Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Daniel Baran Sillo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. DANIEL B. SILLO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwanza nichukue nafasi hii kukushukuru wewe binafsi kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kuchangia katika hotuba hii ya Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa anayoifanyia taifa letu, na sisi Waheshimiwa Wabunge ni mashahidi, kwamba kuna kazi kubwa imefanyika katika majimbo yetu kwenye miradi mbalimbali ya maji, afya nakadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze Mheshimiwa Makamu wa Rais lakini ikitokea pia nimpongeze Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa anayofanya ya kusimamia miradi mbalimbali ya Serikali pamoja na hotuba yake nzuri aliyotoa tarehe 6 mwezi huu katika Bunge lako Tukufu. Bajeti ambayo imeonyesha muelekeo wa Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuchangia kwangu nitajielekeza katika maeneo makuu matatu. Eneo la kwanza ni Eneo la kilimo, eneo la pili ni migogoro ya ardhi, tatu ni ujenzi au uwekezaji katika balozi zetu za nje ya nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze na Sekta ya Kilimo. Ni kweli kwamba tunafahamu sekta hii ya kilimo imeajiri Watanzania nguvu kazi zaidi ya asilimia 65, na asilimia 90 ya walioajariwa katika sekta hii ni wakulima wadogo na wa kati ambao bado hawana uwezo wa kupata mikopo katika Benki mbalimbali ikiwemo Benki yetu ya Kilimo. Kwa hiyo, wanategemea sana ruzuku ya Serikali ili waweze kuendeleza shughuli zao za kilimo. Maana yake nini? Maana yake ni kwamba wakulima wetu wengi wanafanya kilimo cha kujikimu; kilimo cha chakula tu, lakini siyo kilimo cha biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kuna kazi kubwa sana inatakiwa ifanyike ndani ya Serikali kuhakikisha kwamba wakulima wetu wanawezeshwa ili wafanye kilimo chenye tija, kwa maana ya kilimo cha chakula pamoja na kilimo cha biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wote tunafahamu, takwimu zinasema Sekta ya Kilimo inachangia karibia asilimia 27 pato la Taifa, pia inachangia zaidi ya asilimia 60 ya malighafi viwandani, lakini mauzo ya nje ya nchi ni takribani Dola za Kimarekani bilioni 1.2 kwa mwaka. Sekta hii ndiyo inayolisha asilimia 100 ya chakula hapa nchini, kwa hiyo, ni sekta muhimu katika maendeleo ya Taifa letu na mustakabali mkubwa wa wananchi wetu. Hata hivyo, sekta hii inakua kwa wastani wa asilimia nne hadi tano kwa mwaka. Kwa hiyo, kuna kazi kubwa sana ya kufanyika ndani ya Wizara ya Kilimo ili tuweze kuwakwamua wananchi wetu katika sekta hii muhimu. (Makofi)

Mheshimu Naibu Spika, kwa maana hiyo basi, kuna umuhimu mkubwa sana kuwekeza katika sekta hii muhimu ya kilimo. Tuna mpango wetu wa Taifa wa Uchumi Shirikishi. Bila kuwekeza kwenye kilimo itakuwa ni ndoto kufikia uchumi shirikishi. Najua Waziri wetu wa Kilimo ana mipango mizuri sana kwenye sekta hii, namwomba sana aangalie sekta hii kwa jicho la pili ili kuhakikisha kwamba tunafikia uchumi shirikishi kwa kuiwezesha sekta hii ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mazingira haya basi, kazi kubwa ya Serikali ni kuandaa mazingira, maana tunaamini Serikali pekee haiwezi kufanya kazi hii ya kilimo lazima tushirikishe na sekta binafsi. Tuna mfano mzuri wa nchi yetu ya jirani hapo Zambia, Zambia leo kuna sekta binafsi imewekeza sana kwenye kilimo na kilimo kimefanikiwa sana. Kwa hiyo, nitoe wito kwa Serikali kuandaa mazingira mazuri ya kuwezesha sekta binafsi kushiriki katika suala zima la kilimo hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tukiangalia sekta mbalimbali, sekta kama ya nishati pamoja na miundombinu, zinachangia sana katika pato la Taifa, ni kwa sababu Serikali imewekeza. Kwa hiyo, hata sekta ya kilimo hii ikiwezeshwa, basi inaweza ikachangia kwa kiasi kikubwa sana kwenye pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lazima Serikali ielekeze kwenye kuwekeza kwenye sekta za uzalishaji. Manufaa ya uzalishaji ni kama ifuatavyo: moja, unaongeza ajira kwa Watanzania, unaongeza malighafi za viwandani, unakuza biashara ya nje na ya ndani; na kupanua wigo wa kodi. Tumekuwa