Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia hotuba hii ya Waziri Mkuu mchana huu wa leo.

Naomba nianze tofauti kidogo na mwaka jana wakati nachangia hotuba hii. Mwaka jana nilisema Halmashauri ya Wilaya ya Liwale ina miaka 41 lakini haikuwa na jengo hata moja lenye hadhi ya kuitwa Wilaya. Hata hivyo, leo nasimama hapa kwanza namshukuru sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana sana sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuwa Rais msikivu. Lakini vile vile namshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu, kwakweli hotuba yangu aliitendea haki mwaka jana. Leo nasimama hapa tayari tumeshapokea fedha zaidi ya bilioni moja kwaajili ya kujenga jengo la Halmashauri, tumepokea milioni 500 tunajenga jengo la mkuu wa wilaya, tumepokea milioni 450 tumeanza ujenzi wa mahakama ya wilaya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili ni jambo la kushukuru sana. Tangu tumepata uhuru hatujawahi kupata miradi mingi kwenye Halamshauri ya Wilaya ya Liwale kama tulivyopata mwaka huu. Mnyonge mnyongeni lakini haki yake mpeni, nasema ahsante sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vilevile naomba nijielekeze kwenye mchango wangu kwenye kuboresha baadhi ya mambo machache yaliyojiri kwenye hotuba hii nzuri ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Mimi nianze kuzungumzia upande wa ajira. Kwanza nimshukuru Mheshimiwa Rais, kwa kuonesha nia na kudhamiria kuajiri watumishi wengi zaidi kwenye Wizara yetu ya Afya pamoja na Wizara ya Elimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa mchango wangu ni kwamba; ninaomba Serikali izingatie ajira hizi kulingana na jiografia za mahali Halmashauri hizi zilipo. Mimi kule kwangu watu wanakuja kuchukua cheque number tu. Watumishi wengi wanaoajiriwa kuja Liwale wanakuja kwa ajili ya kuchukua cheque number tu. Mwaka juzi nilipata watumishi 81 kwenye kada ya afya, lakini kila tukikaa Kamati ya Mipango na Fedha, watumishi 10 hadi 20 wanahama. Kila mwezi 10 hadi 15 wanahama, kiasi kwamba mpaka leo hii nimerudi kule kule kwenye uhaba wa watumishi. Lakini wakati ule inaajiri kuna vijana walioko kule Liwale wanajitolea kwenye shule zetu na kwenye vituo vyetu vya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwongozo ulisema kwamba wanapoomba ajira basi waende kwa Mkurugenzi waambatishe na CV; yaani Mkurugenzi aandike kuonesha kwamba hawa vijana wamejitolea kwa muda ili waweze kupewa vipaumbele, lakini jambo hili halijawahi kufanyika. Ninao vijana pale wana miaka mitano wengine miaka sita wanajitolea wanataka kufundisha, wanafundisha shule kule lakini walimu wanaokuja kutoka nje wanakuja kuchukua cheque number na wanaondoka. Naomba jambo hili lizingatiwe kwenye suala la ajira ya vijana.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vilevile, kwenye hiyo hiyo ajira wako watu waliomaliza mafunzo, yaani kwenye vyuo vya elimu pamoja na vyuo vya afya kwa mwaka 2019 au 2018 au 2016 lakini wanaajiriwa wengine wa mwaka 2019, 2018 na kwamba waliomaliza mwaka 2016 au 2015 bado hawajapata ajira. Jambo hili nalo liangaliwe. Kwanza wenyewe watakosa umri wa kuajiriwa. Maana kama umemaliza chuo mwaka 2014 leo hii 2022 tayari wanaoomba kuajiriwa utakuta umri umempita. Kwahiyo tutakapoajiri jambo hili mimi ningeomba lizingatiwe sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikitoka huko nielekee kwenye wananyamapori. Suala la wanyamapori hasa kwa sisi wenye halmashauri ambazo tunaishi karibu na hifadhi suala la wanyamapori limekuwa ni kero kubwa sana, hasa kwa upande wa madhara wanayapata wakulima kwa mazao yao kuliwa na wanyamapori. Ipo sera inasema wanapata fidia, lakini fidia zenyewe zinakuwa ni kidogo halafu zinakuja kwa kuchelewa. Ombi langu kwenye upande huu wa wanyamapori, Serikali sasa ione namna ya kuweka askari wa wanyamapori kwenye hizi kata ambazo ziko karibu