Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS (MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA): Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nami nachukua fursa hii kwanza kabisa kuunga mkono hoja hii ya hotuba ya bajeti ya Wizara ya Afya, lakini nachukua fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Afya na Naibu wake pamoja na uongozi mzima wa Wizara kwa kazi kubwa na nzuri ambayo anaifanya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesimama tu hapa kutoa assurance, nimesikia katika michango mingi, kwa kweli kwa kiasi kikubwa Waheshimiwa Wabunge wameongelea sana tatizo la uhaba wa watumishi katika Sekta hii ya Afya. Napenda tu kusema na kurudia kwamba katika mwaka huu wa fedha unaomalizika 2015/2016, katika Sekta ya Afya wataajiriwa wataalam 10,870. Muda wowote kuanzia sasa ndani ya mwezi huu kibali cha ajira kitaweza kutoka na Wizara ya Afya wataweza kuendelea kuwapangia vituo vya kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mgao huo wa watumishi 10,870, watumishi 3,147 ni wa kada mbalimbali 10 zinazohusiana na masuala mbalimbali ya utabibu. Vilevile ukiangalia katika wauguzi, ni wauguzi 3,985. Pia ziko kada nyingine kama za mama cheza au wataalam wa viungo pamoja na Wafamasia na wengineo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia katika miaka mitano tu, kuonesha ni kwa namna gani Serikali imekuwa ikitoa kipaumbele katika upatikanaji wa wataalam wa afya, kwa upande wa utumishi, tumetoa vibali 52,937 na kati ya vibali hivyo walioweza kuajiriwa ni wataalam 38,087 na ambao hawakuweza kuripoti ni 14,860. Asilimia 71.93 ndiyo ambao waliweza kuripoti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini? inawezekana mkaona siyo jambo la kweli; ukiangalia katika sekta binafsi katika ushindani na wenyewe pia wanang‟ang‟ania wataalam hao hao, lakini mwisho wa siku ukiangalia pia katika vyuo vyetu vya umma pamoja na vyuo binafsi mahitaji yanayohitajika pamoja na output inayotolewa bado haitoshelezi. Kwa hiyo, kwa kushirikiana na Wizara ya Afya tuwe katika mkakati wa kuangalia ni kwa namna gani sasa katika vyuo vyetu wataweza kutoka wataalam wengi zaidi ili waweze kuajiriwa na kufanya kazi katika taasisi mbalimbali za afya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano mwaka jana tu, mwaka 2014/2015 pamoja na kwamba ikama zimejazwa na Halmashauri zetu. Ziko kada zaidi ya 12 zenye wataalam 335 hawakuweza hata kupata watu kabisa, ukiangalia ni kada ambazo hata mafunzo yake hapa nchini hayatolewi. Nitolee tu mfano biomedical engineers pamoja na wengine wengi, tunaelewa umuhimu na tunaendelea kujitahidi kuongeza idadi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile ukiangalia 2014/2015 tulitoa kibali cha watumishi 8,345 lakini mwisho wa siku ukiangalia katika soko la ajira kulikuwa na ukosefu wa wataalam katika soko la ajira 4,467, tungependa kuweka idadi kubwa na hata hii idadi yenyewe tunayowaambia ya 10,870 tunaangalia kwa mujibu wa wahitimu wanaotoka katika kila mwaka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia wahitimu waliopo katika mwaka 2015/2016 ni wataalam 10,000 na sisi tunatoa kibali cha 10,870. Kwa hiyo, niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba, tunaona umuhimu wa sekta hii na tutaendelea kwa karibu kabisa kama Serikali na kwa kushirikiana na Wizara ya Afya kuona ni kwa namna gani sasa idadi hii itaweza kuongezeka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia katika mwaka 2010/2011 tulianza na wataalam 7,903, lakini ukiangalia katika mwaka huu wa fedha tutakwenda katika wataalam 10,870. Kwa hiyo itoshe, tu kusema kwamba, kama Serikali tutaangalia katika namna ambavyo wanapangwa sasa. Tutazingatia yale maeneo ambayo yana upungufu mkubwa uliokithiri wa wataalam, vilevile kuangalia sasa ni kwa namna gani tunaweza kuhuisha mfumo wetu katika mchakato wa ajira au upangaji wa vituo, uweze kuwa ni centrally katika sehemu moja ili kuona ni kwa namna gani sasa katika vituo vyetu tunaweza kupata wataalam wa kujitosheleza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niliona niseme hayo, niwahakikishie sana Waheshimiwa Wabunge kila mwaka kwa kadri bajeti itakavyokuwa ikiruhusu, tutakuwa tukijitahidi, sekta hii ni sekta ya pili ambayo tunaipa kipaumbele. Katika Sekta ya Elimu wataalam 20,857 na katika Sekta hii ya Afya wataalam 10,870 lakini bado tunazingatia kwamba ni muhimu vyuo vyetu viweze kuwa na output zaidi ili tuweze kupata wataalam wa kuweza kuwaajiri.