Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Michael Constantino Mwakamo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibaha Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi na mimi ya kuchangia kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Kwanza naipongeza Serikali kwa namna ambavyo inatekeleza majukumu yake na namna ambavyo inahudumia wananchi kwenye maeneo mbalimbali kwa kipindi kizima hiki cha mwaka ambao tunaumaliza sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka jana nilisimama kwenye eneo hili, nilitoa shukrani na nilitoa tamko la kuomba eneo kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu, na tulipatiwa pale eneo la hekari 4,000 na hadi sasa hekari 2,500 zimeshapata wawekezaji na kazi inaendelea. Kwa hiyo nawapongeza sana Serikali kwa kutuletea wawekezaji hawa na kuanza kufanya uwekezaji katika maeneo ambayo yapo kwenye Jimbo langu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na mambo mazuri yote haya ambayo nayaeleza, ninalo ombi dogo ambalo ningependa nilitangulize kabla sijatoa mchango wangu kwenye maeneo ambayo nimejipanga kuyazungumza; kwamba wananchi wa Jimbo la Kibaha Vijijini na hususani kwenye maeneo ya majimbo ya karibu wanaishukuru sana Serikali, hasa Mheshimiwa Rais kwa kufanya ziara maeneo mbalimbali katika maeneo ya jirani na Mkoa wa Pwani na kushiriki nao katika shughuli mbalimbali za kimaendeleo. Lakini kuna ombi moja kubwa sana, na nitumie nafasi hii niliwasilishe ombi hili ili Serikali isikie. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wa Jimbo langu wanamuomba sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muunguano wa Tanzania afike pale Mlandizi azungumze nao, kwa sababu aliwaahidi kuwa atafika wakati ule wa kampeni. Kwa hiyo natumia hadhara hii leo kumuomba akumbuke ahadi ile, afike, afanya mazungumzo nao ili awasikilize wananchi moja kwa moja pamoja na mimi Mbunge wao ninayewazungumzia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini baada ya ombi hilo leo nataka kujielekeza kuzungumzia sekta ya uzalishaji, hasa kwenye habari hii ya kilimo. Wabunge wengi tumezungumza habari ya kilimo, tumeiona kwenye bajeti kwenye hotuba hii ambayo Mheshimiwa Waziri Mkuu amewasilisha. Ametambua kwamba sekta ya kilimo uzalishaji ina takriban asilimi 65 ya wananchi wa Tanzania ambao wanafanya shughuli za kilimo. Hata hivyo, zipo changamoto ambazo pia zimeelezwa, lakini vile vile na mafanikio makubwa ambayo yameelezwa kwenye sehemu hii. Mimi nataka nizungumzie maeneo machache makubwa, hasa yale ambayo mimi nimeyaishi kama mtoto wa mkulima katika maeneo, ambayo waliomo humu wengi naamini nao wameyaishi kama watoto wa wakulima.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakulima wengi katika nchi hii ni wakulima wa ngazi ya chini sana. Ni wazee wetu ambao wanalima kwa kutumia jembe la mkono, ndio wazee hawa ambao wao tunapozungumzia masuala ya upatikanaji wa mbegu ni wale ambao wanavuna mazao yao, wanahifadhi kwenye maghala ya asili na mwaka mwingine unapokuja wanakwenda kupanda tena. Sasa tumezungumza hapa na tunaona mipango ya Serikari, wanajaribu kuzungumzia upatikanaji wa pembejeo za kilimo, na naona kazi kubwa inayofanywa na Waziri wa Kilimo juu ya kukisimamia kilimo katika nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi niombe Serikali; kwamba tunapotazama ukubwa wa kukikuza kilimo tusisahau hili kundi kubwa la wakulima ambao wanaishi vijijini, na ndio hawa ambao wanalea familia kwa kutumia nguvu zao kwa kulima kwa jembe la mkono. Ndio hawa ambao wanalima na wanahakikisha watoto wao katika maeneo ya vijiji wanakwenda shule. Lakini wanapata changamoto mbalimbali ikiwemo suala la kutumia mabonde yaliyopo ambako bodi za mabonde wanawawekea mazingira magumu ya kufanya shughuli