Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Maimuna Salum Mtanda

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Newala Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii. Awali ya yote namshukuru Mwenyezi Mungu kwa zawadi ya uhai ambayo ametupatia. Lakini kipekee niipongeze Ofisi ya Waziri Mkuu kwa wasilisho zuri la hotuba ambayo ipo mbele yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia niipongeze Serikali ya Chama cha Mapinduzi ambayo imefanya jitihada kubwa, ya kuboresha miundombinu ya usafiri na usafirishaji ambayo ndicho kichocheo kikubwa cha maendeleo ya kiuchumi katika nchi yetu. Wamefanya hivyo, tumeshaona, wote ni mashahidi. Ukienda Mkoa wa Dar es Salaam utakuta Daraja la Tanzanite lakini pia kuna Flyover mbalimbali, na katika maeneo mbalimbali Serikali yetu imejitahidi kuboresha miundombinu ya usafiri na usafirishaji. Sababu ya kufanya hivyo ni kuchochea maendeleo ya wananchi na mtu mmoja mmoja kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia, niende sasa kwenye sekta hiyo ya usafiri na usafirishaji katika Mkoa wetu wa Mtwara. Tuna kilio cha muda mrefu cha barabara ya Mtwara – Nanyamba – Tandahimba – Newala hadi Masasi, kilomita 210. Tunaishukuru Serikali kwamba tarehe 25 Novemba, 2021 ilisaini mkataba wa mkopo wa shilingi bilioni 268 kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika; tunashukuru kwa hilo. Sasa, ni yapi matarajio ya wananchi ambao wameteseka muda mrefu? Wananchi wanatumia gharama kubwa sana za nauli kutoka sehemu moja kwenda sehemu nyingine kwa sababu ya ubovu wa barabara. Kwa hiyo, wanachotarajia wananchi hivi sasa baada ya kusaini mkopo ule ni kuona ujenzi unaanza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wa Kusini wameshaumwa na nyoka na sasa wakiona jani hushtuka, bado hawajaamini kama kweli barabara ile pamoja na kusaini mkopo itajengwa. Hii ni kwa sababu ahadi nyingi zilishapita huko nyuma, tukaelezwa pia na idadi ya wakandarasi, ambao wanakwenda kujenga barabara hizo, lakini ilipita na ahadi hizo ziliyeyuka. Sasa, leo tumeshapata hizo fedha, tunachotarajia sisi wananchi wa Kusini ni kuona kwamba barabara ile ya kiuchumi, ambayo inasafirisha zao la korosho linaloipatia nchi hii fedha nyingi za kigeni; ni barabara hiyo sasa kujengwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kujengwa kwa barabara ile kuna manufaa sana. Kwanza kutachochea maendeleo ya Bandari ya Mtwara ambayo Serikali imewekeza fedha nyingi lakini matumizi yake hadi sasa sio ya kuridhisha. Lakini vilevile kutokana na barabara na Bandari ile maendeleo ya wana Kusini hasa wa maeneo ya Mtwara yatachangamka, kutakuwa na kima mamalishe watapika pale Bandarini na pia wauzaji wa bidhaa mbalimbali nao watauza kwa sababu bandari sasa itakuwa active.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto ya miundombinu ya usafiri katika Mikoa ya Kusini kwa ujumla bado si nzuri, sio nzuri kabisa kiasi kwamba umasikini unazidi kuongezeka kwa wananchi badala ya kutoweka. Sasa hivi barabara ya kutoka Newala kwenda Amkeni – Kitangali – Mtama; barabara ile hata wale waliokuwa wanapeleka mabasi yao hawapeleki tena. Mabasi yanayopita kwenye njia hizo yameharibika, mabasi ni mabovu hayamalizi safari. Kwa hiyo, wananchi wanazidi kudidimia wafanyabiashara hawawezi kupeleka magari yao kwa sababu, wanakwenda kuangamiza hayo magari yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, effect ya hivyo ni kwamba uchumi wa mwananchi mmoja mmoja unazidi kudorora. Niiombe sana Serikali yangu sikivu ya Chama cha Mapinduzi ifanye kweli, miundombinu ile iboreshwe ili uchumi wa wananchi wale nao upate kuchangamka.

Mheshimiwa Naibu Spika, miundombinu ya Mtwara iko mingi lakini hiyo mingi haitekelezeki. Kulikuwa na suala la reli ya kutoka Mtwara kwenda Mbamba Bay, tuliambiwa kwamba mwaka 2019 Juni mkataba ungesainiwa wa ujenzi wa reli ile lakini mpaka leo hakuna kinachoeleweka. Lakini pia, kuna Mtwara Development Corridor, imesemwa sasa hivi imepotea. Haya mambo yakiendelea hivi tunazidi kuwapoteza watu ambao wangezalisha chakula lakini pia tungepata manufaa makubwa sana kama ile miundombinu ya usafiri ingeweza kuboreshwa. Tunazo tani nyingi tu za makaa ya mawe kutoka Mchuchuma ambayo yangepita kwenye reli kwenda kwenye Bandari ya Mtwara. Hii kwa sasa haiwezekani kwa sababu reli hiyo haijajengwa hadi hivi tunavyoongea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la bandari bado ni kizungumkuti. Pamoja na Serikali kuwekeza fedha nyingi, kitu pekee ambacho kilikuwa kinapita kwenye Bandari ile ni korosho peke yake. Sasa korosho ina msimu, si muda wote. Sasa hivi tunamshukuru Dangote kwamba cement yake anataka kupitishia kule. Lakini basi tuchangamshe na hivi vingine ili Bandari ile ilete manufaa ambayo Serikali imeikusudia kwa wananchi wa Mtwara.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili ni kuhusu suala la umeme. Umeme si anasa, umeme ni ulinzi kwa sababu wote tu mashahidi kinachoendelea nchi jirani ya Msumbiji wote tunakifahamu. Lakini wananchi wa Newala, hasa wa Newala vijijini wako gizani. Newala vijijini ina vijiji 107 lakini ni vijiji 33 tu ndivyo vyenye umeme. Vijiji 74 havina umeme. Sasa, vijana wetu wanajiajirije kama hakuna umeme katika maeneo yao? Lakini je, ulinzi na usalama wa wananchi wa Newala ukoje kama wanaishi gizani mpaka leo? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaishukuru Serikali ilituletea mkandarasi tangu Agosti mwaka jana, anaitwa Central Electrical International Limited. Lakini tangu akabidhiwe mradi mwaka jana Agosti, kati ya vijiji 74 ambavyo havina umeme amevipitia mpaka leo hii vijiji 21 tu. Na hivyo 21 si kwamba ameshasimamisha nguzo, bado mpaka leo sasa...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi naunga mkono hoja. (Makofi)