na hifadhi ili waweze kupata ulinzi. Kata zenyewe ziko mbali, unaweza kukuta kata labda iko kilomita 70 au kilomita 100 kutoka Halmashauri ya Wilaya. Sasa ukitoa taarifa, mpaka anapokuja askari tayari kwenye vijiji vile watu washapata madhara yakutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ombi langu hapa, Serikali ione namna, ikiwezekana tuanze kuajiri polisi kata; yaani wale askari wa wanyamapori wa kata kama ilivyo kwa polisi kata ili tuweze kusaidiana kukabiliana na tatizo hili la wanyamapori kwenye hizi kata ambazo ziko kwenye mipaka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba nijielekeze kwenye suala la lishe. Pamezungumzwa kwenye lishe; mimi naomba nitoe ushauri, kwa sababu mimi mwenyewe ni mtaalam wa mambo ya usindikaji wa nafaka. Tanzania tuna tatizo kubwa sana kwenye usindikaji wa nafaka. Sisi kitaalam nafaka inasindikwa tuna-extract unga kwa asilimia 85. Lakini kwa utaratibu wa Kitanzania, ili uweze kukoboa watu wanakoboa mahindi mpaka asilimia 60. Kwa hiyo zaidi ya asilimia 40 ya nafaka tunapoteza. Na hii ni kutokana na kwamba sera haijawekwa, vizuri sijui wapo TBS sijui ni TFDA wale ambo sasa hivi wamebadilisha sijui wanaitwa nini sijajua vizuri. Sera zao hazieleweki, hawatoi mwongozo; kwamba ili mtu upate unga kutoka kwenye nafaka inakobolewa kwa asilimia ngapi ili unga uwe na ubora. Sasa hivi mnalisha watu pamba tu, kwa sababu kama mahindi au nafaka yote umeikoboa kwa asilimia 60 unabakiza nini? Tunashindana hata na panya; panya kwenye mahindi anakula kiini kile na lile ganda lote analiacha na sisi ndio tunaneemeka nalo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ipo haja ya kubadirisha sera yetu ya ulaji. Lazima TFDA itoe mwongozo; kwamba kila aina fulani ya chakula, ili ukipate kwenye uhalisia wake kinatakiwa kiwe processed kwa namna gani.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe mfano, Mikoa ya Njombe, Iringa na Ruvuma ni wakulima wazuri sana wa mahindi lakini ndiyo mikoa inayoongoza kwa utapiamlo; unauliza watu wanapataje utapiamlo ilhali wanakula asubuhi, mchana na jioni? Tena unakuta vitumbo vimepanda kwa ajili ya sembe. Lakini wamekula pamba, hawajala chakula kinachotakiwa. Kwa hiyo ni lazima twende na wakati huo huo tuone namna ya kufika hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine; kulikuwa na miradi ilianzishwa kwenye nchi hii, kwamba kila halmashauri ilitakiwa ilete miradi ya kimkakati. Lengo la miradi ile lilikuwa ni kuongeza mapato kwenye halmashauri zetu. Baada ya mapato mengi ya halmashauri kuletwa Serikali Kuu wakasema sasa halmashauri nendeni mkatengeneze mkakati wa kubuni miradi, na watu wakabuni miradi. Kuna watu walibuni masoko, stendi; na sisi kwenye Halmashauri yetu ya Wilaya ya Liwale tulibuni stendi, tukaletewa fedha lakini fedha zile kutokana na zile sheria zetu za manunuzi ambazo zinachelewa fedha zikaondoka, mpaka leo mradi ule umekufa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ile sera ya kuitaka halmashauri ije na miradi ya kimkakati imekufa? Maana tangu fedha zile zimeondoka huu ni mwaka wa tatu, hazitarajiwi kurudi. Lakini vilevile tulikuwa na mradi mwingine, mradi wa soko, hatuelewi uko wapi?

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa mimi naiomba sana Serikali, kama kweli tunataka kuendeleza halmashauri zetu na kukuza vipato kwenye halmashauri zetu basi hii miradi ya kimkakati ipewe kipaumbele. Kama miradi iliyochukuliwa fedha zake basi fedha hizo zirudi, na kama hii miradi mingine mipya ianze ili kweli halmashauri zetu zipate mapato ambayo yanaweza kuhudumia jamii zetu mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine naomba nijielekeze kwenye upande wa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Jambo lingine muda wako umekwisha.

MHE.ZUBERI M. KUCHAUKA: Muda umeisha!

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)