zao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitatoa mfano mmoja mdogo sana. Kwenye Jimbo la Kibaha Vijijini wengi wakuliwa wanalima kwenye bonde la Mto Ruvu. Mwaka jana tunakumbuka, na si mwaka jana tu, tulipata tatizo kubwa la mto ule kupungua maji. Baada ya kutokea tatizo lile kukatokea saka saka kubwa sana ya kukamata wakulima ambao wanalima pembeni mwa lile bonde. Sasa mimi ningeomba Serikali, pamoja na kwamba vyombo vyote hivi vinafanya kazi ya kuwahudumia wananchi, lakini ijaribu kuangalia namna ambavyo watawaelekeza, kwamba ni namna gani wayatumie yale maji ili nao waweze kufanya maisha yao yaendelee. Kwa sababu unavyokwenda kumzuia asifanye shughuli ile, unapokamata mashine zake anazotumia kumwagilia tunasahau kwamba mkulima huyo hana njia nyingine anayoweza kuitumia ili kuishi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ingekuwa vizuri sana kama ungewekwa utaratibu mzuri wa kuelekezwa namna gani bora wanaweza kuyatumia maeneo yale ili waweze kuendelea kuendesha kilimo chao.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tumeona Serikali imewekeza nguvu kubwa sana kwa hawa maafisa ugani. Lakini maafisa ugani ambao wamewapatia uwezo huu wa kuwahudumia wananchi, wanahudumia wananchi wengi ambao ndio wale ninaowazungumzia, wakulima wadogo; wakulima ambao Serikali imewazungumzia, ukitazama kwenye mipango mingi mikubwa sana inayoendelea hapa. Tunazungumza benki ambazo zinatakiwa ziwakopeshe wakulima. Sasa, tujiulize, ni kwa kiasi gani benki hizi zimewafikia hawa wakulima wadogo? Ni kwa kiasi gani wakulima wadogo hawa wanafaidika na hii mipango mikubwa ya Serikali? Tukifanya hivi na tukihakikisha Serikali inaelekeza nguvu kule, ndivyo tutakavyokuwa tumesaidia kundi kubwa la wananchi ambao watahudumiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo nataka nilizungumzie hapa ni eneo la mawasiliano. Tumeona kwenye hotuba, ni namna gani Serikali inaongeza kilomita nyingi za kuhudumia Mkongo wa Taifa. Hata hivyo, mawasiliano vijijini bado ni tatizo kubwa sana. Kwa mfano ukienda kwenye jimbo langu tu kuna Vijiji vya Milalazi, Kimalamisale pamoja na Magindu wanapata mawasiliano kwa shida sana. Na hili nimetaja hapa kama sehemu ya mifano, lakini vijiji vingi nchini vina shida ya mawasiliano. Kwa hiyo, ni vizuri tunapozungumzia suala la mawasiliano tujielekeze katika kupeleka mawasiliano haya vijijini, kwa sababu tunaona kila Wizara kila Idara inayozungumza maendeleo inahusisha maendeleo na masuala ya mawasiliano. sasa kama vijijini kutakosa mawasiliano mazuri yenye uhakika, watu hawa tutawatoaje kwenye mazingira hayo ya mawasiliano? Kwa hiyo ningeomba tuone namna bora ya kushughulika na jambo la mawasiliano. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo nataka nizungumzie ni kuhusu Mkoa wa Pwani. Mkoa wa Pwani una mkakati mkubwa sana wa kimaendeleo; nilizungumza mwaka jana na ninalirudia tena, na ninafahamu kwamba Serikali ina mipango mikubwa ya juu ya kuendeleza maeneo mbalimbali nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika eneo la Mkoa wa Pwani tunalo eneo la Bagamoyo; eneo ambalo lina mkakati mkubwa sana. Tunasikia kwamba kuna mikakati mikubwa ya kuimarisha bandari ile. Ningeomba zifanyike jitihada kubwa sana, yatoke maelekezo ya wazi ya namna gani bandari ile ianze kushughulikiwa ili iweze kubeba mzigo mkubwa wa uzalishaji unaofanyika kwenye viwanda vya Mkoa wa Pwani pamoja na kuwa njia ya kupitisha mizigo inayoelekea maeneo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na tutapoimarisha bandari ile naamini kabisa tutaimarisha barabara inayozungumzwa siku zote, ile inayokatiza Mlandizi kuelekea Nzenga na kwingineko.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa machache haya naomba niunge mkono hoja na mengine nitachangia kwenye Wizara zinazohusika. Ahsante. (Makofi)