Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Dr. Jasson Samson Rweikiza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukoba Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. DKT. JASSON S. RWEIKIZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kunipa nafasi nami nichangie katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Niseme kabisa kwamba, hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu imetuwekea misingi mizuri ya kupanua uchumi wetu na kuukuza kama nchi.

Mheshimiwa Naibu Sika, tunapozungumzia bajeti, tuko humu kwenye Bunge la Bajeti, tunazungumzia uchumi na uchumi imara ndiyo Taifa imara.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hapa nimshukuru Mheshimiwa Rais Samia kwa kuweka nguvu nyingi katika kukuza uchumi wetu. Nataka kuzungumzia suala la kilimo na majuzi hapa tumeona Mheshimiwa Samia, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pale kwenye mkutano uliofanyika katika Ukumbi wa Jakaya Kikwete kazi aliyoifanya ni kubwa sana ya kuboresha kilimo chetu. Nampongeza na kumshukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo nataka nizungumzie suala mahsusi kuhusu kilimo. Kilimo tunasema ndio uti wa mgongo na kwa kweli ndio ukweli wenyewe, bado uchumi wetu mkubwa unategemea kilimo. Tuna maeneo nchi hii ambayo ni mazuri yana rutuba sana, wote mnayafahamu maeneo mbalimbali ukienda Morogoro Mkoa mzima una rutuba kubwa sana, ukienda maeneo ya Kusini kule Tunduru, ukienda Katavi, ukienda Rukwa, ukienda Kigoma, maeneo mbalimbali yote Kahama, kule wapi, kuna rutuba nyingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nchi hii tumejaliwa tuna mito mingi. Licha ya mvua tuliyonayo ya kutosha kumwagilia mashamba yetu vilevile kama kuna shida ya mashaka ya mvua tuna mito kwa hiyo, tuna uwezo wa kulima kwa kutegemea umwagiliaji ambao sio wa gharama kubwa kwa sababu ya mito. Tuna mito kama Mto Mara, umeongelewa juzi hapa, tuna Mto Kagera, tuna Mto Pangani, tuna Mto Malagarasi, tuna Mto Ruvu, tuna Mto Ruvuma, kila mahali kuna mito mingi sana hiyo ni mikubwa. Iko mito midogo ambayo inaingia kwenye mito hiyo inapita maeneo ambayo nimeyataja yale ya ardhi ambayo ina rutuba.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ninapozungumzia kilimo leo nataka nizungumzie maeneo haya. Kabla sijaenda kwenye maeneo hayo niseme kwamba, tuna vijana wengi nchi hii ambao hawana kazi, lazima niseme wazi. Hawana ajira, hawana kazi wanayoifanya, hawana biashara wapo tu, wengi sana. Ukienda Dar-es-Salaam ndio kabisa, ukienda pale Mwenge, ukienda Manzese, Tandika, Buguruni, Miji yote ukienda Mwanza, ukienda Arusha, wako vijana wanauza pipi, wanauza vitambaa vya jasho, siku hizi charger ndio zimekuwa deal ya kuuza charger kama vile zina uadimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hawa vijana wana nguvu, miaka 25 miaka 20 hawana ajira, lakini mimi nasema tuna ardhi nzuri sana maeneo mengi ya nchi hii. Nchi hii ina hekta karibu Milioni Moja haijalimwa zaidi ya nusu haijaguswa, sasa nikasema vijana tulionao nguvu kazi hii kubwa ambayo haitumiki, siyo tu kwamba tunapata hasara kutokutumia vijana hawa, vilevile ni hatari kubwa ambayo tumeiangalia, tunakaanayo hatuitumii ipasavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nataka nipendekeze hapa jambo mahsusi. Nataka nipendekeze na Serikali naomba jambo hili ilichukue tuanze kilimo cha makambi. Peleka vijana kwa mfano 200 kwa mfano kwenye kambi moja, tafuta eneo pale