tukilalamika kwamba walipa kodi tunawarudia wale wale; tukiweza kwenye sekta za uzalishaji ni wazi kwamba tutapanua wigo wa walipa kodi na baadaye Serikali ipate mapato ya kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu sasa kwenye sekta hii ya kilimo, kwanza kama nchi lazima tujielekeze kwenye uzalishaji na siyo kwenye matumizi. Mambo ya kufanya ni kama ifuatavyo: Moja, ni kujenga au kuendeleza miundombinu ya umwagiliaji ili kuwe na kilimo cha msimu wote wa mwaka; la pili, lazima tuainishe maeneo maalum ya kilimo na aina ya mazao katika maeneo husika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakumbuka kulikuwa na crop map hapa nchini, ni vizuri sana tukaifuata ili tuweze kuzalisha, tuwe na maeneo mahsusi kwa ajili ya mashamba, pia tuwe na aina ya mazao husika. Eneo lingine, lazima tuboreshe utafiti ili tuweze kuzalisha mbegu bora hapa nchini. Leo hii tunalia kilo moja ya mbegu ni Shilingi 12,000/=; gunia la mahindi ni Shilingi 20,000/=. Haileti tija kabisa! Kwa hiyo, kuna haja kubwa sana ya kuendeleza utafiti na hatimaye kuzalisha mbegu bora hapa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni kutafuta masoko ya uhakika kwa mazao ya wananchi wetu. Nitatoa mfano, Mkoa wa Manyara au Babati Vijijini kuna mashamba makubwa ya mbaazi, lakini wakulima wanalima na baada ya kuvuna, hawana pa kuuza. Kwa hiyo, naomba sana Serikali itafute masoko ya uhakika ya mazao yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni kuwa na mfuko maalum wa kuwalinda wakulima wetu hasa wakati bei za pembejeo zinapopanda na wakati bei za mazao yao zinavyoshuka. Mfuko utawasaidia sana wananchi wetu kujikumu na kuendelea na kilimo cha uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni kujenga maghala ya kutosha ili kuokoa upotevu wa mazao. Taarifa inasema kuwa tunapoteza karibia asilimia 30, postharvest loss. Nina imani kubwa sana kwamba tukijenga maghala ya kutosha, basi hili litapungua sana. Kwenye eneo hili, naipongeza sana Serikali, imejenga maghala kule Babati, Sumbwawanga na maeneo mengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili ni migogoro ya ardhi kati ya wawekezaji na wananchi wetu. Naipongeza Serikali, iliundwa timu ya Mawaziri nane, walizunguka nchi nzima kutatua migogoro hii, lakini bado kuna migogoro katika maeneo yetu kati ya wawekezaji na wananchi wetu. Kwa hiyo, naiomba sana Serikali, bado kuna changamoto hii ya migogoro kati ya wawekezaji na wananchi wetu na katika maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, natambua sana Sera ya Uwekezaji ni nzuri, inaleta ajira kwa Watanzania, lakini pia inaleta mapato kwa maana kulipa kodi ya Serikali. Nitatoa mfano, kule kwangu Babati kuna migogoro kati ya Kata ya Kiru kule Magara, lakini pia kiwanda cha Minjingu na wananchi wa vijiji vya City na Minjingu. Kwa hiyo, naiomba Serikali ijielekeze katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ni kati ya Hifadhi na Vijiji vyetu. Natambua kazi kubwa ya Serikali iliyofanya kutatua migogoro kati ya Hifadhi za Taifa na vijiji, lakini bado changamoto ipo. Naiomba sana Serikali, Mawaziri washirikiane na Wabunge ambapo sisi ndiyo wawakilishi wa wananchi, ndio tunajua migogoro iko wapi? Tukishirikiana kwa pamoja, naamini tukienda pamoja, basi migogoro hii itapungua au itakwisha kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la mwisho ni ujenzi au uwekezaji katika Balozi zetu nje ya nchi. Natambua Balozi zetu zina viwanja vingi nje ya nchi; na ninaipongeza Serikali imeanza kujenga katika Balozi zetu kule Oman, lakini bado kuna viwanja havijaendelezwa. Nitatoa mfano kwa nchi ya Zambia. Zambia kwenye Balozi yetu kuna viwanja karibia nane na vipo kwenye very prime area. Kwa hiyo, nadhani tukijenga humo tutapata fedha za kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna njia tatu; kuna mortgage financing, kuna mifuko yetu ya kijamii na PPP. Serikali ikijielekeza huko tutapata fedha…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Haya, sekunde tatu malizia.

MHE. DANIEL B. SILLO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nashukuru kwa nafasi hii, naunga mkono hoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)