Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Zuena Athumani Bushiri

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi kuchangia hotuba ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Nianze kwa kuipongeza Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi inayoongozwa na Rais wetu Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri sana anazozifanya katika Taifa hili Mungu aendelee kumlinda na kumbariki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze Makamu wa Rais, nimpongeze Waziri Mkuu, Baraza la Mawaziri, Spika na wewe Naibu Spika kwa kazi nzuri mnazozifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya pongezi hizi nianze kuchangia katika Sekta ya Maliasili na Utalii. Nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa jitihada zake za kuitangaza Tanzania kimataifa kupitia programu yake ya Royal Tour nakuiingizia nchi yetu mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mafanikio tunayoyapata, tunapata lakini pia tuna changamoto za wanyamapori. Kumekuwa na malalamiko mengi sana kwa wananchi wanaoishi kwenye mipaka ya hifadhi. Kumekuwa na matukio makubwa mawili ya Tembo kuua wananchi na Tembo kuharibu mazao ya wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mkoa wa Kilimanjaro tunazo wilaya tatu ambazo ni Wilaya ya Rombo, Mwanga na Same ambazo zinaathirika sana na wanyamapori. Katika Wilaya ya Same vijiji vya Mahore, Muheza, Kihurio, Bagamoyo, Kalamba na Kadando vimekuwa vikiathirika sana na wanyamapori hawa kwa kusababisha vifo kwa wananchi pamoja na uharibifu wa mazao yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatoa fidia, fidia inayotolewa na Serikali ni Sh.25,000 endapo mwananchi atakuwa ameharibiwa zao lake kwa hekari moja. Hivi tunavyoongea nimepata malalamiko kutoka kwenye Kijiji cha Mahore, aliyekuwa Diwani wa Kata ya Mahore ametuma meseji kwamba tuombe msaada kwa kuwa askari wa wanyamapori wamezidiwa na tembo na hivyo wananchi wa maeneo hayo wameacha kazi zao na kwenda kulinda tembo ili kuhakikisha kwamba mazao yao yanakuwa. Naomba sana Serikali iangalie suala hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo Serikali inatoa Shilingi Milioni Moja kama kifuta machozi kwa mwananchi ambaye ameuawa na tembo. Kulingana na hali ya maisha ambayo tunayo sasa hivi na kupanda kwa vitu, viwango hivi tukiviiangalia haviendani na hali ya maisha. Baba huyu au Mama huyu ambaye atuuawa na tembo, ameacha familia ambayo yeye ndiye alikuwa akitegemewa kiasi cha Shilingi Milioni Moja hakiwezi kusaidia chochote. Naiomba Serikali yangu sikivu, iangalie kwa makini fidia hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo yote Serikali hii sasa hivi tunayokwenda nayo ya Mama Samia Suluhu Hassan, ni lazima tumpongeze kwa kuwa anajaribu sana kutatua matatizo ya Hifadhi za Wanyama. Tushirikiane Serikali pamoja na wananchi ili tuangalie ni nini ambacho kinaweza kuzuia wale wanyama wasisogee katika makazi ya wananchi ili kulinda mali zao pamoja na uhai wao. Niiombe Serikali kupitia Bunge hili Bajeti ya 2022/2023 iongezwe katika sekta hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya mchango huo naomba sasa niende katika sekta ya barabara. Niendelee kuipongeza Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa kazi nzuri ambayo imefanya, kwa kujenga barabara zetu nchini kote. Niiombe Serikali imalize barabara ambazo zimejengwa vipande vipande ili ziweze kumalizika na wananchi waweze kufaidi katika shughuli zao za ujenzi wa Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee barabara ambayo imejengwa vipande vipande barabara ya Same – Mkomazi. Hivi karibuni Kamati yangu ya Uwekezaji Mitaji ya Umma tukiwa kwenye ziara tulitembelea Hifadhi ya Mkomazi. Katika mojawapo ya mambo ambayo wameomba Serikali iwasaidie ni barabara ya Mkomazi - Same. Wamedai barabara ile ni fupi kwa wale ambao wanatokea Tanga na Dar es Salaam wanaifahamu, lakini wamesema watalii wengi wanaotokea Dar es Salaam na Tanga wanapenda barabara ile kwa kuwa ni fupi, lakini barabara ile imejengwa vipande kwa vipande, imeanza Kiurio kipande, ikaachwa Ndungu kipande, Maore kipande, Kisiwani kipande.

Mheshimiwa NaibU Spika, hivyo wanaiomba Serikali Hifadhi ya Mkomazi Game Reserve imetuma Kamati ya PIC, Mwenyekiti wangu yupo pale atathibitisha kauli hiyo. Tuiombe Serikali ili watalii wale waweze kupita njia iliyo rahisi kufika katika hifadhi na barabara ile ikiboreshwa kwa madai yao watalii wetu watapata urahisi wa kufika katika hifadhi vizuri na kwa usalama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi niendelee kuipongeza Serikali kwa kazi nzuri sana inazofanya na niendelee kuiomba Serikali iangalie yale matatizo ambayo yanawagusa sana wananchi wa Tanzania, kama vifo na kuharibiwa mali zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, ninaunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)