Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Naibu Spika, nishukuru sana kupata nafasi hii. Kwanza, niipongeze Serikali kwa jitihada kubwa ambazo zinafanywa na Serikali yetu kwa kupeleka huduma muhimu za elimu, afya na maji na miundombinu kwa ujumla. Nataka nijikite kwenye eneo la Mradi wa Bandari ambao umewekezwa kwenye Wilaya ya Tanganyika, Mradi wa Bandari ya Kalema. Serikali imejenga Mradi wa Bandari ambao ni mkubwa na kimsingi tunayo fursa kubwa sana ambayo Serikali inaweza ikaipata pale ambapo tutafanya maboresho makubwa. Nchi ya DRC Kongo imejiunga na Umoja wa Afrika Mashariki, malengo ni kutaka kuitumia fursa ya soko la Afrika Mashariki. Sasa sisi kama Nchi ni vyema tukawa na uwekezaji mkubwa ili fursa iliyopo sasa, iweze kuwanufaisha wananchi wa Tanzania kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa ile bandari hautakuwa na faida kama hatutakuwa na uwekezaji mkubwa na fursa ile itatumiwa na nchi jirani ambao wataichukua kama fursa muhimu. Niiombe sana Serikali ujenzi wa Bandari ya Kalema uende sambamba na uwekezaji wa ujenzi wa reli na uimarishaji wa reli ya kutoka Kaliua, Mpanda hadi Kalema. Sambamba na hilo ni lazima kuwe na mpango mkakati wa ujenzi wa barabara ya Kabungu hadi Kalema. Kwani, ile bandari itakapokuwa imekamilika kama hakutakuwa na miundombinu shirikishi ujenzi ule utakuwa hauna maana yoyote. Kwa hiyo, naomba na naishauri Serikali tuwekeze mradi ule uwe na matawi yake ya ujenzi wa reli na ujenzi wa barabara. Ni muhimu sana katika kuimarisha ushirikiano wa East Africa tufanye mipango na mikakati ambayo Serikali itaisimamia kuhakikisha Nchi ya Congo inatumia Bandari ile ya Kalema. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Kongo ni Nchi kubwa na ina madini na ina mzigo mkubwa sana ambao tukiutumia kwa Bandari ya Kalema na Bandari ya Kigoma tutakuwa na fursa kubwa sana ya Bandari ya Dar es Salaam ikapata mzigo wa maana.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ni suala la kilimo. Nchi yoyote ile inaendelea kwa kuwekeza kwenye kilimo, bila uwekezaji mkubwa wa Serikali kwenye kilimo hatutafanya kitu chochote cha maana. Naomba sana lazima Serikali ije na mpango mkakati wa uwekezaji kwenye kilimo cha umwagiliaji. Kilimo cha umwagiliaji kitawasaidia watanzania wote na kitaimarisha uchumi kwa nchi yetu. Niiombe sana Serikali iwekeze kwenye kilimo cha kisasa tuwe na mabadiliko ambayo, yataanza kuepuka sasa kilimo cha kutegemea jembe la mkono. Sambamba na hilo ni muhimu kwa Serikali kuwekeza kwenye mbegu, tuwekeze kwa wataalam, lakini kubwa zaidi ni kuimarisha Vyama vya Ushirika. Kwenye Vyama vya Ushirika ndivyo vinavyoweza kumkomboa mkulima mdogo mdogo ambaye anaweza sasa kuwa kiunganishi na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunahitaji Serikali iangalie umuhimu wa kusogeza huduma za pembejeo. Bei za pembejeo ni kubwa sana kiasi kwamba Watanzania wanashindwa kumudu hizo bei. Niombe Serikali yetu iimarishe Mfumo wa kuleta pembejeo na kujenga viwanda vya pembejeo ambavyo vitasaidia kupunguza gharama. Sambamba na hilo ni kuimarisha masoko, mazao mengi ambayo yanalimwa masoko yake ni ya shida. Tutoe ukiritimba wa Serikali ambao mkulima akilima kwa jasho lake, wakati fulani huwa anaanza kupangiwa bei na kuzuiliwa mazao yake kutokupelekwa nje ya nchi. Hili tunaomba Serikali ilifanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna ushauri kwa Serikali kwenye eneo la uvunaji wa hewa ya ukaa. Nchi yetu ina misitu mingi ambayo haijatumika vizuri, wenzetu wa nchi zingine wanatumia fursa ambayo ipo kwenye maeneo yao. Serikali ni vyema sasa ikaangalia Mfumo wa uwekezaji na kuwasogeza wawekezaji wanaokuja kuwekeza kwenye uvunaji wa hewa ya ukaa. Mataifa mengi duniani yanaharibu mazingira sisi tuna misitu ambayo inamilikiwa na Serikali za vijiji, tuna misitu ambayo inamilikiwa na Halmashauri na misitu inayomilikiwa na Serikali Kuu. Katika maeneo haya ni vyema Waziri mwenye dhamana, akaja na mpango wa kubadili Sheria itakayonufaisha maeneo hayo yote yaweze kuvuna hewa ya ukaa. Kuna fedha nyingi sana ambazo tunazipoteza kama Taifa, eneo ambalo tuna Hifadhi za Serikali hawaruhusiwi kuvuna hewa ya ukaa. Sasa tukija na mabadiliko ya Sheria yatasaidia katika maeneo yote yaweze kuvuna hewa ya ukaa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kwenye eneo hili ninaiomba Wizara ya Maliasili, mgogoro uliopo Wilaya ya Tanganyika kati ya TAWA na Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika waushughulikie ili wananchi waweze kunufaika kwani tayari tulishafanya mpango mkakati ambao utawawezesha wananchi kupitia Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika wapate fedha karibu zaidi ya Shilingi Bilioni Tano ambazo zitawanufaisha kwenye huduma zile za kimsingi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho nizungumzie suala la barabara. Barabara inayotoka Mpanda kwenda Uvinza inayounganisha Mkoa wa Katavi na Mkoa wa Kigoma, tunaomba Serikali iishughulikie na kuijenga ili iweze kuwa kiunganishi kwani ni barabara ambayo inaunganisha nchi na nchi, lakini kwenye maeneo haya tutakapokuwa tumejenga hii barabara Watanzania na nchi jirani watanufaika kwa sababu, miundombinu ndiyo inayoleta mazingira mazuri ya kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaiomba na kuishauri Serikali mradi wetu wa maji wa Mkoa wa Katavi kutoa maji Ziwa Tanganyika kuja Makao Makuu ya Mkoa wa Katavi, tunaomba sana mradi huu ufanyiwe kazi ndani ya kipindi hiki kwani miradi mingi midogomidogo imekuwa haina tija na kwenye Mikoa ya Kigoma, Rukwa na Katavi ndiyo mikoa ambayo haijanufaika, wanayaangalia maji ambayo yapo kwenye Ziwa Tanganyika bila kunufaika nayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)