji wa miradi. Nishukuru nimesoma kwenye maoni ya Kamati, nimegundua wamezungumzia ufinyu wa eneo la Bandari ya Dar es Salaam; na wameona ufumbuzi pekee wa kuondoa tatizo la Bandari ya Dar es Salaam ni kutanuka kwenda kufanya shughuli kwenye Bandari inayofikiriwa ya Bagamoyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze sana Kamati na Serikali. Ushauri na rai yangu pale; niwaombe sana hili wazo si la kuliachia jamani. Wote tunaona sasa hivi nchi yetu tunaitumia Bandari ya Dar es Salaam kutoa mizigo kwenda nchi za jirani na ndilo eneo pekee linalotuingizia pato la kutosha kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vizuri kwa kweli tukatengeneza ile Bandari ya Bagamoyo ikafanyiwa utaratibu ianze mchakato wake kwa sababu itaisaidia Bandari ya Dar es Salaam. Na kwa sababu Bagamoyo na Dar es Salaam ni jirani, meli zile zitakuwa zinafanya kazi vizuri na wakati huo zitakuwa zinatoa mzigo pale na kwenda kwenye maeneo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe Serikali, kwenye bajeti inayokuja, kwenye mpango unaokuja, ni vizuri wakaiweka hii katika hatua ya kwenda kuitekeleza. Yale masharti ambayo yanaonekana yana changamoto ndio wakati Serikali kuyaondoa, na tutakapokuwa tumeyaondoa yale basi shughuli hiyo itakwenda kuanza vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba ukiangalia suala la Bandari ya Dar es Salaam kwa maana ya kwamba na kuitazama hiyo Bandari ya Bagamoyo kuifikiria kwenda kuanza, ukiangalia Dar es Salaam kote ndiyo kunakoanza njia kuu zinazoweza kutoa mizigo. Tuna Reli ya Kati, tuna Reli ya TAZARA, tuna Barabara ya Dar es Salaam – Morogoro – Mwanza, na sasa tuna mwendokasi (SGR); zote hizi ni njia kuu za kusafirisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunategemea kule kwenye chanzo cha njia kuu za kusafirisha ndiko ambako mizigo itashuka, sasa kwa sababu tayari nako tumeongeza Bandari ya Kwala ambayo nayo inawekwa pale kwa ajili ya kusaidia kupunguza mzigo wa Dar es Salaam, sasa itakuwa imekaa mwelekeo mzuri tu. Bagamoyo itakuwa inafanya kazi, Dar es Salaam inafanya kazi, Bandari ya Kwala inapokea mizigo; hizi reli nilizozitaja zinatoa mizigo kupeleka kwenye maeneo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na kwa kufanya hivi niishauri Serikali, ni vizuri kwenye bajeti inayokuja ikawekeza nguvu hii miradi mikubwa kama huu wa Bagamoyo na barabara yake ya kutoka Bagamoyo kwenda maeneo mengine ili iweze kuungana na Kwala, mizigo iwe inasafirishwa kwa urahisi. Kwa kufanya hivi Pato la Taifa na pato la mtu mmoja mmoja litaongezeka. Tukifanya hivyo vilevile tunasababisha wawekezaji ambao wanakwenda kukaa kwenye maeneo yale ambayo miundombinu hiyo ipo watakuwa wanafanya kazi kwa njia rahisi zaidi, na kwa kufanya hivyo basi tutakuwa tunakamilisha malengo ya kukuza uchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, mimi nishauri na nitoe maoni machache. Kwanza niiombe Serikali kwamba ifanye mapitio ya mabonde yote makubwa. Badala ya kukaa kuanza kufikiria ni maeneo gani tupeleke pesa za kilimo zikafanye kazi yenyewe ifanye kazi ya kupitia mabonde yote makubwa kama vile Bonde la Mto Ruvu, Wami, Mto Rufiji, kule Ifakara, kuna mabonde makubwa, waende kwenye maeneo hayo wakafanye utafiti wa kutosha kwa kupima udongo ule, waone unaweza kutumika kwa namna gani na maeneo hayo yanafaa kilimo cha namna gani, tupeleke hii bajeti kubwa ya Serikali ya kilimo kwenye maeneo hayo ili tuweze kuondoa changamoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kwenye maeneo hayo kuna suala limezungumzwa la kutengeneza programu maalum ya uwezeshaji wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa. Sote humu ndani Wabunge tunafahamu, kila Mbunge amepiga kelele ni namna gani fedha zinavyotumika vibaya kwenye halmashauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ukiangalia tatizo la matumizi mabaya ya fedha kwenye halmshauri inawezekana likawa linasababishwa na usimamizi mdogo unaotokea katika sekretarieti za mikoa. Kwa hiyo hili wazo la kwenda kuwapatia hawa uwezeshaji mkubwa wa kuweza kusimamia unaweza ukasaidia kutupunguzia hizi changamoto za upotevu wa fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye TAMISEMI nina jambo la kushauri kutokana na jinsi nilivyouona mpango; itoe maelekezo ya kutosha kwenye halmashauri juu ya namna bora ya kukusanya mapato, lakini pia namna bora wanayoweza kufanya reallocation ya matumizi ya pesa za Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna namna ambavyo wanapanga kwenye bajeti. Bajeti zinapitishwa na halmashauri, zinakuja zinapitishwa hapa Bungeni lakini ikifika wakati halmashauri hizohizo ambazo zimeomba kupitishiwa bajeti hizo, wanaomba kufanya reallocation ya miradi yao, wanapunguza mapato yao waliyowekewa kukusanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hii sera ingeangaliwa vizuri ili hii fursa isitolewe, kwa sababu unapotoa kibali cha kubadilisha bajeti uliyoiomba mwenyewe kwamba utakusanya maana yake unapunguza nguvu ya kukusanya mapato; na unapopunguza nguvu ya kukusanya mapato maana yake unasababisha mapato ya nchi yasiongezeke.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya machache hayo, naomba kuunga mkono hoja.