na mchango wangu huu unahusu Wizara nyingi sio huyu wa kilimo peke yake, Wizara nyingi zaidi ya kumi, iundwe task force ya Wizara zaidi ya kumi jambo hili lipewe kipaumbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, peleka vijana kwa mfano 200 nimesema kwenye kambi moja, wape mkopo, Serikali itafute fedha iwape mikopo ili wanapokwenda pale vijana 200, maana yake ni mbugani, porini, hakuna nyumba, wajenge nyumba za full suit za kuanzia, juu bati chini bati. Wapate tractor, ukitumia jembe la mkono unajidanganya haina tija na ni mateso, wapate ma-tractor angalao mawili, power tiller angalao mbili, wapate mbolea, wapate mbegu, wapate pembejeo mbalimbali. Chakula cha kuanzia angalao miezi sita, wanunue chakula na mahitaji mengine waanze pale.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimefanya hesabu hapa za kirejareja, ukipeleka vijana 200 kwenye kambi ukawapa eka 2,000, ukawapa Milioni 200 kama mkopo wakaanza kulima kwa tractor ndani ya muda mfupi utapata mazao mengi sana na pesa nyingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema nimefanya mahesabu ya kukadiria hao watakaoundwa, kama itakuwa imeundwa hiyo KAMATI itafanya hesabu za uhakika, lakini ukiwapa vijana eka 2,000 vijana 200 wakaanza kulima kwa utaratibu watakaokubaliana wa kambi, wakaanza na mazao ya muda, maharage, mahindi, alizeti, ufuta, mpunga na mazao mengine ndani ya miezi mitatu, miezi minne, wataweza kuvuna mazao mengi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, wakilima mahindi wakapata eka moja magunia 20 kwa kiwango cha chini, ndani ya miezi mitatu wamevuna mahindi ya kutosha kuuza kupata fedha ya kutosha. Ndani ya mwaka mmoja wakilima misimu miwili, misimu mitatu, kama wanamwagilia maji watalipa lile deni, wataanza kujiendeleza. Pale palipokuwa kambi ya muda ya mabati ya full suit watajenga nyumba za kudumu, watajenga shule, zahanati, wataweka mitaa na maendeleo mengine, tutaongeza ajira, vijana hawa ambao wako Mijini wanazurura tutakuwa tumewaondoa tumeleta maendeleo makubwa, tutauza chakula hiki nchi za nje. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tutauza Uarabuni ambao hawalimi lakini wanakula vizuri. Tutauza Congo, tutauza hapa Kaskazini kote kuna shida ya kilimo tutapata fedha nyingi na vijana hawa tutakuwa tumewaondoa kwenye balaa ya kukosa ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi kwangu Jimboni pale kuna vijana wanaendesha pikipiki bodaboda hizi wako nchi nzima. Kule vijijini unakuta kituo kidogo kina bodaboda 40, wanafanya kazi gani?

Mheshimiwa Naibu Spika, anakaa mpaka jioni hata abiria mmoja hampati anaondoka hana kipato. Wakiwa kwenye kambi ya kilimo hii baada ya mwaka mmoja wataweza kupata pesa hata kujilipa mshahara wa Shilingi Milioni Moja kwa mwezi, watajilipa watakuwa wamejiendeleza na watapata ufanisi mkubwa sana na nchi itapata chakula cha kutosha itaweza kuuza chakula hiki nje na kuboresha maisha ya Watanzania na kuboresha uchumi wa nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mchango wangu mimi ni huo kwamba, tufanye kilimo cha makambi ambacho kitaondoa baa la vijana kutokuwa na kazi, baa la kukosa chakula, amesema Mheshimiwa Mbunge hapa tunahangaika na mafuta, tukilima alizeti shida hii itakuwa imekwisha kwa wingi na tutapata mazao mengi sana. Nchi itaneemeka, hiyo mikopo italipwa na vijana itarudishwa Serikalini na tutakuwa tumepiga hatua ya maendeleo nzuri sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)